Wednesday, November 21, 2012

Chakula cha mchana chamaliza utoro Nyasa


Na Albano Midelo
UTORO ni moja ya changamoto kubwa inayozikabili shule nyingi za msingi katika wilaya ya Nyasa ambazo zipo mwambao mwa ziwa Nyasa mkoani Ruvuma.
Shule za mwambao mwa ziwa Nyasa zinakabiliwa na utoro unaotokana na sababu mbalimbali zikiwemo wanafunzi kujihusisha na uvuvi,biashara ndogo ndogo,mazingira duni ya kujifunzia na ukosefu wa chakula cha mchana .
Shule ya msingi Mango iliyopo katika kata ya Kihagara wilayani Nyasa ni miongoni mwa shule ambayo kabla ya mwaka 2007 ilikuwa na idadi kubwa ya wanafunzi watoro hali ambayo ilikuwa inachangia kushusha taaluma katika shule hiyo.
Shule ya msingi Mango ni miongoni mwa shule kongwe mwambao mwa ziwa Nyasa ambayo ilianzishwa na kanisa katoliki mwaka 1933 kabla ya kuchukuliwa na serikali,hivi sasa ina wanafunzi 508 kati yao wavulana 275 na wasichana 233.
Mkuu msaidizi wa shule hiyo Marion Mchilas anasema mahudhurio ya wanafunzi hivi sasa katika shule hiyo ni asilimia 97 ukilinganisha na awali ambapo mahudhurio yalikuwa kati ya asilimia 60 hadi 75.
Amesema wazazi na walezi kwa muhula wanachangia mahindi na maharage kwa ajili ya  chakula cha mchana na kwamba mpango huu umepunguza utoro kwa asilimia 30 hivi sasa wanafunzi wanaohudhuria masomo muda wote wakiwemo wanafunzi waliokuwa watoro wa kila siku.
“Katika shule hii wanafunzi wengi wanaishi mbali na maeneo ya shule hali ambayo ilikuwa inasababisha utoro kabla ya kuanzia mpango huu wa kutoa chakula cha mchana shuleni,mtendaji wa kijiji ametusaidia sana kuwahamasisha wazazi na walezi waliokuwa wagumu hivi sasa karibu wote wanachangia’’,alisema.
Anabainisha kuwa kutokana na shule kutoa chakula shuleni kumechangia shule hiyo kufanya vizuri katika taaluma ikiwemo kuwa na matokeo mazuri ya mtihani wa Taifa wa darasa la saba kila mwaka.
Takwimu zinaonesha kuwa shule ya msingi Mango mwaka 2007 wanafunzi waliohitimu darasa la saba walikuwa 62 kati yao wanafunzi waliofaulu walikuwa ni 58,mwaka 2008 shule hiyo ilifaulisha wanafunzi 25 kati ya 30 waliohitimu na kwamba kati ya 25 wanafunzi wanane walichaguliwa kwenda katika shule zenye vipaji maalum.
Kulingana na takwimu za ufaulu katika shule hiyo mwaka 2009 wanafunzi waliohitimu darasa la  saba walikuwa 92 kati yao wanafunzi 75 walifaulu,mwaka 2010 wanafunzi waliohitimu walikuwa  30 kati yao wanafunzi 17 walifaulu na mwaka 2011 wanafunzi 31 walifaulu mtihani wa Taifa kati ya wahitimu 62.
Mchilas amesisitiza kuwa ukaguzi wa shule ambao unafanyika kila mwaka katika shule hiyo kutoka kitengo cha ukaguzi wilaya kumechangia shule hiyo kufanya vizuri kitaaluma ambapo amesema kitengo cha ukaguzi ni muhimu kwa maendeleo ya shule za msingi.
Pamoja na mafanikio hayo mkuu huyo wa shule amezitaja changamoto ambazo zinaikabili shule hiyo kuwa ni pamoja na upungufu wa vyumba vinne vya kusomea kati ya vyumba 11 vilivyopo,upungufu wa walimu wanane,hivi sasa shule ina walimu sita tu.
