Na Albano Midelo
TANZANIA ni nchi
ambayo imepiga hatua kubwa katika uboreshaji wa elimu ya sekondari ambapo hivi
sasa kila kata kuna sekondari hali ambayo imewezesha watanzania wengi kufikia
elimu ya sekondari.
Hata hivyo pamoja na
mafanikio ambayo yamepatikana tangu serikali ilipoanzisha mpango wa uboreshaji
wa elimu ya sekondari nchini MMES,kuna changamoto mbalimbali zinazozikabili
sekondari za kata hali ambayo inachangia kushusha taaluma bora kwa wanafunzi.
Shule ya sekondari ya
Mango iliyopo kata ya Kihagara wilaya mpya ya Nyasa mkoani Ruvuma ni miongoni
mwa shule za sekondari za kata za serikali ambazo zinakabiliwa na changamoto
lukuki hivyo kuchangia kushuka taaluma.
Shule ya sekondari ya
Mango ilianzishwa mwaka 2006 ina wanafunzi 405 wakiwemo wasichana 185 na
wavulana 220,ina walimu sita tu wanaofundisha masomo ya sanaa hali ambayo
imesababisha wanafunzi wanaosoma katika shule hiyo kufanya vibaya katika masomo
ya Sayansi.
Mwalimu wa taaluma
katika sekondari hiyo Constatine Haule akizungumza kwa niaba ya mwalimu anasema shule inakabiliwa na upungufu mkubwa
wa walimu wa masomo ya Sayansi ambapo masomo yote ya sayansi katika shule hiyo hayafundishwi
kabisa.
“Sekondari yetu
imebahatika kuwa na vitabu vyote muhimu kwa masomo ya Sayansi vikiwemo vya
Hisabati,Biolojia,Fizikia,Kemia,Kompyuta pamoja na vifaa muhimu kwa ajili ya
kufundishia masomo hayo lakini kati ya walimu sita waliopo hakuna hata mwalimu
mmoja anayeweza kufundisha masomo hayo’’,alisema.
Amebainisha kuwa
wanafunzi wengi wanapenda kusoma masomo ya Sayansi na vitabu vipo vya kutosha
lakini hakuna mwalimu wala mtu ambaye anaweza kuwaelekeza na kuwapa wanafunzi
mwongozo wasome nini katika masomo hayo.
Kutokana na hali hiyo
Haule anasema matokeo ya kidato cha nne katika sekondari hiyo ni mabaya na
hayaridhisha ambapo takwimu zinaonesha kuwa wanafunzi waliohitimu kidato cha
nne mwaka 2009 walikuwa 36 kati ya hao wanafunzi saba walifeli,wanafunzi 29
walipata daraja la nne hakuna mwanafunzi hata mmoja ambaye alipata daraja la
tatu,pili na la kwanza.
Matokeo ya mtihani wa
Taifa wa kidato cha nne katika sekondari hiyo mwaka 2010 yanaonesha kuwa
wanafunzi 71 walifeli,wanafunzi 40 walipata daraja la nne,wanafunzi wawili
walipata daraja la tatu hakuna mwafunzi aliyepata daraja la pili na la kwanza.
Mwaka 2011 yanaonesha
kuwa katika sekondari ya Mango jumla ya wanafunzi 72 walifanya mtihani wa Taifa
wa kidato cha nne ambapo wanafunzi 45 walifeli,wanafunzi 24 walipata daraja la
nne,wanafunzi watatu walipata daraja la tatu ambapo hakuna mwanafunzi aliyepata
darala la pili na la kwanza.
Hata hivyo mtaaluma
wa sekondari hiyo anasema shule imejitahidi kitaaluma katika mtihani wa Taifa kwa wanafunzi wa
kidato cha pili ambapo mwaka 2007 wanafunzi 37 walifaulu na wanafunzi saba
walifeli,mwaka 2008 wanafunzi 113 walifaulu na wanafunzi 20 walifeli,mwaka 2009
wanafunzi 82 walfaulu na wanafunzi watano walifeli,mwaka 2010 wanafunzi 98
walifaulu na wanafunzi watatu walifeli ambapo mwaka 2011 wanafunzi 88 walifaulu
na wanafunzi 18 walifeli.
