Monday, May 21, 2012

TANAPA yawazawadia waandishi bora Tanzania

  
 Na Mwandishi maalum
HIFADHI za Taifa Tanzania TANAPA imetoa zawadi ya shilingi  milioni  10 kwa waandishi bora wanane wa habari za utalii nchini.
Waandishi hao ni wale walioshinda tuzo za uandishi bora wa habari Tanzania zilizotolewa na Baraza la habari Tanzania MCT na kutangazwa rasmi Aprili 30 mwaka huu kwenye ukumbi wa Diamond Jubilee jijini Dar es salaam mbele ya mgeni rasmi Rais Jakaya Kikwete.
Waandishi hao kutoka vyombo mbalimbali vya habari nchini walikabidhiwa hundi za fedha zao kati ya shilingi laki tano hadi milioni moja na nusu na kaimu mkurugenzi mkuu wa TANAPA Ahmed Mbugi katika hafla fupi iliyofanyika kwenye ukumbi wa TANAPA mjini Arusha.
Meneja uhusiano wa TANAPA aliwataja waandishi hao kuwa ni pamoja na Albano Midelo mwandishi wa habari wa kujitegemea ,Iman Mant gazeti la Dairynews,Juma Nugaz wa  Clouds Television  na Gordon Kalulunga mwandishi wa kujitegemea.
  Wengine ni Monica Luwondo  mwandishi wa The Guardian,Cassius Mdami mwandishi wa Channel Ten television,Alex Mwagwiza shirika la utangazaji Tanzania TBC,Joseph Zablon gazeti la Mwananchi na Paul Sarwatt wa gazeti la Raia mwema.
Aidha TANAPA katika kuhakikisha kuwa ina watia moyo wanahabari kuandika habari za utalii,imegharamia safari za kujifunza kwa waandishi hao kwenda nchini Afrika ya kusini kwa wiki moja lengo likiwa ni kuangalia namna utalii wa ndani ulivyofanikiwa katika nchi hiyo ambayo ina idadi kubwa ya watalii wa ndani ukilinganisha na watalii kutoka nje ya nchi.
Akizungumza mara baada ya kukabidhi hundi za fedha kwa waandishi hao,kaimu mkurugenzi wa TANAPA Ahmed Mbugi amesema sekta ya utalii ni muhimu hapa nchini kwa kuwa inachangia asilimia 17 ya uchumi wa Taifa.
Amewashauri wanahabari nchini kuvitangaza vivutio vya utalii vilivyopo nchini ili viweze kufahamika vizuri ndani na nje ya nchi na kwamba wanahabari wanaweza kusaidia kuiboresha sekta hiyo kutokaka na jamii kuviamini vyombo vya habari hivyo kusababisha idadi ya watalii kuongezeka mwaka hadi mwaka.
“Nawahakikishieni TANAPA ipo tayari kushirikiana na wanahabari,tupeni taarifa mapema tunazo hifadhi za Taifa nyingi ambazo zinavivutio vya aina mbalimbali wakiwemo wanyama,ndege,mimea na viumbe wengine kwa kutumia kalamu zenu mnaweza kuwaelimisha wananchi wakatambua umuhimu wa utalii na kutembelea maeneo yenye vivutio’’,alisema.
Alizitaja hifadhi za Taifa zilizopo nchini kuwa ni pamoja na hifadhi ya Taifa Arusha, Gombe, Katavi, Mahale,Mikumi,Ziwa Manyara, Ruaha ,Rubondo,  Serenget,Saadan,Tarangire,Udzungwa,Kitulo,Mkomazi, Saanane na mlima Kilimanjaro.
Wakizungumza mara baada ya kukabidhiwa hundi zao waandishi hao wameipongeza TANAPA kwa kutambua mchango mkubwa unaofanywa na waandishi wa habari nchini na kwamba kitendo hicho kimewapa nguvu ya kujituma zaidi katika kuandika habari za utalii nchini.
albano.midelo@gmail.com

No comments:

Post a Comment