Wednesday, August 15, 2012

Mgogoro wa ziwa Nyasa umalizwe bila vita


MGOGORO wa mpaka baina ya Malawi na Tanzania kwenye Ziwa Nyasa, umekuwapo tangu enzi za ukoloni.

Wakoloni, kwa nyakati tofauti, wamekuwa wakigawana ardhi na rasilimali za Afrika baada ya mikikimikiki ya vita na mauaji yasiyozingatia uhuru, haki na usawa wa watu wenye miliki yao!
Hivi ndivyo walivyokuwa wakifanya wakoloni tangu 1884/1885 na baada ya kongamano la kuigawa Afrika kwa utashi wa kibeberu.Afrika iligawanywa na kumilikishwa kwa Wazungu. Watu wa Afrika walinyang’anywa uhuru, utu na heshima yao na kufanywa watumwa kwenye ardhi yao.

Afrika tunayoiona leo, iliwekewa mipaka na wakoloni.
Wakoloni walijigawia maeneo kulingana na utashi wa nguvu zao za kijeshi na kimamlaka katika kutawala na kuvuna rasilimali za Afrika.
Kwa jinsi hiyo, uchambuzi huu unakuja baada ya kufukuta kwa vuta nikuvute juu ya mgogoro wa mpaka baina ya Malawi na Tanzania katika Ziwa Nyasa.
Ubishi wa mpaka baina ya nchi mbili jirani, unatokana na mkataba wa kikoloni uliyoingiwa tarehe 1, Julai mwaka 1890 kati ya Uingereza na Ujerumani maarufu kama Anglo-Germany Treaty.
Mkataba huo unaainisha mpaka wa Malawi na Tanzania kwenye mwambao wa ziwa (mashariki ya ziwa).
Kwa kutumia kipengele cha mkataba huo; Malawi kwa upande wake inadai sehemu yote ya ziwa ni eneo lake.
Kwa upende mwingine, Tanzania inadai kwamba, “mpaka wa ziwani, yaani unaogawa ziwa katikati baina ya nchi mbili, ndio mpaka halisi.”
Dhana hizi mbili, zinazokinzana zimeshachukua sehemu kubwa ya mijadala ya kidiplomasia tangu enzi za Mwalimu Julius Nyerere (Rais wa kwanza wa Tanganyika/Tanzania) na Hastings Kamuzu Banda (Rais wa kwanza na wa maisha wa Malawi).
Marais hawa, kwa nyakati tofauti wamekuwa wakirushiana vijembe vya kisiasa juu ya umiliki wa eneo hilo lenye maji mengi (nyassa/niassa, kwa lugha za wenyeji wa maeneo hayo) na hata kwa zaidi ya miaka 50 sasa hakuna suluhisho la kudumu juu yake.
Haijalishi, hata kama ilishindikana kupata suluhisho enzi zile, sasa ni wakati muafaka suala hilo liwekwe tena mezani kwa utashi wa kisiasa ili kutafuta suluhuhisho muafaka.
Utafiti uliyofanywa na Kanali Fulgence S. Msafiri (wa Jeshi la Wananchi wa Tanzania, JWTZ) na kuwasilisha andiko la utetezi wake wa tasnifu kwenye Chuo Kikuu cha Naval Postgraduate School (Monterey, California) Juni mwaka 2011, unaweza kutumiwa kama msingi wa udadavuzi wa kadhia ya mgogoro baina ya Malawi na Tanzania.
Nimeamua kutumia tasnifu ya Afande Fulgence S. Msafiri kwa kuwa ni andiko lenye sura ya kutafuta suluhisho la mgogoro huu kwa njia zenye manufaa kwa pande zote zinazohusika bila ya kuingia kwenye songombingo za kivita mbazo huleta madhara mengi ya kijamii, kiuchumi na kisiasa.
Vita haiombwi; na ubabe ni ushamba! Kwa jinsi hiyo, nampongeza sana Afande Fulgence S. Msafiri kwa kufanya utafiti uliopelekea kuandikwa kwa tasnifu ya kitaaluma inayoweza kutumika kama nyenzo ya utatuzi wa mgogoro huu.
