Saturday, November 10, 2012

Gombe makazi ya sokwe waliyosalia duniani


Na Albano Midelo
 SEKTA ya utalii inachangia pato kubwa la taifa kutokana na uwepo wa vivutio vingi vya utali vilivyopo katika maeneo mbalimbali nchini kama vile hifadhi za Taifa,mapori ya wanyamapori,milima,maziwa,fukwe ,maeneo ya kihistoria, pamoja na vivutio vingine vingi.

Mapato yanayotokana na utalii hapa nchini yanaweza kuongezeka zaidi endapo vivutio vilivyopo vitaboreshwa na kutangazwa kwa nguvu zote ndani na nje ya nchi ili kuwavutia watalii wengi wa ndani na nje.
Matangazo ya vivutio mbalimbali vya utalii  katika vyombo vya habari vya kitaifa na kimataifa yatawezesha vivutio hivyo kufahamika kitaifa na kimataifa hivyo idadi ya watalii kuendelea kuongezeka mwaka  hadi mwaka na kuliingizia taifa mapato makubwa.

Tanzania ni miongoni mwa nchi duniani ambazo zimebahatika kuwa na hifadhi nyingi za Taifa zikiwemo hifadhi ya Taifa Arusha,Gombe,Katavi,mlima Kilimanjaro,Mahale,Mikumi,Ziwa Manyara, Ruaha, Rubondo, Serengeti, Saadan, Tarangire, Udzungwa, Kitulo,Mkomazi na Saanane.


Katika hifadhi za wanyamapori hapa nchini kuna wanyama kama vile simba, tembo, chui, pundamilia,nyati,nyumbu,faru pamoja na ndege wa aina mbalimbali ambao ni kivutio cha utalii ingawa wanyama hao wanapatikana katika hifadhi nyingine duniani.

Ukiachana na wanyama hao Tanzania pia imebahatika kuwa na wanyama wenye kivutio cha kipekee na ni adimu kwa kuwa hawapatikani kirahisi hali ambayo inasababisha wanyama hao kuwa na soko kubwa kwa watalii.

Miongoni mwa wanyama hao ambao hawapatikani kirahisi ni mnyama anayeitwa sokwe ambao hapa nchini wanapatikana kwa wingi katika hifadhi ya Gombe  na milima ya Mahale mkoani Kigoma.

Hata hivyo inaelezwa na watafiti wa wanyama hao ambao wanafanana  na binadamu katika tabia kwa asilimia 98 pengine ndiyo maana wanaitwa sokwe mtu kwamba  hivi sasa sokwe wanatoweka kwa kasi kubwa ulimwenguni hali ambayo inaleta hofu kubwa ya wanyama hao kutoweka na kufutika katika uso wa dunia.

 Watafiti wanabainisha kuwa Sokwe au sokwe mtu ni mnyama ambaye alibakiza asilimia mbili tu angeweza kufanana na binadamu kitabia kwa asilimia 100 ambapo hivi sasa anafanana kwa asilimia 98 hali ambayo inamfanya mnyama huyu kutafutwa kwa udi na uvumba baada ya kuwa kivutio adimu na cha kipekee cha utalii.

Baadhi ya nchi ulimwenguni tayari zimetangaza hali ya hatari kuhusu kutoweka kwa mnyama huyo katika nchi zao ambaye ni kivutio cha kipekee cha watalii hasa kutokana na mnyama huyo kuwa na tabia za kibinadamu.

Kutokana na mnyama huyo kutoweka katika sehemu mbalimbali nchini,Tanzania hivi sasa inapokea watalii wengi ambao wanafika hapa nchini kwa lengo la kumtafuta mnyama huyu na kuweza kumuona katika hifadhi ya Gombe na milima ya Mahale mkoani Kigoma.

Wanyama hao wakiwa katika hifadhi ya Gombe wanaendelea kuzaliana na kuendeleza kizazi chao hasa baada ya wahifadhi na watafiti kuwatunza na hivyo kuendelea kuwepo katika uso wa dunia kwa ajili ya maendeleo ya kizazi cha sasa na kijacho.

Mhifadhi wa wanyamapori Richard Nchasi anasema utafiti wa kisayansi unaonesha kuwa sokwe mtu anaweza kuishi kati ya miaka 40 hadi 50 na kwamba sokwe mtu wanaotunzwa katika bustani maalum wanaweza kuishi hadi miaka 60.

“Sokwe mtu hupevuka anapofikisha umri wa miaka kati ya tisa hadi 13 na huzaa baada ya kufikisha umri wa miaka kati ya 15 hadi 16,uzito wa sokwe mtu ni hadi kilo 120’’,alisema mhifadhi Nchasi.

Kulingana na mhifadhi huyo,sokwe mtu wanaishi kwa kutegemea vyakula ambavyo vinatokana na mimea kama vile ndizi,matango,matikiti,karoti,mchicha na matembele.

Watafiti na wahifadhi wa sokwe katika hifadhi hiyo wanasema wamekuwa wanafanya utafiti wa wanyama hao tangu asubuhi hadi jioni na hivyo kuchunguza tabia zao mbalimbali wanazozionesha.

Mhifadhi kutoka hifadhi ya Gombe Noelia Mnyonga anasema hifadhi ya Taifa ya  Gombe  ni ndogo kuliko zote nchini ikiwa na jumla ya kilometa za mraba 52 tu ,hata hivyo hifadhi hiyo inapata umaarufu mkubwa kwa kuwa na makazi machache  yaliosalia ya sokwe ulimwenguni.

Mnyonga anabainisha kuwa hifadhi ya Gombe ipo umbali wa kilometa 16 kaskazini mwa mji wa Kigoma ikiwa katika ukanda mwembamba wa msitu unaokatizwa na miteremko mikali inayoingia katika mwambao mwa ziwa Tanganyika.

Hata hivyo anasema hifadhi ya Taifa ya Gombe ilipata umaarufu duniani baada ya mtafiti wa tabia za sokwe duniani Dk.Jane Gooddall kufanya utafiti kuhusu maisha na tabia ya sokwe wa Gombe kwa muda wa miaka 40 na kuandika vitabu kadhaa kuhusu wanyama hao.

Mmoja wa  watafiti wa mnyama huyo Issa Salala  anasema kuwa sokwe katika hifadhi hiyo  wakiwa na afya njema wanakuwa wachangamfu,anayataja magonjwa ambayo yanaongoza kuwashambulia sokwe kuwa ni mafua ambayo yanawaathiri sana wanyama na wasipotiwa haraka husababisha vifo kwa sokwe hao.

Hata hivyo anasema kwa kawaida inapogundulika ugonjwa wa mafua umemshika sokwe,watalaamu wa afya za wanyama wanachukua hatua za haraka ili kuhakikisha kuwa mnyama huyo anapata matibabu haraka ili kunusuru maisha ya mnyama huyo adimu ulimwenguni.

Kwa mujibu wa sensa iliyofanyika hivi karibuni katika hifadhi za Gombe,Mahale na Kibondo zimebaini kuwa sokwe mtu katika hifadhi hizo wanafikia 2000 ukilinganisha na idadi ya sokwe mtu karibu 4000 waliokuwepo miaka kumi iliyopita na kwamba sokwe mtu akizaa ananyonyesha kwa miaka miwili na wanazaa kila baada ya miaka minne hadi mitano.

Hifadhi ya Taifa ya Gombe ukiachia kuwa na sokwe,lakini pia hifadhi hiyo ina wanyama wengine wakiwemo kima wenye mikia  myekundu na kima wa bluu hali ambayo inawafanya watalii wanaoingia ndani ya hifadhi hiyo kuwa salama kwa safari za miguu kwa kuwa hakuna wanyama jamii ya paka kama simba na chui.

Kwa upande wa hifadhi ya Taifa ya Mahale iliyoundwa na vilima vilivyojipanga na kufunikwa na misitu minene  ni hifadhi jirani na Gombe na inapakana na ziwa Tanganyika ikiwa na kilometa za mraba 1613 ni hifadhi yenye makazi ya jamii adimu zilizobakia za sokwe barani Afrika.

kaimu mkurugenzi mkuu wa Hifadhi za Taifa TANAPA Ahmed Mbugi anasema katika hifadhi ya Taifa ya Mahale  kundi kubwa la sokwe huonekana katika vilima na mabonde ambapo mabaki ya matunda yaliyoliwa na kinyesi kibichi ni miongoni mwa vitu vitakavyowaongoza watalii hadi kuwafikia viumbe hawa adimu.

“Wakati mzuri wa kutembelea hifadhi za Taifa Gombe na Mahale ni wakati wa kiangazi kati ya mwezi Julai hadi Oktoba kwa kuwa sokwe hawapendi kutembea nyakati za mvua’’,anasisitiza Mbugi.

 Mtalii anaweza kwenda katika hifadhi ya Taifa ya Gombe na Mahale kwa usafiri wa anga,nchi kavu na reli hadi mjini Kigoma kisha kupanda boti kuvuka ziwa Tanganyika hadi makao makuu ya hifadhi hizo.


                     



1 comment: