Monday, December 10, 2012

Mchakato wa Sr.Bernadeta Kufungwa Januari 14,2013



Na Albano Midelo

MCHAKATO wa kumtangaza mtumishi wa Mungu Sr.Bernadeta Mbawala kuwa mwenyeheri ngazi ya jimbo kuu la Songea unatarajia kufungwa rasmi Januari 14 mwakani.

Hayo yamesemwa na msimamizi mkuu msaidizi wa mchakato huo Bro.Regnald Cruz ambaye anamwakilisha Baba mtakatifu wa Roma  aliyewasili jimbo kuu la Songea Jumamosi jioni kwa ajili ya kufuatilia,kukagua na kuangalia hatua mbalimbali za mchakato huo katika ngazi ya jimbo zinavyoendelea tangu kuzinduliwa kwake Januari 26 mwaka huu.

Msimamizi mkuu msaidizi amefurahishwa na kazi nzuri ambayo imefanywa na kamati zote za mchakato wa mtumishi wa Mungu hali ambayo imesababisha mchakato ngazi ya jimbo kukamilika kwa takribani miezi kumi tu badala ya miaka miwili ambayo ilipangwa awali.

Alisema mchakato wa kumtangaza mtumishi wa Mungu ngazi ya jimbo ni mgumu ambao huwa unachukua kati ya miaka miwili hadi mitano kabla ya kukamilika na kufungwa kwa hatua ya juu makao makuu ya Baba mtakatifu Roma.

“Nimeridhika na kazi nzuri ambayo imefanyika katika mchakato wa kumtangaza Sr.Bernadeta Mbawala ngazi ya jimbo,mtumishi huyu wa Mungu amekuwa mtanzania wa kwanza kufanikisha mchakato huu ngazi ya jimbo,naomba endeleeni kusali kwa bidii hadi siku ya kufungwa rasmi mchakato huu Januari 14 mwakani’’,alisisitiza.


Bro.Cruz alisema kamati zote zimefanyakazi  kubwa ambayo imevuka vigezo ambavyo vimewekwa na makao makuu Roma,alitolea mfano wanaotakiwa kutoa ushuhuda ngazi ya jimbo wanatakiwa wawe 30 lakini katika jimbo kuu la Songea watu 52 wametoa ushuhuda na bado kuna watu wengi ambao hawajapata nafasi ya kutoa ushuhuda wao.

Msimamizi mkuu huyo msaidizi  ameipongeza kamati ya habari na mawasiliano kwa kufanyakazi yake vema ya kusambaza habari kupitia magazeti,redio na mitandao ya kijamii hali ambayo imesababisha watu wengi kuelewa kuhusu mchakato wa Sr.Bernadeta hivyo kushiriki kikamilifu na kufanikisha ngazi ya jimbo.

“Nilishangaa nilipofika Dar es salaam nilipowauliza baadhi ya watu kwamba wanamjua mtumishi wa Mungu Sr. Bernadeta Mbawala walinieleza kwa ufasaha kila kitu,nilitambua kuwa hii ni kazi nzuri ya vyombo vya habari  hususan vya kanisa kutoa habari na makala mbalimbali za redio na magazeti,watu wameelewa na sasa mchakato ngazi ya jimbo umefanikiwa kwa wakati’’,alisema.

Hata hivyo alisema baada ya mchakato ngazi ya jimbo  kufungwa rasmi mapema mwezi Januari mwakani,kitakachofuatia ni mchakato wa kumtangaza Sr.Bernadeta Mbawala makao makuu ya kanisa Roma Italia ambako alisisitiza gharama za mchakato zitakuwa kubwa zaidi na kwamba mchakato huo Roma unaweza kuchukua miaka kadhaa hadi kukamilika.

Alibainisha kuwa mchakato ngazi ya jimbo utakapofungwa rasmi Januari 14 mwakani, kamati zitakazoendelea na kazi ni kamati ya fedha na kamati ya habari na mawasiliano na kwamba kamati nyingine za mchakato ambazo ni kamati ya mahakama,Teolojia na Historia zitamaliza kazi siku hiyo ambayo mchakato utafungwa ngazi ya jimbo.

“Watu wenye ushuhuda wanaweza kuwasiliana na kamati ya habari na mawasiliano ,hata hivyo miujiza ambayo inatakiwa kutolewa ushuhuda ni wale ambao wameponywa na mtumishi wa Mungu magonjwa ambayo yameshindikana katika vituo vya afya,ni lazima waonyeshe kumbukumbu za hospitali ambazo zinaonesha walikuwa na magonjwa hayo awali kabla ya kupata miujiza ya kuponywa’’,alisema.

Watu wengine ambao wanaweza kutoa ushuhuda wao kwa mujibu wa Bro.Cruz ni wale ambao wamepata miujiza ya kipekee katika jamii hivyo ametoa wito kwa watanzania wote ambao wamepata miujiza watumie nafasi hiyo  adimu kueleza maajabu ya mwenyezi Mungu katika maisha yao waliyoyapata kupitia Sr.Bernadeta.

Bro.Cruz amekuwa jimboni Songea kuanzia Jumamosi hadi Jumanne wiki hii ambapo ameweza kukutana na kamati zote za mchakato ikiwemo kamati ya habari na mawasiliano,kamati ya Historia, kamati ya Fedha,kamati ya Teolijia na kamati ya mahakama.

Pia alitembelea Abasia ya Peramiho mahali ambapo yalifukuliwa masalia ya Sr.Bernadeta,alitembelea katika kijiji cha Likuyufusi wilayani Songea mahali ambapo mtumishi wa Mungu Sr.Bernadeta Mbawala alizaliwa na kuangalia eneo hilo wananchi wa kijiji hicho wametoa ekari nne ambazo zinatarajiwa  kuendelezwa ikiwemo kujengwa kanisa.

Bro.Cruz pia ametembelea katika kanisa la Chipole ambapo sanduku dogo la masalia ya mtumishi wa Mungu Sr Bernadeta yamehifadhiwa na kanisa kuu la kiaskofu ambapo limewekwa sanduku kubwa la masalia.

Akizungumza wakati anatoa salamu kutoka kwa Baba mtakatifu Jumapili kwa waumini katika kanisa kuu la kiaskofu msimamizi mkuu msaidizi huyo aliwaasa waumini kuendelea kusali kwa bidii hadi hapo utakapofungwa rasmi mchakato ngazi jimbo Januari mwakani.

albano.midelo@gmail.com,simu 0766463129


                                                           

No comments:

Post a Comment