
Na
Albano Midelo
MAZINGIRA bora
kujifunzia, kufundishia na kuishi ni miongoni mwa mambo muhimu yanayohitajika
ili kuhakikisha elimu bora inatolewa katika shule za msingi na sekondari.
Miundombinu
hafifu katika shule za msingi na
sekondari ni miongoni mwa changamoto zinazozikabili shule hizo na kuchangia
kushusha taaluma katika shule hizo hali ambayo inasababisha wanafunzi kuwa
watoro na walimu kushindwa kufundisha ipasavyo kutokana na kuishi katika
mazingira mabovu.
Uchunguzi ambao
umefanywa katika kata za Kihagara na Liuli wilayani Nyasa unadhihirisha ukweli
huu baada ya kubainika shule karibu zote 12 ambazo zimefanyiwa uchunguzi
zinakabiliwa na upungufu mkubwa wa vyumba vya madarasa,madawati na nyumba za
walimu.
Katika shule ya
msingi Ndonga iliyopo katika kata ya Kihagara umebaini kuwa shule hiyo yenye
wanafunzi 309 ina vyumba vinne tu vya madarasa kati ya mahitaji ya vyumba tisa
hali ambayo inasababisha chumba kimoja cha darasa kutumika na madarasa mawili
kwa wakati mmoja hivyo kuwa na msongamano mkubwa wa wanafunzi.
Shule ya Ndonga
kulingana na mkuu wa shule hiyo Gorge Mbapira ina vyumba viwili vya madarasa
ambavyo vimeezuliwa na upepo tangu mwaka jana hadi sasa havijaezekwa hali ambayo
inawalazimu walimu kuwafundisha wanafunzi
huku wakichomwa na jua hali ambayo inachangia utoro katika shule hiyo
ambayo mahudhurio ni chini ya asilimia 50.
Kulingana na Mbapira
katika shule hiyo yenye walimu watano kuna nyumba moja tu ya mwalimu mkuu yenye
vyumba vitatu,kutokana na uhaba wa nyumba, walimu watatu wanaishi katika nyumba
hiyo huku mwalimu mmoja ikimlazimu kuishi jikoni hali ambayo inamwathiri
mwalimu huyo kisaikolojia na kushindwa kufanya kazi yake ipasavyo.
“Shule ina nyumba
moja tu ya mwalimu mkuu yenye vyumba vitatu,walimu wanne hawana nyumba,nimeamua
kuishi nyumba moja na walimu watatu,mwalimu mmoja anaishi katika chumba cha
jiko,hali ni mbaya’’,anasisitiza Mbapira.
Katika shule ya
msingi Kihagara yenye wanafunzi 498 mkuu wa shule hiyo Anet Ngindo anasema
inakabiliwa na upungufu wa vyumba vya kusomea ambapo darasa la kwanza na la
pili wanasomea katika chumba kimoja.
Hata hivyo kitaaluma
shule hiyo yenye walimu saba kati ya mahitaji ya walimu 14 inafanya wasitani ambapo mwaka 2009 mtihani wa Taifa wa darasa la saba
walifaulu 18 kati ya 78,mwaka 2010 walifaulu 17 kati ya 34 na mwaka 2011
walifaulu sita kati ya 123 waliohitimu.
Katika shule ya
msingi Tumbi kata ya Kihagara yenye wanafunzi 478 ina upungufu wa madawati 40
kati ya mahitaji ya madawati 175 na upungufu wa vyumba vitano vya madarasa.
Katika shule ya
msingi Mango yenye wanafunzi 508 iliyopo kata ya Kihagara inakabiliwa na upungufu wa vyumba vinne vya
madarasa kati ya vyumba 15 vinavyohitajika,shule haina nyumba hata moja ya mwalimu.
Katika shule ya
sekondari ya Mango kuna upungufu mkubwa wa nyumba za walimu ambapo hivi sasa
kuna nyumba tatu tu za walimu,shule haina mabweni, ofisi ya walimu, maabara na
maktaba.
