Friday, July 20, 2012

Maji yenye sumu yanamaliza watu Nyasa


Na Albano Midelo
  Wakazi zaidi ya  4000 wa kijiji cha Mkili kata ya Ngumbo wilaya ya Nyasa mkoani Ruvuma kilichopo mwambao mwa ziwa Nyasa, wanaathirika na madawa yanayomwaga kwenye mto  Ndumbi ambao maji yake wanayatumia katika shughuli mbalimbali ya nyumbani.

 Wananchi wa kijiji hicho wanategemea mto huo kwa kila kitu ikiwemo maji ya kunywa hivyo sumu zinazomwagwa kwenye mto huo zimeleta athari kubwa ikiwa ni pamoja na  wananchi kuugua magonjwa ya homa za matumbo wakati wote na wengine wameripotiwa kupoteza maisha.

Takwimu zinaonesha kuwa mwaka jana pekee katika kipindi cha mwezi Septemba hadi Novemba watu watano walipoteza maisha katika kijiji cha Mkili baada ya kupata magonjwa ya homa za matumbo yanayotokana na unywaji wa maji yenye kemikali katika mto Ndumbi au kula chakula ambacho kimeathirika na kemikali hizo.


Uchunguzi uliofanywa katika kijiji hicho pamoja na vijiji jirani umebaini athari kubwa zaidi katika kipindi cha kuanzia mwezi Septemba hadi Desemba kila mwaka wakati ambao kina cha maji katika mto huo kinakuwa kimepungua katika kiwango kikubwa.

Sumu zinazomwagwa kwenye mto huo uchunguzi umebaini kuwa zinatokana na   baadhi ya wananchi wanaofanya uvuvi haramu kwa kutumikia kemikali zenye sumu katika mto Ndumbi ambao unamwaga maji yake ziwa Nyasa.Wananchi hao wanategemea mto huo kwa maji ya kunywa,kuoga,kupikia,kumwagilia bustani.

Wananchi wanaoishi kwenye milima ya Livingstone ambako mto Ndumbi unaanzia  wanadaiwa kufanya uharibifu wa kumwaga sumu mbalimbali zikiwemo madawa ya kuulia wadudu kwenye kahawa ambazo ni gramakson,DDT,Blue copper,mbolea ya urea pamoja na sumu za kienyeji aina ya mtunyungu  ambazo zinauwa samaki pamoja na viumbe wengine kwenye mto huo.

Hata hivyo uchunguzi umebaini kuwa wanaoathirika  sio wakazi wa kijiji cha Mkili pekee bali wakazi wa vijiji vingine vya jirani mwambao mwa ziwa Nyasa wanaolazimika kunywa maji ya sumu za kemikali za viwandani na mimea vikiwemo  vijiji vya Ngumbo,Yola,Mbuli,Ndonga,Liwundi na Ngumbo ambao kwa miaka mingi wamekuwa wanakunywa maji ambao sio safi na salama kutokana na kukosa maji ya bomba tangu nchi ilipopata uhuru mwaka 1961.

Tilia Woka ni mkazi wa kijiji cha Mkili  ambaye anaishi eneo la milimani jirani na mto Ndumbi anasema wakazi wa kijiji cha Mahande ndiyo wanaofanya vitendo vya kutia kemikali zenye sumu kwa lengo la kuvua samaki waliopo kwenye mto Ndumbi kila mwaka bila kujali athari ambazo zinajitokeza kila mwaka.

“Wavuvi hao haramu kila mwaka kwa siri wanatia sumu katika eneo la chanzo cha mto kisha dawa hiyo kadri maji yanavyoshuka kuelekea ziwani hujichanganya na kuwalewesha samaki huku wengine wanakufa ,wavuvi hao hufuata mto huo huku wakiwakamata samaki waliolewa na kuwafanya kitoweo”,anasema.

“Wavuvi hawa haramu ni wajanja sana wanawahi asubuhi majira ya saa 12  wakiwa katika kikundi na kuweka dawa kwenye mto Ndumbi ,dawa hiyo inafika ziwani majira ya  kumi jioni,wao hawafiki hadi ziwani wanakuwa wameshapata samaki  kabla ya kufika ziwani,wengi wanaokula samaki hao wanalalamika kuumwa matumbo na tunaomba serikali iongeze ulinzi ili kuwakamata waharifu hawa wanaohatarisha maisha ya wananchi’,anasema Moses Hyera mkazi wa kijiji cha Mkili.