Afande Msafiri (2011) anaandika kwamba matatizo ya kushindwa kupatikana kwa utatuzi wa kudumu wa mgogoro wa mpaka baina ya nchi mbili (yaani, Malawi na Tanzania) yanatokana na kufeli kwa (1) mawasiliano na (2) ushirikiano.
Mambo haya mawili, yaani mawasiliano na ushirikiano baina ya nchi mbili zenye mgogoro, ni muhimu katika kufanikisha upatikanaji wa suluhisho la mzozo wa mpaka wa Ziwa Nyasa ambalo ni sehemu ya urithi wa Malawi na Tanzania.
Kushindikana kwa mawasiliano kwa sehemu kubwa, kunatokana na taarifa za kihistoria, kulilazimishwa na mfumo wa siasa zilizokuwa zikitumika na nchi hizi.
Enzi za utawala wa Kamuzu Banda aliyedhaniwa kuwa “kibaraka” wa makaburu na Mwalimu Nyerere aliyedhaniwa kuendesha siasa za ujamaa na kuwasaidia wapinzani wa utawala wa Kamuzu Banda; nchi hizi mbili hazikuwa na mawasiliano ya moja kwa moja.
Baada ya mageuzi ya kisiasa yaliyoifanya Malawi kuchukua mkondo wa demokrasia ya vyama vingi mwaka 1993 na ofisi ya rais wa Malawi kuingia kwenye siasa za vuguvugu, suala la mpaka wa ndani ya ziwa haukupewa kipumbele ilhali kwa nyakati tofauti kulikuwapo na rabsha na sintofahamu za hapa na pale baina ya mamlaka za Malawi na Tanzania juu ya umiliki wa maji ya Ziwa Nyasa hali iliyowahi kupelekea wavuvi wa Tanzania kusumbuliwa ziwani walipokuwa wakiendesha shughuli za uvuvi na hali kama hiyo ilitokea kwa upande wa pili (yaani, Tanzania).
Pamoja na ukweli huu, hakukuwa na hatua za makusudi na za kimkakati katika kuhakikisha kwamba mgogoro huo unafanyiwa kazi ya kidiplomasia kwa utashi wa hali ya juu wa kisiasa kwa kuhusisha ngazi muafaka na zinazohusika katika kufufua mawasiliano ya moja kwa moja na ushirikano utakaopelekea kupata muafaka wa kudumu.
Mwaka huu, na hususan kwenye Bunge la Bajeti la 2012/2013, suala la mgogoro wa mpaka baina ya Malawi na Tanzania juu ya Ziwa Nyasa, umeibuka upya na hata kupelekea mamlaka za Tanzania kutoa kauli ya utayari wa kwenda vitani kama Malawi wangekaidi “amri halali” ya mamlaka halali za Tanzania.
Nadhani, ni muafaka kuonesha hapa kwamba mizozo yote ya mipaka duniani aghalabu hutokea baina ya pande mbili zenye masilahi kwenye eneo husika.
Kama mfano, mwaka 1990 Saddam Hussein al-Tikrit aliyekuwa Rais wa Iraq, aliivamia Kuwait kwa madai kwamba sehemu hiyo (yaani, Kuwait) ni jimbo la Iraq!
Ukweli wa kihistoria na kistratejia, Kuwait ni nchi inayoaminika kuwa na kiwango kikubwa cha mafuta yasiyochimbwa chini ya ardhi (huge untapped petroleum reserve).
Vilevile, Ethiopia na Eritrea (nchi iliyojitenga kutoka kwa Ethiopia) ziliingia mara kadha wa kadha vitani kwa mgogoro wa mpaka.
Mifano ni mingi, lakini mfano wa hivi karibuni ni wa muhimu zaidi.
Sudan ya Kusini iliyojitenga kutoka Sudan (lililokuwa taifa la kwanza kwa ukubwa wa eneo katika Afrika), ziliingia vitani kugombea eneo lenye utajiri mkubwa wa mafuta la Abyei (lililopo mpakani baina ya nchi mbili zilizojitenga).
Kwa ujumla, migogoro, mizozo na hata wakati mwingine mapambano baina ya nchi zinazopakana imekuwa ikishuhudiwa duniani kutokana na kushindikana kwa suluhisho la kisiasa juu ya mipaka ya nchi husika iliyowekwa na wakoloni au kwa kushindwa kutafsiri au kuanisha mgawanyo wa uhuru, haki na adilifu wa rasilimali zilizomo kwenye maeneo husika.
Tanzania imekuwa na mgogoro wa mpaka wa Ziwa Nyasa kwa muda wa miongo mitano sasa!
Kwa nini leo; na au kwa nini wakati huu?! Hili ni suala mhimu kwa wapembuzi kujiuliza na kutafakari juu yake.
Nini kilichopelekea serikali (kupitia mamlaka zinazohusika) kulipuka na kukaza misuli ya macho juu ya sakati hili leo ilhali lilikuwapo miaka 50 iliyopita?
Nadhani, ushahidi wa moja kwa moja unatosha kuonesha ni kwa nini. Malawi imeanza utafiti wa gesi na mafuta kwenye eneo lenye mzozo na linalobishaniwa baina yake na Tanzania.
Makampuni matatu (ya kigeni) yalipewa leseni na serikali ya Malawi kufanya utafiti kwenye eneo lenye mzozo.
Ushahidi kutoka kwa wenyeji (upande wa Tanzania) wa meneo yanayobishaniwa wamekuwa wakishuhidia harakati za watafiti kufanya kazi ya kuchunguza utajiri (unaosemekana) wa mafuta na gesi kwenye maji ya Ziwa Nyasa upande wa unaodaiwa wa Tanzania!
Suala kubwa hapa, ni utajiri wa gesi na mafuta! Malawi, kama wanavyosema na kuonesha kwenye vielelezo vya ramani za sasa na za kikoloni, wanadhani kwamba Tanzania inawafanyia “hiana” na kuwaonea husda kwamba, “Ziwa Nyasa (wanaliita Ziwa Malawi) ni mali yao waliyopewa na Mungu.”
Na kwa jinsi hiyo, kufanya utafiti wa gesi na mafuta, ni haki yao; huku Tanzania kwa upande wake ikidai kwamba, “mpaka wake na Malawi ni katikati ya ziwa na rasilimali ya ziwa hilo, lazima itumike kwa mgawanyo unaozingatia uwiano wa nusu kwa nusu ziwani.” Hapa ndipo penye songombingo inayozaa “vuta-n-kuvute” ambayo kama haitashughulikiwa kwa hekima, busara na weledi nchi mbili zinaweza kuingia vitani kwa kila moja kutaka kulinda “heshima na uhuru.”
Binafsi, nakubali kwamba nchi yoyote iwayo, iwe ndogo au kubwa, inahitaji kulinda heshima na uhuru wake! Isipokuwa, bila kujali itikadi za kimtazamo na au kifalsafa, lazima tukubali pia kwamba, “hekima ni uhuru.”
Nchi isiyotumia hekima katika kufanya maamuzi yenye taathira kiuchumi, kijamii na kisiasa kwenye mawanda ya mawasiliano ya watu wa dunia na ushirikiano wa kikanda na kidunia, haiwezi kuwa huru kwa vile itakuwa inajitenga na jamii ya watu wengine wanaoishi kwa kutegemeana.
Hakuna nchi inayoweza kuishi kama “kisiwa” kinachoelea kwenye maji yanayolindwa na samaki wakali na wenye sumu huku watu wengine kutoka maeneo yanayozunguka maji hayo wakizuiliwa kushirikiana na watu wa kisiwa husika!
Binadamu ni kiumbe wa kijamii na kwa jinsi hiyo, ameumbwa awasiliane na watu wengine na ashirikiane nao katika kuendesha maisha yake kiuchumi, kisiasa na kijamii.
Nakumbuka, wakati nikisoma darasa la sita (mwaka 1983), mwalimu wangu mmoja alinisimulia kisa (alichokitafsiri kwa Kiswahili kutoka kwenye kitabu cha Kiingereza cha darasa la sita wakati ule) cha Mkisi mmoja aliyevuka Ziwa Nyasa kwenda kutafuta mbegu ya muhogo Nyasaland.
Nadhani ni ukweli usiyokuwa na shaka kwamba, makabila anuai yanayozunguka Ziwa Nyasa yanapatikana nchi zote zinazozunguka ziwa hili.
