KITENGO cha wenye
ulemavu wa akili kilichopo katika shule ya msingi Namtumbo mkoani Ruvuma
kimetelekezwa hali ambayo imesababisha kitengo hicho kubakiwa na watoto watano kati ya 26 walioandikishwa.
Kitengo hicho ambacho
kilianzishwa mwaka 1997 ndiyo kitengo pekee kinachotoa elimu kwa watoto wenye
ulemavu katika wilaya nzima ya Namtumbo kwa kuwa hakuna kitengo wala shule
ambayo inatoa elimu maalum katika makundi mengine ya wenye ulemavu wa wasioona
na viziwi.
Mkuu wa kitengo hicho
Lezile Kampango akizungumza kwa masikitiko makubwa alisema ni dhahiri kitengo
hicho kimesahaulika kwa kuwa tangu alipoletwa katika kitengo hicho mwaka 2005
hadi sasa kitengo hicho hakijawahi kupata fedha yeyote kwa ajili ya chakula
pamoja na mahitaji mengine muhimu kwa watoto hao.
“Huwezi kuamini
lakini ndivyo ilivyo watoto hawa wanashindwa kupata chakula hali ambayo
imesababisha watoto wengi kuwa watoro kwa mfano leo ni watoto watatu tu ndiyo
wamefika shuleni,mimi mwenyewe wakati mwingine nawachukua hadi nyumbani kwangu
kuwapatia chai na chakula changu ili waendelee kusoma,mlemavu bila chakula
hasomi’’,alisisitiza.
Kampango amedai kuwa wananchi na serikali
katika wilaya ya Namtumbo licha ya kitengo cha wenye ulemavu katika
wilaya nzima kuwa kimoja wameshindwa hata kujenga darasa moja kwa ajili ya
watoto hao hali ambayo inamlazimu kuwafundisha wanafunzi hao chini ya mti na
wakati wa mvua anakwenda kuwafundishia katika nyumba yake.
“Natamani kuomba
uhamisho kwenda mahali pengine ili elimu yangu niweze kuitumia katika mazingira
bora na rafiki kwa wenye ulemavu,hebu fikiria mimi nawafundisha wanafunzi chini
ya mti,wakati wa mvua nakwenda kuwafundishia
nyumbani kwangu,nimetoa taarifa kwa wahusika katika ngazi zote lakini
hakuna hatua zilizochukuliwa hadi sasa’’,alisema.
Afisa elimu wa
Halmashauri ya wilaya ya Namtumbo Rhoda Mbilinyi amekiri wilaya nzima kuwa kitengo kimoja tu chenye walemavu wa akili na
kwamba wanafunzi katika kituo hicho wanachanganywa na wanafunzi wengine kwa
kutumia elimu jumuishi na kwamba mfumo huo pia unatumika katika shule nyingine
za wilaya hiyo kwa kuchanganyika na wanafunzi wengine wa kawaida.
Kuhusu ruzuku kwa
wanafunzi wenye ulemavu katika kituo hicho Mbilinyi amesema ruzuku inawajumuisha
wanafunzi wote wa shule ya msingi Namtumbo wakiwemo wenye ulemavu,hata hivyo
amesema ruzuku inayopelekwa ni finyu na haitoshelezi mahitaji ya wanafunzi
wakiwemo wenye ulemavu.
“Ni kweli wanafunzi
wenye ulemavu ili waweze kusoma wanahitaji mazingira rafiki vikiwemo
vivutio,katika kitengo cha walemavu Namtumbo kuna vivutio vichache kama vile
mpira,filimbi,wakati fulani walikuwa wanapata uji,lakini hivi sasa uchangiaji
umekuwa mgumu,tunahamasisha katika kipindi hiki cha mavuno wazazi waanze
kuchangia kwa ajili ya kitengo cha elimu maalum Namtumbo’’,alisisitiza.
