Monday, November 26, 2012

Mwanamke amuua mtoto na kumzika mwenyewe


Na Albano Midelo
KATIKA hali isiyokuwa ya kawaida mwanamke mmoja Jenista Mapunda (24) mkazi wa Mfaranyaki mjini Songea amejifungua mtoto kisha kumnyonga na kumzika yeye mwenyewe alfajiri ya siku ya Jumapili katika makaburi ya Mfaranyaki.
Watu waliofika kushuhudia tukio hilo la aina yake walimshangaa kwa kuwa na roho ya ukatili hali ambayo pia ilimfanya kuchimba kaburi yeye mwenyewe,kumzika mwanawe na kuweka msalaba wa mti kama ilivyo desturi kwenye maziko .
Kalista Kifaru(38) mkazi wa Mfaranyaki alisema majira ya saa 12 alifajiri aliambiwa na mtoto wake ambaye alipita eneo la makuburi kwamba amemuona mwanamke analia amelala juu ya kaburi  ndipo alitoa taarifa kwa mwenyekiti wa mtaa wa Mfaranyaki Gabriel Ndewele.
Mwenyekiti wa mtaa wa Mfaranyaki Gabriel Ndewele akiwa pamoja na baadhi ya wakazi wa Mfaranyaki walikwenda katika eneo la tukio ambapo walimkuta Jenista akiwa ameishiwa nguvu kutokana na kutokwa na damu nyingi.

Alipohojiwa Jenista alidai kuwa kutokana na ugumu wa maisha  alipojifungua karibu na vyoo vya shule ya msingi Misufini aliamua kumnyonga mtoto wake hadi kufa kisha kumbeba na kwenda kuchimba kaburi na kumzika kwenye makaburi ya Mfaranyaki.
“Nilipojifungua niliamua kumnyonga kubeba maiti kuchimba kaburi mimi mwenyewe kisha kumzika, nilizidiwa pekee yangu niliishiwa nguvu kutokana na kutokwa na damu nyingi,niliamua kulia na kulala juu ya kaburi la mtoto wangu’’,alisema.
Polisi wamethibitisha kuwepo kwa tukio hilo ambapo hivi sasa wanamshikiliwa  mwanamke huyo kwa upelelezi na uchunguzi zaidi.Hata hivyo mwanamke huyo amepelekwa kupatiwa matibabu katika hospitali ya mkoa wa Ruvuma na hali yake inaendelea vizuri.



albano.midelo@gmail.com,simu 0766463129



No comments:

Post a Comment