Katika shule ya
msingi Puulu shule yenye wanafunzi 539 inakabiliwa na uhaba mkubwa wa madawati
ambapo madawati yaliopo ni 107 na upungufu ni madawati 134,shule hiyo ina
upungufu wa vyumba saba,vyumba vilivyopo ni vinane.
Mkuu wa shule hiyo
Catherbet Maluka anasema wanafunzi hawana vyoo vya kudumu ambapo vyoo vilivyopo
vya muda vina matundu sita,matundu ya vyoo vya kudumu vinavyohitajika kwa
wasichana ni matundu 10 na wavulana ni matundu 12.
Katika shule ya
sekondari ya kata ya mtakatifu Paulo ya Liuli kwa mujibu wa mjumbe wa Bodi ya
shule hiyo ambaye pia ni diwani wa kata ya Liuli Charles Chawila katika
miundombinu inakabiliwa na upungufu wa
mabweni,majengo chakavu,hakuna bwalo,maktaba na maabara yenye upungufu wa
vifaa.
Katika shule ya
msingi Nambira kwa mujibu wa mwalimu mkuu wa shule hiyo yenye wanafunzi 210
inakabiliwa na changamoto kubwa ya
miundombinu ya majengo ikiwemo wanafunzi kutumia banda ambalo limejengwa kwa
miti kwa ajili ya kusomea darasa la tatu.
“Shule inatumia banda
ambalo limejengwa kwa miti na kuezekwa kwa nyasi kwa ajili ya kusomea darasa la
awali lenye wanafunzi 45,wanafunzi hao wanasoma kuanzia asubuhi na inapofika
saa tisa banda hilo hutumika kama kilabu ’’,alisema mwalimu mkuu.
Mkuu wa shule ya
msingi Hongi Simon Ndunguru anazitaja changamoto katika miundombinu
zinazoikabili shule hiyo kuwa ni upungufu
wa madawati 57 hali ambayo inasababisha wanafunzi watano hadi sita kukaa katika
dawati moja na upungufu wa vyumba saba vya madarasa vilivyopo ni 12.
Katika shule ya
msingi Mwongozo yenye wanafunzi 654,shule inakabiliwa na uhaba upungufu wa
vyumba 15 vya kusomea vilivyopo ni vitano tu,ofisi zinazohitajika ni nane
zilizopo ni tatu tu na darasa la awali lililopo ni chakavu halifai kwa kusomea
na wanafunzi wanakalia vigoda ambavyo wanabeba toka nyumbani.
Mwalimu mkuu wa shule
ya msingi Nkalachi Fabian Ndunguru
anasema shule hiyo ilianzishwa mwaka 1987 yenye wanafunzi 318 ina vyumba
nane vya kusomea kati ya mahitaji ya vyumba 17 na upungufu wa madawati.
Afisa elimu msingi
katika Halmashauri ya wilaya ya Mbinga David Mkali ameahidi kuandaa takwimu za
mapungufu yote katika zote za shule za
msingi ikiwemo upungufu wa vyumba vya madarasa,nyumba za walimu,madawati ili
kukabiliana na upungufu uliojitokeza.
Ameahidi kuanzisha
mpango wa kuchangia elimu ya msingi katika shule zote za msingi kwa
kuwahamasisha viongozi wa vitongoji,vijiji, kata na tarafa ili kufuatilia
changamoto katika maeneo yao na kuzitafutia ufumbuzi wa kudumu.
Afisa elimu huyo
ameahidi kufanya vikao na madiwani wa
kata zote zenye matatizo kuelezwa matatizo ya kielimu ambayo yapo katika shule
zilizopo kwenye kata zao na kuzitafutia ufumbuzi wa kudumu ili kuboresha elimu
.
Katika kuhakikisha
kuwa taaluma inapanda katika shule za msingi,Mkali ameitaja mikakati kabambe
kuwa ni pamoja na kuanza kuandaa kazi za kitaaluma zinazofanana,kuanzisha mfumo
wa walimu kutoa mazoezi mengi darasani na kuwatembelea walimu kila kata ili
kujionea na kusikiliza changamoto zao na kuzitafutia ufumbuzi.
No comments:
Post a Comment