Mratibu wa elimu
maalum katika Halmashauri ya wilaya ya Namtumbo
Joseph Chengula amezitaja changamoto ambazo zinakikabili kitengo cha elimu maalumu
kwa watoto wenye ulemavu wa akili Namtumbo kuwa ni pamoja na upungufu wa walimu
watalaamu ambapo katika Halmashauri nzima wapo walimu wawili tu.
Changamoto nyingine
ni kitengo kukosa wafanyakazi wengine kama vile wapishi na walinzi,ukosefu wa
miundombinu,vifaa vya kujifunzia na kufundishia na samani mbalimbali,ukosefu wa
bajeti ya kuendeshea kitengo na kitengo kukosa usafiri .
Kulingana na mratibu
huyo ,kitengo cha walemavu wa akili cha Namtumbo kinakabiliwa na matatizo
makubwa katika majengo ambapo kitengo kina tundu moja la choo kati ya mahitaji ya
matundu matano.
“Kitengo hakina
nyumba hata moja ya mwalimu kati ya mahitaji ya nyumba mbili,hakuna stoo kati
ya stoo mbili zinazohitajika, hakuna bwalo la chakula,jiko,hakuna chumba hata
kimoja cha darasa kati ya mahitaji ya vyumba viwili, hakuna bweni hata moja
kati ya mahitaji ya mabweni mawili na kwamba hakuna ofisi hata moja ya walimu
kati ya mahitaji ya ofisi mbili’’,alisema.
Kulingana na Chengula
Halmashauri ya wilaya ya Namtumbo ina watoto wengi wenye ulemavu wa aina
mbalimbali ambao wanastahili kuwepo shuleni lakini wanakosa fursa hiyo kutokana
na wilaya hiyo kukosa shule kwa ajili ya watoto wenye ulemavu.
Takwimu za mwaka 2011
zinaonesha kuwa katika wilaya ya Namtumbo kuna wanafunzi wenye ulemavu wapatao 181 ndiyo wanaosoma katika shule mbalimbali wakiwemo wenye ulemavu
wa akiri 34,wasioona 18,viziwi 11,walemavu wa viungo 109 na albino tisa.
Hata hivyo takwimu
hizo zinaonesha kuwa kuna wanafunzi wenye ulemavu wapatao 71 ambao walitakiwa
kuandikishwa shule hawasomi wakiwemo wenye ulemavu wa akiri 21,wasioona
mmoja,viziwi 11,wenye ulemavu wa viungo 35 na albino watatu.
Makamu mwenyekiti wa
Halmashauri ya wilaya ya Namtumbo Kassim Ntara anasema Halmashauri hiyo
haijawahi kupata fedha kutoka TAMISEMI kwa ajili ya walemavu pekee isipokuwa
kuna fedha inayoletwa kwa maendeleo mengine ya elimu,afya na huduma nyingine.
Hata hivyo Ntara
anasema katika mwaka mpya wa fedha wa
2012/2013 Halmashauri imetenga kiasi cha shilingi milioni saba kwa ajili ya
kitengo cha walemavu wa akili Namtumbo na kwamba kuna mpango wa kujenga shule
moja ya wenye ulemavu kama ilivyoagizwa na serikali.
Takwimu za shirika la umoja wa mataifa
la kuhudumia watoto ulimwenguni(UNICEF) za mwaka 2002 zilionesha kuwa asilimia
98 ya watoto wenye ulemavu katika nchi zinazoendelea ikiwemo Tanzania
hawapatiwi kabisa elimu jambo ambalo ni hatari kwa walemavu.
Imeelezwa kuwa asilimia hii ndogo
inasababishwa na kuwepo kwa shule chache maalum hapa nchini kwa ajili ya watu
wenye ulemavu,ukosefu wa wataalamu,sera na sheria nyingi za nchi hizo hazitaji moja kwa moja au kutoa utaratibu
mzuri wa kutoa elimu kuhusu wenye ulemavu,ukosefu wa vifaa maalum na muhimu vya
kuwawezesha kusoma pamoja na miundo mbinu duni
isiyokidhi mahitaji ya watu wenye
ulemavu.
albano.midelo@gmail.com,simu 0766463129
No comments:
Post a Comment