Januari Haule anayeishi kando kando mwa mto Ndumbi, anasema wakazi wa eneo hilo wanaathirika  kutokana na madawa yanayowekwa kwenye mto huo  hasa kuugua matumbo,kupoteza maisha  na mifugo mingi inakufa na kusababisha umaskini mkubwa kwa wakazi wa mwambao mwa ziwa Nyasa

“Mwaka 2010 wavuvi hao haramu waliweka kwa awamu tano dawa hizo zenye kemikali kwenye mto Ndumbi na kuleta athari kubwa hasa kwenye mazalia ya samaki aina ya magege na mbelele ambao wanapenda kuzaliana mahali ambapo maji ya mto yanaingia ziwa Nyasa hivyo wanauwa samaki wengi kwenye mto Ndumbi, samaki wanatoweka hasa mwaka 2010 hali ilikuwa  mbaya zaidi”,anasema.

 Utafiti ambao umefanywa katika mto Ndumbi umebaini kuwa maji yake hayafai kabisa kwa matumizi ya binadamu pamoja na viumbe wengine kwa kuwa yameonekana yana kemikali mbaya za sumu hasa kutokana na kumwaga sumu mbalimbali zikiwemo zile zinazodaiwa kutoka katika mabomba ya maji taka yaliotegwa katika hospitali ya misheni Litembo ambayo yanamwaga maji kwenye mto huo na kuishia ziwa Nyasa.

Mganga mkuu wa kituo cha afya Mkili  Thomas Magulilo anasema maji katika mto Ndumbi hayafai kabisa kwa matumizi ya binadamu na kwamba wananchi wa kijiji hicho waliagizwa kuhakikisha kuwa wanachemsha maji hayo kabla ya kunywa ambapo uchunguzi umebaini kuwa asilimia 99 ya wakazi wa kijiji hicho wanakunywa maji kutoka kwenye mto Ndumbi au ziwa Nyasa bila kuchemsha wala kuweka dawa za kuyatibu kama water guard.

“Asilimia 90 ya watu wanaofika kupima katika kituo hiki cha afya, wanagundulika kuwa na vijidudu vya ugonjwa wa homa za matumbo hivyo hali ni mbaya,katika kijiji kizima hakuna kisima cha maji wala bomba,wananchi tunawaelimisha kuchemsha maji wengi wanadai hayana radha wanaendelea kunywa maji bila kuchemsha”,anasema mganga wa kituo cha afya.

Bosko Ndimbo mkazi wa kijiji cha Mahande anasema katika kijiji hicho watu wengi wanatumia mbolea aina ya urea kuulia samaki kwenye mto huo hivyo mifugo mingi inateketea iwapo inakunywa maji au kula vyakula vilivyochanganywa na mbolea ya urea pamoja na dawa za asili aina ya utupa.

“Mwenyekiti wa kijiji cha Mkili Kisika Mahoya anasema utiaji wa sumu sio tu kwamba unafanyika kwenye mto Ndumbi pekee bali pia unafanyika kwenye mito mingine inayopita katika kijiji hicho inayoitwa Mnywamaji na Chipindi inayomwaga maji yake ziwa Nyasa na kusisitiza kuwa tatizo hilo ni kubwa na linaweza kuleta madhara mkubwa ya kiafya na kimazingira.

Imanuel Kipera ni kaimu afisa mtendaji wa kata ya Ngumbo anasema madawa ya kahawa yalipigwa marufu kutumika hata hivyo baadhi ya wananchi ambao wamezificha dawa hizo ndiyo wanaofanya uvuvi haramu kwenye mito na kuhatarisha maisha ya viumbe hai.

“Mimi kitaaluma ni afisa wa mifugo na kilimo,madhara ya madawa haya kwa samaki ni kwamba kuanzia eneo ambalo unakuwa umemwaga sumu hadi mto unakoelekea viumbe wote wanaathirika kuanzia samaki,mifugo na  watu ambao wanatumia maji hayo,mtu anayekula samaki wenye sumu anaweza kupata magonjwa mbalimbali yakiwemo ya moyo na kansa ambayo hutokea baada ya muda mrefu”,anasema.

Hata hivyo anasisitiza wananchi kupatiwa elimu ili kutambua afya ni jambo bora zaidi kuliko kupata kitoweo na kwamba kuna baadhi ya madawa ya kahawa ya maji ambayo wanayatumia  yana athari na madhara makubwa na kwamba serikali ya kata inachukua hatua za kukabiliana na wavuvi hao haramu ambao wanafanya kazi hiyo kwa siri na hata wengine wanatia dawa hizo usiku.

