Na Albano Midelo
RAIS mstaafu Benjamin Mkapa anatamani kila Jumapili kusali
katika kanisa kuu la mtakatifu Kilian la jimbo la Mbinga kutokana na kile
alichoeleza kuwa ni uzuri wa kuhamasisha
na kumotisha uchaji wa Mungu unaofanywa
na kanisa hilo.
Rais mstaafu Mkapa alieleza vionjo vyake kuhusu kanisa hilo
wakati anawahutubia maelfu ya waumini waliofurika katika maadhimisho ya Jubilei
pacha jimboni Mbinga ambapo Rais mstaafu Mkapa alikuwa ni mgeni rasmi.
Akizungumza kwenye sherehe hizo ambazo zilihudhuriwa na
maaskofu kutoka nchi nzima,mapadre,watawa viongozi wa serikali na
mashirika,Rais mstaafu Mkapa alibainisha kuwa licha ya kusali katika kanisa
hilo mara tatu bado hajakifu na anatamani kupata fursa zaidi za kufika kusali
na kuabudu kila Jumapili.
Amelishukuru kanisa katoliki la Mbinga kwa kusaidia kukuza
maendeleo ya kijamii na kiuchumi hali ambayo imesababisha jimbo la Mbinga kupata
mafanikio makubwa yaliyotukuka.
“Kama sio kanisa,ukanda huu wa kusini ungalikuwa nyuma
kielimu,mimi mwenyewe ni tunda la juhudi za kanisa,hata nikabahatika kuingia
kwenye mkondo wa elimu,tutakuwa sio wakweli na tutakuwa hatutendi haki kama
hatutalishukuru kanisa hadharani’’,alisisitiza Rais mstaafu Mkapa.
Kulingana na Mkapa chini ya uongozi wa mhashamu mstaafu Askofu
Dk.Emanuel Mapunda alisimamia eneo la elimu ukiwemo mtandao wa taasisi za malezi na mafunzo
zilizoimarishwa kuanzia chekechea,shule za
awali, msingi, sekondari,vyuo vya VETA,kompyuta na ualimu.
“Kwa namna ya pekee naona heshima ya kuungana na mhashamu
Askofu Emanuel Mapunda ambaye ni ndugu yangu,rafiki yangu na mwanadarasa mwenza
wa miaka ya nyuma tukiwa waseminari pale Kigonsera na tukiwa tunatumia dawati
moja’’,alisema Rais mstaafu Mkapa.
Hata hivyo Rais mstaafu Mkapa alibainisha mwenzake ambaye ni
Askofu mstaafu Mapunda aliendelea na Mungu hadi kufikia uaskofu na yeye wakati huo aliacha malezi ya seminari lakini
hakuthubutu kuyaacha maadili ya dini yake hadi sasa.
Mkapa anasisitiza kuwa historia ya binadamu daima imekuwa na
kipimo kimoja tu cha ufadhili wa kweli ambacho amekitaja kuwa ni huduma kwa
njia ya majitoleo na sadaka.
Kwa upande wake Askofu mkuu wa jimbo kuu katoliki la Songea
mhashamu Norbert Mtega akihubiri katika adhimisho la misa takatifu ya Jubilei
pacha ya miaka 25 ya jimbo la Mbinga amewakumbusha watanzania wakati wanatoa
maoni kwa ajili ya kuandika katiba mpya wasisahau kipengele cha dini kwa kuwa
katiba inakwenda pamoja na Mungu.
“Katiba ambayo haina Mungu ni sawasawa na kutokuwa na
katiba,Mungu ni lazima awekwe mbele katiba haipaswi
kujadiliwa na kundi la watu wachache kwa maslahi yao binafsi, hivyo
ni vyema ikajadiliwa kwa makini zaidi na wananchi wenyewe kwa
kuwa ndio wenye haki,’’,alisisitiza
albano.midelo@gmail.com,simu 0766463129
No comments:
Post a Comment