|
Na Albano Midelo
Hakuna ubishi jamii bado
haijaonesha dhahiri nia ya kulisaidia kundi la wenye ulemavu ambapo hata
idadi ya shule kwa ajili ya wenye ulemavu ni chache ukilinganisha na idadi ya
shule za msingi na sekondari ambazo zinajengwa kwa ajili ya watu wasiokuwa na
ulemavu.
Takwimu kutoka Halmashauri ya
wilaya ya Namtumbo mkoani Ruvuma zilizotolewa hivi karibuni zinaonesha
kuwa wilaya nzima ina shule moja tu ya wenye ulemavu huku watoto wenye ulemavu 71 wenye umri wa
kuanza shule katika wilaya hiyo hawasomi kutokana na ukosefu wa shule za wenye walemavu.
Mchango wa madhehebu ya dini
katika kuhakikisha watu wenye walemavu wanapata elimu ni jambo ambalo
linafaa kuungwa mkono na serikali pamoja na wadau wengine kuhakikisha kuwa
shule hizo ambazo zimeanzishwa zinapata mahitaji yote muhimu wakiwemo
walimu waliopata mafunzo ya kufundisha watu wenye walemavu pamoja na na
vifaa vyote muhimu vya kufundishia na kujifunzia.
Miongoni mwa shule ambazo
zinatoa mchango mkubwa kwa walemavu hapa nchini ni Shule ya msingi
ya mtakatifu vinsenti iliyopo katika Halmashuri ya manispaa ya
Songea mkoani Ruvuma ambayo inahudumia watoto wenye ulemavu katika
kundi la viziwi ambao wana mahitaji maalum kama ilivyo katika makundi mengine
ya walemavu.
Mkuu wa shule hiyo Sr.
Anna Mgaya anabainisha kuwa shule ya St.Vinsenti awali ilianzishwa mwaka 1984
na kanisa katoliki jimbo la Mbinga baada ya kufanyika maafikiano kati ya
kanisa na serikali.
Shule hiyo yenye mazingira
mazuri ya kusomea inahudumia walemavu viziwi kutoka mikoa ya
Ruvuma,Lindi,Mtwara,Mbeya,Rukwa,Iringa na baadhi ya wanafunzi wanatoka jijini
Dar es salaam.
“Makubaliano ya kuanzisha shule
hii yalifanyika baada ya kufanyika utafiti na kugundulika kuwa wapo watoto
wengi viziwi katika kanda ya kusini ambao wanakosa nafasi ya shule baada ya
ukanda mzima wa kusini kutokuwepo kwa shule ya walemavu viziwi”,anasema
Mgaya.
Uongozi wa kanisa
katoliki ukishirikiana na shirika la watawa wa mtakatifu Vinsenti wa Paulo
Mbinga walifanikiwa kupata wafadhili kutoka nchini Ujerumani kupitia chama
cha misaada cha MISERIOR ambao walikubali kugharamia ujenzi wa shule
hiyo ya walemavu viziwi kuwa Songea.
Shule ya mtakatifu
Vinsentu ilipata usajili Januari 15,1989 na kupewa namba RV/01/02/033 ambapo
ilifunguliwa rasmi na waziri mkuu mstaafu hayati Rashid Mfaume
Kawawa Februari 2,1992.
Kulingana na Sr.Mgaya shule
hiyo ina uwezo wa kupokea wanafunzi 200 tu na kwamba kutokana na hali
hiyo Kila mwaka watoto walemavu viziwi wengi wanakosa nafasi ya kujiunga
katika shule hiyo kutokana na shule kukosa uwezo wa kuchukua wanafunzi wengi
zaidi ya hao.
“Idadi ya wanafunzi waliopo hivi sasa
katika shule yetu ni 139 kati yao wavulana ni 74 na wasichana ni 65,ambao
wanasoma kuanzia shule ya awali hadi darasa la saba, shule pia ina
kitengo cha ufundi katika fani za useremala na ushonaji, kuna kitengo cha
ushauri nasaha,upimaji na utengenezaji wa shime sikio,anasema.
Ameyataja mafanikio ya
kuridhisha yaliopatikana tangu kuanzishwa kwa shule hiyo katika nyanja
mbalimbali kuwa ni pamoja na shule kujitosheleza katika majengo na
samani,vifaa vya kujifunzia na kufundishia mazingira mazuri ya kujisomea na
nyumba za walimu zinazokidhi mahitaji ya walimu.
Kwa mujibu wa mkuu huyo wa shule,ufaulu
wa wanafunzi wanaohitimu darasa la saba kila mwaka unaridhisha kwa mfano mwaka 2008 waliohitimu walikuwa 13
waliofaulu ni 13 na mwaka 2010 waliohitimu walikuwa 19 na wote 19
walifaulu kwenda sekondari.
Hata hivyo Sr.Mgaya
anasema shule hiyo inaendeshwa kwa fedha za serikali katika
chakula,usafiri,vifaa vya madarasani licha ya fedha zinazotolewa kutokidhi
mahitaji halisi ya uendeshaji wa shule hiyo.
Anasema Kitengo cha
ufundi katika shule hiyo, kinatoa mafunzo ya awali katika fani za useremala
na ushonaji na kufanya mitihani ya VETA na kupewa vyeti vya ufundi.
Changamoto zinazoikabili shule hiyo
kwa mujibu wa mkuu wa shule ni pamoja na upungufu wa walimu kulingana
na ikama ya walimu wa walemavu,upungufu mkubwa wa watumishi wasiokuwa walimu,ruzuku
inayotolewa katika shule haitoshelezi mahitaji na upungufu wa maji kutokana
na uhaba wa visima.
“ Changamoto nyingine kubwa ni
ukosefu wa umeme wa uhakika hasa wakati wa usiku,nishati ya umeme wakati wa
usiku ni muhimu sana kwa walemavu viziwi wanategemea sana mwanga kwa ajili ya
mawasiliano,utafiti unaonesha kuwa wakati wa usiku bila mwanga
unakuwa umekata mawasiliano kwa walemavu viziwi hivyo kuhatarisha
maisha yao”,anasisitiza.
Hata hivyo anasema shule hiyo
ina watoto 46 wanaoishi katika mazingira magumu kati ya hao 26 ni
watoto yatima ambao hawana msaada wowote hivyo ametoa wito kwa mashirika
binafsi,serikali na wafadhili kuangalia uwezekano wa kuitambua shule
hiyo kuwa kuwa kituo rasmi chenye watoto yatima.
Matarajio ya shule hiyo ni kuanzisha
darasa la kompyuta kwa ajili ya watoto hao walemavu kujifunza somo la
kompyuta ili kuendana na ulimwengu wa sayansi na teknolojia ambao unategemea
teknolojia ya habari na mawasiliano TEHAMA na kwamba tayari kompyuta
zimefungwa katika chumba kimoja cha darasa. .
Sr. Mgaya anabainisha zaidi
kuwa walemavu viziwi wana uwezo mkubwa katika masomo ya vitendo hivyo
wanaweza kufanya vizuri sana katika somo hilo kama ilivyo katika fani ya
ufundi ambapo wanafunzi hao wana uwezo wa hali ya juu.
albano.midelo@gmail.com,simu
0766463129
|
Wednesday, August 8, 2012
Mt.Vinsent shule ya wenye ulemavu inayoongoza kitaaluma
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment