Wednesday, August 15, 2012

Shule ya Luhira mkombozi wa wasioona kusini

Na Albano Midelo
KITENGO cha walemavu wasioona Luhira katika Halmashauri ya manispaa ya Songea mkoani Ruvuma,ndiyo kitengo pekee kwa ajili ya wasioona ukanda wa kusini .
Kitengo hicho ambacho ni ukombozi kwa watoto wasioona nchini kilianzishwa mwaka 1982,hata hivyo shule ya msingi Luhira ni miongoni mwa shule kongwe nchini ilianzishwa mwaka 1929,waziri mkuu wa kwanza wa Tanzania hayati Rashid Kawawa amepata elimu yake ya msingi katika shule hii.

Mkuu wa kitengo cha shule ya wasioona Luhira ambaye pia ni mlemavu wa macho mwalimu Salum Hapendeki anasema kitengo hicho kina wanafunzi 40 wasioona kati yao wavulana ni 20 na wasichana ni 20 na kwamba uwezo wa kitengo hicho ni kuchukua wanafunzi wasioona 60.
“Tunashindwa kuchukua wanafunzi 60 wasioona kutokana na shule yetu ambayo ni ya bweni inakabiliwa na upungufu mkubwa wa vitanda na magodolo,katika mkoa wa Ruvuma pekee kuna watoto wengi wasioona wenye umri wa kwenda shule ambao hawasomi,kwa mfano tulipata maombi ya watoto 14 kutoka Tunduru ili wafike kusoma hapa tumeshindwa kuwachukua tutawalaza wapi?’’,alihoji Hapendeki.
Hata hivyo Hapendeki anaishukuru wizara ya TAMISEMI ambayo inatoa fedha kila mwaka katika Halmashauri ya manispaa ya Songea kwa ajili ya kuendeshea elimu maalum ambapo shule yake inanufaika kila mwezi kwa kupata fedha  za chakula,usafiri na vifaa vya kujifunzia na kufundishia.
“TAMISEMI kupitia Halmashauri ya manispaa ya Songea pamoja na wadau wengine wa elimu kama vile Mamlaka ya Elimu Tanzania TEA inatoa fedha na vifaa kwa mfano katika shule yetu tumepewa fimbo nyeupe za kuongezea wasioona na mashine maalum ya photocopy aina ya thermoform kwa ajili ya wasioona yenye thamani ya shilingi milioni 18 inatusaidia sana’’,alisisitiza.
Hata hivyo mkuu huyo wa kitengo cha wasioona anasema rim ambazo zinatumika kwa ajili ya photocopy katika mashine hiyo ni rim maalum kwa ajili ya wasioona ambazo zinapatikana jijini Dar es salaam pekee kwa shilingi laki tatu bei ambayo ni kubwa ukilinganisha na rim za karatasi za kawaida.
Changamoto nyingine ambazo zinakikabili kitengo hicho ni ukosefu wa umeme wa uhakika hali ambayo inahatarisha usalama wa watoto hao pamoja na walimu kushindwa kutumia vifaa vya kufundishia na kujifunzia vinavyotumia umeme hivyo kuchangia kushusha elimu kwa watoto wenye ulemavu.
Changamoto nyingine ni shule hiyo kukosa uzio hali inayosababisha watu wasiohusika wakiwemo waharifu kuingia,upungufu wa mashine za kuandikia aina ya braili  na shule kukosa mazingira rafiki ya wenye ulemavu wasioona.
Baadhi ya wanafunzi wenye ulemavu wameiomba serikali kuhakikisha kuwa inatoa kipaumbele cha kupatiwa nishati ya umeme wakati wote ili waweze kupata elimu bora na kusisitiza kuwa kwao elimu bora  ni jicho  hivyo ni lazima waipate.
 Langson Mtega mwalimu mlemavu asiyeona anasisitiza kuwa katika mkoa wa Ruvuma kuna idadi kubwa ya watoto wasioona ambao hawasomi hata hivyo walemavu hao wamekosa msaada wa kufikishwa katika shule hiyo ili kupata elimu ambayo ni ukombozi katika maisha yao.

 Kulingana na Mtega changamoto zinazoikabili shule hiyo ya wasioona ni pamoja na uchakavu na upungufu wa vifaa vya kufundishia kwa walemavu hao zikiwemo Braili za kuandikia walemavu hao hali inayoathiri utoaji wa elimu bora kwa walemavu hao.
 Aliitaja changamoto nyingine kuwa ni ukosefu wa nishati ya umeme katika shule hiyo hali inayosababisha vifaa vingi vya kufundishia vinavyotumia umeme kushindwa kutumika.
“Hatuelewi kwanini shirika la ugavi wa umeme nchini TANESCO mkoani Ruvuma linashindwa kutupatia huduma ya nishati ya umeme wa uhakika na kuaminika kutokana na umuhimu wa umeme kwa wenye ulemavu wasioona’’,alisema.  
 Pamoja na changamoto zinazokikabili kitengo hicho,kitaaluma kila mwaka wanafunzi wasioona wanamudu kufanya vizuri mtihani wa Taifa wa darasa la saba kwa mfano mwaka juzi kati ya wanafunzi watano waliofanya mtihani wanafunzi wanne walifaulu na kuchaguliwa kuendelea na masomo ya sekondari na mwaka jana kati ya wanafunzi wawili  waliofanya mtihani wote walichaguliwa kuendelea na elimu ya sekondari.
Ulemavu wa macho unatokana na magonjwa ya  macho ambayo hapa nchini yanatishia ustawi wa jamii kutokana na takwimu kuonesha kuwa idadi ya wagonjwa wenye matatizo ya kutoona na uoni hafifu kuongezeka kwa kasi kubwa.
Kwa mujibu wa takwimu za shirika la Afya Duniani Tanzania inakadiriwa  kuwa na watu 450,000 wasioona na wengine  takriban 1,350,000 wana uoni hafifu.
Kulingana na takwimu hizo duniani kote inakadiriwa kuna takriban watu milioni 30 wenye matatizo ya kutoona na wengine watu milioni 90 wana uoni hafifu.
 Kaimu meneja wa mpango wa Taifa wa huduma za macho Dk.Bernadetha Shilio anabainisha kuwa serikali kupitia wizara ya Afya na ustawi wa Jamii imeridhia dira ya mwaka 2020 ya kutokomeza upofu unaoweza kuzuilika ulimwenguni ifikapo mwaka 2020.
Kwa upande wake Dk.Hassan Rumbe anabainisha sababu zinazosababisha upofu kuwa ni  pamoja na mtoto wa jicho unaosababisha kwa asilimia 50,kovu kwenye kioo cha jicho inayosababishwa na trakoma,upungufu wa vitamin A na surua inasababisha upofu kwa asilimia 20.
Magonjwa mengine ambayo yanasababisha upofu ni magonjwa ya retina kama vile kisukari,umri mkubwa na kwamba mambo yanayosababisha kutoona kwa watoto ni  makengeza,upeo mdogo wa kuona,mtoto wa jicho,maambukizi yatokanayo na magonjwa ya ngono toka kwa mama na  matatizo ya macho ya kuzaliwa nayo.
Hata hivyo cha watu wasioona nchini wametoa rai kwa serikali kuacha tabia iliyozoeleka ya kutumia mabomu ya machozi kwenye maandamano au mikusanyiko ya watu kwa kuwa mabomu hayo yanachangia kuongeza idadi  watu wasioona au wenye uoni hafifu.



















https://mail.google.com/mail/images/cleardot.gif

No comments:

Post a Comment