Changamoto nyingine amezitaja kuwa ni upungufu wa vitendea kazi ambapo shule hiyo ina upungufu mkubwa wa vitabu vya kiada na ziada hali ambayo imefikia darasa moja kuwa na vitabu vitatu kwa kila somo linalofundishwa kila siku yaani Hisabati,Kiswahili na Kiingereza.
Mkuu huyo ameelezea masikitiko yake kwa shule hiyo kongwe ambayo inafanya vizuri kitaalamu,walimu wote katika shule hawana nyumba hali ambayo inawafanya walimu kwenda kupanga uraiani ambako hakuna nyumba nzuri zinazokidhi viwango zikiwemo zilizoezekwa kwa nyasi.
“Shule hii haina hata nyumba moja ya mwalimu,mimi mwalimu mkuu pia sina nyumba ya kuishi,zipo nyumba zinazomilikiwa na kanisa katoliki ambazo zimechakaa,zinavuja, zimebomoka na hakuna mtu anayeweza kuishi,tumewaomba kamati ya shule kwa kushirikiana na serikali ya kijiji watujengee nyumba utekelezaji bado’’,anasema.
Mkuu wa shule ya msingi Nambira Erasmus Haule anasema wanafunzi katika shule hiyo wanapata chakula cha mchana kwa kuchangiana wanafunzi waliotengeneza kikundi cha watu watano ambalo kila mmoja amepangiwa siku moja mzazi wake kuandaa chakula na kuleta shuleni .
Chakula cha mchana katika shule ya msingi Puulu kwa mijibu wa mwalimu mkuu Carthibet Maluka kumesababisha mahudhurio ya wanafunzi kuwa zaidi ya asilimia 95 na shule kufanya vizuri kitaaluma kwa mfano mwaka 2009 waliohitimu darasa la saba walikuwa 89 waliofaulu walikuwa 87,mwaka 2010 walifaulu 65 kati ya wahitimu 68 na mwaka 2011 walifaulu 70 kati ya wahitimu 73
Uchunguzi ambao umefanywa katika shule 10 za msingi katika kata za Liuli na Kihagara umebaini kuwa kuna maendeleo makubwa ya taaluma katika shule ambazo  wanafunzi wanapata chakula cha mchana kwa kujiunga katika vikundi .
Wazazi na walezi wamekuwa wanachangia gharama za kuandaa chakula ambapo kila mmoja amepangiwa siku yake ya kuleta chakula shuleni hali hiyo imesaidia mahudhurio ya wanafunzi kuwa mazuri  kati ya asilimilia 90 hadi 95 kwa siku.
Baadhi ya shule za msingi ikiwemo shule ya msingi Mango,Mwongozo,Nambira,Hongi,Muungano na Kihagara wazazi na walezi baadhi yao wanakataa kuchangia chakula katika shule zao hali ambayo inasababisha watoto wao kukosa chakula cha mchana na kuchangia utoro.
Hata hivyo wazazi na walezi wa wanafunzi wanaosoma katika shule hizo wameshauri  walimu kuzingatia ratiba maalum ya masomo kwa wanafunzi badala ya ratiba ya sasa ambayo wanafunzi wanatumia muda mwingi kufanyakazi za mikono badala ya masomo darasani.
Afisa elimu msingi wa Halmashauri ya wilaya ya Mbinga David Mkali ambaye pia anasimamia wilaya mpya ya Nyasa akizungumzia kuhusu utoaji wa chakula cha mchana katika shule za msingi amesema asilimia zaidi ya 80 katika shule za msingi wanatoa chakula cha mchana kwa wanafunzi.
Amesema hali hiyo imesababisha utoro wa wanafunzi kupungua katika kiwango kikubwa ambapo shule nyingi mahudhurio kwa siku ni zaidi ya asilimia 90 na kwamba wilaya pia imejipanga kukabiliana na sababu nyingine za utoro  ikiwemo baadhi ya wanafunzi kujihusisha na uvuvi ambapo wanatumia sheria na kufanya vikao na wadau katika eneo husika ili kumaliza kabisa utoro.







No comments:

Post a Comment