Na Albano Midelo
TANZANIA
ni nchi pekee katika Afrika mashariki ambayo imebahatika kuwa na vivutio vya
kipekee ambavyo huwezi kuviona katika sehemu nyingine yeyote duniani.
Tanzania
ina maliasili mbalimbali kama vile maziwa, Bahari ya Hindi, milima, wanyama
pori,mambo ya kale,mawe ya ajabu ,vimondo ambavyo vimedondoka toka angani
pamoja na vivutio vingine vingi.
Nchi yetu
imebahatika kuwa na maziwa mengi kuliko nchi yeyote katika bara la
Afrika.Maziwa hayo ni pamoja na ziwa Viktoria,Tanganyika,Nyasa,Rukwa na maziwa
mengine madogo.
Maziwa
hayo yote licha ya kuwapatia wananchi wake kitoweo na kipato kutokana na samaki
wanaovuliwa ,pia ni kivutio kikubwa cha
utalii.
Ziwa Tanganyika lililopo magharibi mwa nchi ni
miongoni mwa kivutio cha utalii.Ziwa
hilo lipo katika mikoa ya Kigoma na Rukwa na kuelekea hadi katika nchi jirani
za Kongo DRC na Burundi.
Ziwa
Tanganyika ni ziwa lenye sifa za kipekee sio tu katika Tanzania bali hata
ukilinganisha na maziwa mengine ulimwenguni hakuna ziwa ambalo linafanana na ziwa
Tanganyika.
Ziwa
Tanganyika lina sifa kuu nne ambazo pamoja na kuwa ziwa refu kuliko maziwa yote
ulimwenguni likiwa na urefu wa kilometa 673 kutoka kaskazini hadi kusini mwa
ziwa hilo.
Sifa
nyingine ya ziwa Tanganyika ni kuwa na kina kirefu kwenda chini.Ziwa hilo
linashika nafasi ya pili kwa kina kirefu ulimwenguni baada ya nafasi ya kwanza
kuchukuliwa na ziwa Baikar ambalo lipo
katika nchi ya Rusia.
Kina cha
ziwa Tanganyika ni kilometa 1.47 au meta 1470
hivyo ziwa hilo kuwa na kina cha kipekee ambacho ni kivutio cha utalii
kianchoweza kuwasukuma watalii kufika
katika ziwa hilo kuona maajabu hayo.
Ziwa hilo
linawashangaza wengi kwa ukubwa na ujazo wake ambao ni kilometa za ukubwa 18,900
na kwamba ziwa hilo linachukua asilimia 17 ya maji yote baridi ulimwenguni.
Kana
kwamba haitoshi ziwa Tanganyika lina utajiri mkubwa wa viumbe hai wa aina mbalimbali wakiwemo
samaki,mamba,viboko pamoja na viumbe wengine wa majini.
Watu
wanaotaka kujifunza kupitia ziwa hilo wanapata fursa ya mambo mbalimbali ya kibaiolojia na kiuchumi
hasa kutokana na samaki wa aina
mbalimbali waliomo katika ziwa hilo.
Ziwa
Tanganyika lina aina za samaki zaidi ya 400
na kati ya aina hizo za samaki
kuna aina ya samaki ambao wana uwezo wa kutoa umeme wanaofahamika kwa jina la
electric fish haya ni maajabu mengine ya
dunia ambayo yanawashangaza wengi.
Kutokana
na sensa ya samaki ya mwaka 1999 ziwa Tanganyika linakadiriwa kuzalisha samaki
kati ya tani 165,000 hadi 200,000 zenye thamani ya dola za kimarekani milioni
80 hadi milioni 100.Miongoni mwa samaki maarufu katika ziwa hilo ni
dagaa,migebuka,kambale,sangara,magege,samaki wa mapambo,singidae na kuhe.
Mhifadhi
wa kutoka hifadhi ya Gombe Noelia Mnyonga ambaye analifahamu vyema ziwa Tanganyika,
akizungumzia samaki ambao wanatoa
umeme,anabainisha kuwa aina hiyo ya samaki wanatoa umeme pale wanaposogelewa na
adui hivyo kuwa kivutio adimu na cha kipekee ulimwenguni.
“Samaki
huyu kwa kuwa anatoa umeme iwapo angetangazwa ndani na nje ya nchi watalii
wengi wangemimika kwenda katika ziwa Tanganyika ili kwenda kumuona na hivyo
serikali kupata kipato kikubwa”,anasisitiza Mnyonga.
Anaongeza
kuwa watalii hao baada ya kusikia habari za samaki anayetoa umeme hakuna ubishi
wangependa kufika ziwa Tanganyika na kuona samaki huyo anatoaje umeme na kwamba
aina hiyo ya samaki haipatikani katika maziwa mengine duniani zaidi ya ziwa
Tanganyika.
Baadhi ya
watalii wanapenda kujifunza maisha ya viumbe wa majini akiwemo samaki huyo
anayetoa umeme hivyo wanapopata fursa ya kufika katika maziwa kama ziwa Tanganyika wangependa kufanya
utafiti wa aina mbalimbali za samaki na kufahamu aina na tabia za samaki.
Ukiachia
samaki huyo anayetoa umeme,ziwa Tanganyika pia lina aina nyingine za samaki
wakiwemo dagaa maarufu wa kigoma.Katika miji ya Kigoma na Sumbawanga wakazi katika miji hiyo wanafanya biashara ya
dagaa hao wanaovuliwa katika ziwa Tanganyika.
Biashara
ya dagaa kutoka ziwa hilo endapo itaboreshwa
na wadau wake kujipanga vizuri dagaa hao wanaweza kuleta maendeleo
makubwa kwa wananchi na kuinua maendeleo yao kiuchumi.
Hata
hivyo baadhi ya wakazi katika miji hiyo wanapeleka dagaa hao katika nchi za
jirani ikwemo Kongo DRC,Burundi na Zambia katika kiwango ambacho hakitoi mapato
makubwa.
Mhifadhi
wa ziwa Tanganyika anatoa wito kwa serikali kutoa fursa kwa wawekezaji kuwekeza
katika ziwa hilo kwa kujenga viwanda vya kusindika dagaa ili hatimaye dagaa hao
waweze kupelekwa kuuzwa nje ya nchi katika viwango vya kimataifa ili kutoa
faida kubwa zaidi .
Ziwa
Tanganyika lingeweza kuwasaidia wananchi wanaoishi katika ziwa hilo hususani
mikoa ya Kigoma na Rukwa endapo wangejiunga katika vikundi na kupata mtaalamu
ambaye angewafundisha mambo ya kitalii na kufanya utalii wa uvuvi.
Vikundi
hivyo kupitia utalii wa uvuvi wangeonyesha njia
zao za asili za kuvua samaki,upikaji wa samaki kwa njia ya asili ,uhifadhi
wa samaki kwa njia ya asili hivyo kuwavutia watalii kuona hatua mbalimbali za uvuvi wa
asili.
Watalii
wengi hawajaona njia za asili za kuvua,kupika na kuhifadhi samaki kutokana na
ukweli kuwa wao wamezoea kuvua samaki kwa kutumia mitambo maalum.
Wananchi
wanaozunguka hifadhi ya ziwa Tanganyika wanaweza kufaidika na uvuvi wa kitalii
na kwamba pato watakalolipa watalii hao litakwenda moja kwa moja katika
serikali za vijiji au vikundi vyao.
Kwa kuwa
tayari watalii watakuwa wamefika katika hifadhi hiyo ya ziwa Tanganyika,pia
wananchi watapata fursa ya kuuza samaki hao kwa watalii huku wakionyesha
utamaduni wao kwa ngoma za asili ambapo watalii watatozwa fedha za kuangalia
utalii huo wa kiutamaduni na kujiongezea kipato.
Hata
hivyo mkuu wa mkoa wa Rukwa Injinia Stella Manyanya ameshauri kuimarisha ushirikiano baina ya nchi jirani za
Kongo DRC , Burundi na Tanzania ili kulifanya ziwa Tanganyika kuwa na matumizi
endelevu kwa kuwa ziwa hilo limezungukwa na nchi hizo.
Ameshauri
mabalozi katika nchi hizo wasaidia kuunganisha utalii kutoka katika nchi zote
sanjari na kuboresha mazingira ya ziwa Tanganyika ili kuwalinda viumbehai
waliomo ndani ya ziwa ziwa hilo.
Hata
hivyo uchunguzi umebaini kuwa kina cha ziwa Tanganyika kinapungua mwaka hadi
mwaka kutokana na uharibifu mkubwa wa mazingira
ambao unaendelea kufanywa kutokana na shughuli mbalimbali za kibidamu.
“ Watu
wanakata miti ovyo kwenye hifadhi ya ziwa Tanganyika,vyanzo vya maji
vinavyotiririka kuelekea kwenye ziwa hilo vimeharibiwa katika kiwango
kinachotisha hivyo kuathiri ziwa hilo ambalo ni muhimu kwa uchumi wa
Taifa’’anasisitiza mhifadhi wa ziwa hilo.
Anashauri
wadau wote wa mazingira katika nchi zinazozunguka ziwa Tanganyika kuungana kwa
pamoja katika kulinda mazingira ya ziwa Tanganyika hasa kuhamasisha kupanda
miti katika maeneo mbalimbali hivyo kufanya ziwa Tanganyika kuwa endelevu.
albano.midelo@gmail.com,simu 0766463129.
No comments:
Post a Comment