“Kwa kweli tatizo hili la kuweka sumu kwenye maji ambayo yanategemewa na wakazi zaidi ya 3000 katika kijiji cha Mkili ni zito ,wananchi wengi wanaugua ugonjwa wa homa za matumbo ,baadhi yao wanafariki kila mwaka,kata yetu haina kisima hata kimoja wala bomba tunagemea kupata maji ya mito na ziwa Nyasa,tunaomba serikali yenye nguvu itusaidia”,anasisitiza.

Mganga mkuu wa mkoa wa Ruvuma Dk.Daniel Malecela ameahidi ofisi yake kuendelea kuwaelimisha wananchi umhimu wa kuchemsha maji pamoja na kufuatilia  athari ambazo wanazipata wananchi wa kijiji cha Mkili ambao wanaugua homa za matumbo  kutokana na kutumia maji yenye kemikali tena bila kuchemshwa.

Afisa mazingira mwandamizi kutoka Baraza la Taifa la  hifadhi  na usimamizi wa mazingira(NEMC) Pendo Kundya anasema viuatilifu vyote hatari vinavyohatarisha maisha ya binadamu na vilivyopigwa marufuku kama DDT na BLUECOPER inatakiwa wananchi kutoa taarifa kote nchini badala ya kuendelea kuyatumia madawa hayo kinyemela.

 Utafiti umebaini kuwa madawa hayo yaliomalizika muda wake wa matumizi au kuharibika yameonekana katika maeneo yasiopungua 325 nchini kote ambapo Kati ya kemikali hizo zipo jamii ya madawa hatari yanayopigwa vita ulimwenguni kote kutokana na kuhatarisha afya za binadamu na mazingira ya viumbe hai wote kwa ujumla.




Anavitaja viuatilifu chakavu vya kilimo kuwa ni pamoja na vile vyote ambavyo vinatumika kuuwa  wadudu,wanyama na kuzuia magonjwa ya mazao na mimea yaliyozidi miaka miwili tangu kutengenezwa na kusisitiza kuwa viuatilifu chakavu ni sumu kali iliyopo katika mazingira na inayoathiri afya ya viumbehai wakiwemo binadamu na kwamba wananchi kote nchini wanapaswa kuorodhesha kitaalam na watalamu wenye ujuzi kwa kutumia vifaa maalum vya kinga.
      
Mkuu wa mkoa wa Ruvuma Dr.Christine Ishengoma amewaagiza wakuu wote wa wilaya katika mkoa kusimamia na kuvilinda vyanzo vyote vya maji  pamoja na kuwachukulia hatua kali wote ambao wanabainika wanalima au kufanya uharibifu katika vyanzo hivyo ili kulinda maisha ya viumbehai wote na hasa binadamu.

Hata hivyo uchunguzi umebaini kuwa vyanzo vya maji katika maeneo mbalimbali nchini vimekuwa vikiendelea kufanyiwa uharibifu mkubwa licha ya serikali kupiga marufuku shughuli zozote ambazo zinaharibu vyanzo hivyo.

 Serikali mnamo mwaka 2002 ilipitisha mwongozo wa namna ya kutunza vyanzo vyote vya maji vilivyopo ili visipotee wala kuchafuliwa.Sera hiyo ya maji inalenga kuhakikisha kuwa vyanzo vya maji vilivyopo vinatunzwa,kulindwa na kuendelezwa kwa utaratibu unaozingatia uwiano wa mahitaji ya viumbehai wote wakiwemo binadamu ,wanyama, mimea,wadudu pamoja na viumbe hai wote ambao hawawezi kuishi bila maji.

Ili kuhakikisha kuwa vyanzo vya maji vinatunzwa na kuwa endelevu kwa manufaa ya viumbehai vya sasa na vijavyo ni vema kutotupa wala kumwaga uchafu au kemikali za sumu karibu na vyanzo hivyo,,kutochoma misitu ovyo,kupanda miti inayofaa au miti rafiki kwa maji karibu na vyanzo vya maji,kutojenga vyoo karibu na vyanzo vya maji,kutochimba mchanga au madini ndani  au karibu na vyanzo hivyo pamoja na kutosafishia madini au kitu kingine katika vyanzo.
Mwandishi wa makala haya ni mwanafunzi wa chuo kikuu huria cha Tanzania mwaka wa pili katika shahada ya uandishi wa habari anapatikana kwa simu 0766463129, baruapepe albano.midelo@gmail.com






















No comments:

Post a Comment