Amesema licha ya
kwamba idadi kubwa ya wanafunzi katika shule hiyo wanafeli,bado kiwango cha
taaluma amedai ni bora zaidi ukilinganisha na sekondari nyingine za kata
zilizopo mwambao mwa ziwa Nyasa ambako kuna mazingira duni ya kujifunzia na
kufundishia.
“Tatizo kubwa
linalochangia taaluma kuwa chini katika shule hii na shule nyingine ni wazazi
na walezi kukosa mwamko wa kielimu,wanafunzi hawajachanganyika kama zilivyo
sekondari nyingine hivyo wanafunzi kubadilika inakuwa ni vigumu’’,alisisitiza.
Amekiri ukaguzi wa
mara kwa mara unafanyika katika sekondari hiyo,hata hivyo alizotaja baadhi ya
changamoto ambazo zinachangia kushusha taaluma kuwa ni pamoja na upungufu
mkubwa wa walimu wa masomo ya Sayansi,wanafunzi wanatoka katika mazingira
magumu ,upungufu mkubwa wa nyumba za walimu ambapo hivi sasa kuna nyumba tatu
tu na mwamko hafifu wa elimu kwa baadhi ya wanafunzi na wazazi.
Ameitaja mikakati
ambayo inachukuliwa kuwa ni pamoja na kukamilisha ujenzi wa hosteli ili
kuwawezesha wanafunzi kuishi shuleni ukilinganisha na hivi sasa wanaishi mbali
na shule na kusababisha utoro na mimba kwa wanafunzi wa kike.
Baadhi ya walimu
wanaofundisha katika sekondari hiyo wamedai kuwa mazingira duni ya kufundishia
na kuishi yamesababisha walimu kukata tamaa ya kutoa elimu bora hasa ukosefu wa nyumba za kuishi walimu
pamoja na mshahara ambao haulingani na hali halisi ya maisha.
Wamesema wananchi katika kijiji hicho
hawana mwamko mkubwa wa kuunga mkono juhudi za maendeleo ya sekondari hiyo hali
iliyosababisha ujenzi wa vyumba vya madarasa,hosteli na nyumba za walimu
kufanya polepole.
Takwimu
za wilaya zilizotolewa mwishoni mwa mwaka jana na Godfrey Mwakilembe kwa niaba
ya Afisa elimu sekondari wa wilaya zinaonyesha
kwamba kuna walimu 412 wanaofundisha shule 51 za sekondari za serikali wakati
mahitaji halisi ni walimu 726. Kati ya walimu hao 95 tu ndio wa masomo ya
sayansi na hisabati.
Uchunguzi
umebaini kuwa, shule nyingi za sekondari hazina maabara kwa ajili ya mafunzo ya
sayansi kwa vitendo, maktaba,nyumba za walimu,vifaa vya kufundishia na
kujifunzia .
Katika
shule ya sekondari ya Ngumbo masomo yote
ya sayansi katika sekondari hiyo yanafundishwa na mwalimu mmoja tena kwa nadharia kutokana na shule hiyo
kukosa maabara na vifaa ambapo wakati wa
mitihani wa Taifa wa kidato cha nne wanafunzi hawafanyi mitihani ya vitendo
hali ambayo inakatisha tamaa wanafunzi kuchukua masomo ya sayansi na inadumaza
elimu katika sekondari hiyo.
Kutokana na changamoto zinazojitokeza wadau wa elimu kwa
kushirikiana na wananchi wana kila sababu ya kuhakikisha changamoto hizo
zinatafutiwa ufumbuzi wa kudumu.
albano.midelo@gmail.com,simu 0766463129

No comments:
Post a Comment