Jaribu kuchukua hata mandhari ya pwani zake, upande wa mwambao wa Malawi na mwambao wa Tanzania wananchi, wanaoishi maeneo hayo wanafanana kwa asili yao na shughuli zao.
Mila na desturi za Wanyasa, Wanyakyusa, Wayao, Wamatengo, Wangoni, Wanyanja, Wanyiha na wengineo wanaounda makabila yanayozunguka Ziwa Nyasa, wana asili inayofanana sana na hawawezi kutenganishwa na siasa.
Watu wanaozunguka Ziwa Nyasa wanaishi kwa kulitegemea ziwa hilo tangu maji hayo yalipojikusanya hapo baada ya nguvu za asili za dunia kutengeneza Bonde la Ufa lililofanya bonde kuwapo mahala hapo!
Kwa watu wanaozunguka ziwa hilo (Nyasa), wanalijua ziwa hili kama nyassa (au niassa), ikiwa na maana eneo lenye maji mengi na hata wale waliyeitwa wavumbuzi (waliowatangulia wakoloni) walipokuja na “kuvumbua, sema kuona mara ya kwanza wakiwa Wazungu) waliwakuta watu wa makabila mbalimbali wakilitumia ziwa kwa manufaa ya maisha yao kiuchumi, kisiasa na kijamii.
Ziwa Nyasa, kwa vyovyote vile ni mali ya watu wote wanaozunguka ziwa hilo na si kinyume chake!
Hakuna; narudia, hakuna anayeweza kuwanyang’anya watu wanaozunguka Ziwa Nyasa uhuru na haki yao ya urithi wa asili.
Utashi wa wakoloni na tamaa ya kuvuna rasilimali kunachochea tamaa na uchu uliyopitiliza kwa baadhi ya wanasiasa wasiozingatia hekima na busara ya kutawala siasa katika kutafuta ufumbuzi wa kudumu kwa kuzingatia mwasiliano endelevu na ushirikano wenye tija na ufanisi kwa wale wote wanaohusika katika kujenga mujtamaa wa maelewano yanayozingatia utu, heshima na uhuru ya kila taifa linalohusika kwenye mzozo huu.
Kama mfano, kwenye sakata jingine kama hili; Malawi ilipewa visiwa viwili vya Likoma na Chisamula ambavyo vipo kwenye maji ya ziwa upande wa Msumbiji!
Nadhani, kama isingalikuwa mawasiliano na ushirikano baina ya nchi hizo mbili, sidhani kama hilo lingaliwezekana!
Hapana shaka yoyote kwamba, hata kwa upande wa Malawi na Tanzania inawezekana.
Vita si suluhisho la migogoro ya mipaka; japokuwa baadhi ya watu wanapenda vita! Naandika hivi kwa kuwa kabla sijaamua kulijadili suala hili kwenye kurasa hii ya “Mada ya Wiki” tayari mjadala huu ulishaanza kwenye mitandao ya kijamii kama vile tweeter, facebook, jamiiforums, wanabidii, wanamabadiliko na kwenye kurasa za maoni za magazeti ya kwenye mtandao.
Maoni yanatofautiana; wapo wanaotamani mgogoro huu uishe kwa diplomasia na utatuzi wa kisiasa, wapo wanaodhani kwamba njia muafaka ni kuiadabisha Malawi kwa kuipiga kijeshi, na wapo wanaodhani kwamba suala hili liachwe kama lilivyo kwa sasa kwa kuwa nchi ina matatizo mengi ya kiuchumi na kujiingiza kwenye songombingo za kivita kunaweza kuliingiza taifa kwenye hamkani ya kisiasa kama ilivyokuwa mwaka 1978 wakati wa Vita vya Kagera.
Kama nilivyotangulia kuandika, nadhani suluhisho la Afande Fulgence S. Msafiri (Juni, 2011), linaweza kuwa la kimkakati kama litachukuliwa na kufanyiwa kazi.
Afande Msafiri (2011) anaandika kwamba, mgogoro wa mpaka wa ziwani baina ya Malawi na Tanzania, unaweza kutatuliwa kwa kuzingatia nukta nne (4) kama hivi: Malawi na Tanzania wakutane na kujadiliana na waamue kutafuta suluhu ya mpaka baina yao; nchi zote zifanye kazi kwa pamoja kutekeleza makubaliano ya uchoraji wa mpaka (wa ziwani) kwa mujibu wa kanuni zinazotawala maeneo ya maji (maziwa na mito) yanayozikutanisha nchi na nchi; kila nchi ichukue hatua za kuzuia uharibifu wa maeneo oevu yanayolizunguka ziwa; na Malawi na Tanzania zianzishe muundo wa ushirikiano utakaowezesha kuanzishwa kwa miradi ya pamoja kama vile uzalishaji wa umeme unaotokana na nguvu ya maji na uvuvi.
Kwa asilimia mia moja, nakubaliana na ushauri aliyoutoa Afande Fulgence S. Msafiri (Juni, 2011) na kwa kuongezea ningeshauri yafuatayo katika kupata muafaka wa kiuchumi, kisiasa na kijamii. Tanzania na Malawi zikubaliane juu ya: (1) kuanzisha kamati ya uratibu wa matumizi ya Ziwa Nyasa itakayoshughulikia mawasiliano na ushirikiano wa kirafiki baina ya serikali ya Tanzania na Malawi; (2) Tanzania na Malawi zikubali kuanzisha mamlaka ya bonde la Ziwa Nyasa kwa ngazi ya mikoa inayozunguka ziwa na kuipa mamlaka hiyo wajibu wa kuangalia mgawanyo wa rasilimali za ziwa; na (3) Tanzania na Malawi kwa kupitia kamati za ushirikiano wa kikanda, waanzishe taasisi ya uendelezaji ujirani mwema baina ya makabila yanayozunguka Ziwa Nyasa ambayo kihistoria, ni watu wanaofanana kwa mila na dasturi zao.
Mwisho, napenda kutofautiana na wale wanaodhani kwamba njia pekee ya kutatua mgogoro huu, ni vita!
Kwa kuwa hata nguli wa falsafa ya vita Sun Tzu kwenye kitabu chake cha “The Art of War,” ametahadharisha kwamba, “Generali wa vita anaweza kushinda bila ya kumwaga damu.”
Nadhani ni muafaka, na kwa ujumla, nakubaliana moja kwa moja na Sun Tzu na Afande Fulgence S. Msafiri kwamba, “Tanzania na Malawi wanaweza kumaliza mgogoro wa mpaka kwa njia ya amani na mazungumzo ya kisiasa bila ya kumwaga damu ya wananchi wa pande mbili na kuepusha hasara za kiuchumi, kijamii na kisiasa.”
Vita haviombwi; na ubabe ni ushamba, tutumie vema siasa tumalize migogoro yetu kwa utumizi wa hekima, busara ya hali ya juu na kwa kuzingatia uhuru, haki na uadilifu.
CHANZO;TANZANIA DAIMA



http://www.freemedia.co.tz/images/blank.gif

http://www.freemedia.co.tz/images/blank.gif

http://www.freemedia.co.tz/images/blank.gif
Ltd.

1 comment:

  1. Binafsi, nilipenda kujua ni akina nani ambao Tanzania inawapeleka Malawi kujadiliana kuhusu suala hili. Afande Msafiri ni muhimu awemo katika ujumbe huu, kwani amefanya utafiti kuhusu suala husika. Ningependa kujua waliomo wana uzoefu au ujuzi gani na suala hili, vinginevyo nitasema Tanzania tunafanya mchezo. Kwamba tunafanya mchezo imejidhihirisha pia katika kauli za wale walioongelea vita.

    Ni upuuzi kwa nchi kushindwa kuelewa kuwa suala kama hili la mpaka Ziwa Nyasa, ambalo lina historia ndefu, nyaraka na vielelezo mbali mbali, na pia lenye kugusa sheria mbali mbali, linahitaji utafiti, tafakari na busara, sio kutunisha misuli.

    ReplyDelete