Tuesday, May 22, 2012

Shule ya Mkapa haina nyumba za walimu


  
Mwalimu mkuu wa shule ya msingi Mkapa Hans Mwailima

Na Albano Midelo
KATIKA hali isiyokuwa ya kawaida shule ya msingi Mkapa  iliyopo  katika kata ya Rwinga wilayani Namtumbo mkoani Ruvuma ambayo imepewa jina la Rais mstaafu Benjamin Mkapa haina nyumba hata moja ya walimu.
Mwalimu mkuu wa shule hiyo Hans Mwailima alisema kuwa shule hiyo ina walimu 11 lakini hakuna nyumba hata moja ya mwalimu hali ambayo imesababisha walimu kuhangaika kupanga nyumba kwa wanakijiji ambazo hazipatikani kwa urahisi na kusababisha kero kubwa kwa walimu.
“Sijawahi kuona shule inakosa hata nyumba ya mwalimu mkuu,lakini hapa licha ya shule yetu kupewa jina la Rais mstaafu Benjamin Mkapa shule ina matatizo makubwa katika miundombinu yake kwa kuwa hata vyumba vya madarasa vilivyopo ni  vinne tu inakatisha tamaa’’alisisitiza.

Baadhi ya walimu wanaofundisha katika shule hiyo wakizungumzia kero hiyo ya nyumba za kuishi walidai kuwa inawakatisha tama kwa kuwa wamelazimika kupanga kwa wanannchi ambao wengine wana nyumba zilizoezekwa kwa  nyasi hivyo mwalimu kuishi katika nyumba ambazo hazina viwango.
Waemtoa wito kwa kamati ya shule hiyo kwa kushirikiana na serikali kuhakikisha kuwa walimu wa shule hiyo wanajengewa nyumba bora haraka ili waweze kutimiza majukumu yao ya kufundisha wanafunzi kwenye mazingira yanayovutia kwa walimu na wanafunzi.
Uchunguzi umebaini kuwa moja ya sababu kuu zinazochangia kuzorotesha maendelea katika shule hiyo ni mgongano wa sera  katika siasa kwa kuwa uongozi ni wa vyama viwili vya CCM na CUF vyenye itikadi tofauti vinavyochangia kukataza baadhi ya kazi za kujitolea kama vile kuwa na benki tofali kwa ajili ya miradi ya maendeleo.
Mkuu wa shule ya msingi Mkapa Mwailima anasema wakazi wa  eneo hilo hawataki kushiriki katika kazi za kujitolea hasa ufyatuaji wa tofali hali ambayo inasababisha serikali kupitia ofisi ya mkurugenzi kushindwa kuwasaidia vifaa vya viwandani kama mabati na saruji.
Uchunguzi umebaini kuwa  tatizo la nyumba za kuishi  lipo karibu katika shule zote saba zilizopo katika kata ya Rwinga mjini Namtumbo ambapo katika shule ya msingi Kidugalo  kuna nyumba moja tu ya mwalimu kati ya mahitaji ya nyumba 13.
Mratibu elimu kata ya Rwinga Thomas Komba amezitaja shule nyingine zinazokabiliwa na upungufu mkubwa wa nyumba za walimu kuwa ni Rwinga,Selous,Minazini na Mandepwende.
Hata hivyo makamu mwenyekiti wa Halmashauri ya wilaya ya Namtumbo Kassimu Ntara amesema anatarajia kuzitembelea shule hizo ili kubaini ukubwa wa tatizo na kushirikiana na mkurugenzi ili kupunguza kero hizo zinazochangia kushusha elimu katika wilaya hiyo.
albano.midelo@gmail.com

No comments:

Post a Comment