Friday, December 14, 2012

Walimu St.Paul's katika tuhuma nzito



Na Albano Midelo

Kaimu mkuu wa shule Hosea Hinju na baadhi ya walimu katika  sekondari ya mtakatifu Paulo  ya Liuli wilayani Nyasa mkoani Ruvuma wanakabiliwa na tuhuma nzito za kudaiwa kujihusisha na vitendo vya ngono na baadhi ya wanafunzi wa shule hiyo.

Baadhi ya wanafunzi wa kike wa sekondari hiyo ya kata wamedai kaimu mkuu wa shule na baadhi ya walimu  wamekuwa anawalazimisha wanafunzi wa kike kufanya nayo ngono hali ambayo imesababisha shule hiyo kukabiliwa na mmomonyoko wa maadili ambao pia umeshusha kiwango cha taaluma katika shule hiyo.

“Sisi wanafunzi wa kike tunasumbuliwa sana na baadhi ya walimu akiwemo mkuu wa shule wakitaka kufanya ngono,wengine tunakataa lakini wengi wetu wanafanya ngono kutokana na vishawishi mbalimbali,baadhi ya wanafunzi wanakwenda kuwapikia walimu katika nyumba zao na kufanya ngono’’,walidai.

Wanafunzi watano wa kike wanaosoma kidato cha tatu ambao majina yao yanahifadhiwa walidai kuwa  idadi kubwa ya wanafunzi wa kike waliomaliza kidato cha nne mwaka huu walikuwa wanafanya ngono na walimu akiwemo kaimu mkuu wa shule hiyo wametaka mkuu huyo aondolewe kwa kuwa anawadharirisha watoto wa kike.


Baadhi ya wazazi na walezi ambao watoto wao wanasoma katika shule hiyo ya sekondari ambayo kabla ya kuchukuliwa na serikali ilikuwa inamilikiwa na kanisa Anglikana Dayosisi ya Ruvuma wamekiri kupata taarifa kuwa kaimu mkuu wa shule na baadhi ya walimu wa sekondari hiyo wanafanya mapenzi ya wanafunzi .

Mathias Chikeki mwenyekiti mstaafu wa Bodi ya sekondari ya mtakatifu Paulo anasema taaluma katika shule hiyo ilisimamiwa vizuri na mkuu wa shule mwanamke ambaye amehamishiwa mjini Mbinga na kwamba tangu Hinju amekabidhiwa sekondari hiyo maadili na taaluma imeporomoka kwa kasi.

“Sisi wazazi na walezi tuna taarifa kwamba walimu wanatongoza wanafunzi na kufanya nao mapenzi,tuliitisha kikao na kuwaonya walikanusha kuwa sio kweli,shule ina walimu zaidi ya 15 wapo wenye stashahada na shahada kwanini wanafunzi wanafeli katika kiwango cha kutisha’’,alihoji Chikeki.

Matokeo ya mtihani wa Taifa wa kidato cha nne  ya mwaka 2010 na mwaka 2011 katika sekondari ya mtakatifu Paulo yanadhihirisha kuwa  kiwango cha taaluma katika shule hiyo kinatisha ukilinganisha na sifa ambayo shule hiyo ilikuwa nayo awali.

Kulingana na matokeo hayo mwaka 2010 wanafunzi 93 walifeli mtihani,daraja la nne walipata wanafunzi 38 ,daraja la tatu wanafunzi wawili tu daraja la pili mwanafunzi mmoja na hakuna mwanafunzi hata mmoja ambaye alipata daraja la kwanza.

Kwa mujibu wa matokeo hayo mwaka 2011 wanafunzi 97 walifeli,wanafunzi 40 walipata daraja la nne hakuna mwanafunzi hata mmoja aliyepata daraja tatu,pili na la kwanza hali ambayo wazazi na walezi wametaka kaimu mkuu wa shule hiyo kuondolewa kwa kuwa ameshindwa kusimamia maendeleo ya sekondari hiyo.

Diwani wa kata ya Liuli Charles Chawala amekiri kusikia tuhuma dhidi ya kaimu mkuu wa shule hiyo ambapo ameahidi yeye kama msimamizi wa maendeleo katika kata hiyo atafuatilia ili ufumbuzi upatikane na kurudisha heshima ya sekondari hiyo.

“Kwa ujumla taaluma katika sekondari ya mtakatifu Paulo imeporomoka kutokana na sababu mbalimbali zikiwemo ukosefu wa mabweni,baadhi ya wanafunzi hawana mwamko kutokana na kusumbuliwa kimapenzi na  baadhi ya walimu ingawa walimu wamekanusha’’,alisema.

Hata hivyo anasema katika sekondari hiyo kila mwaka kunajitokeza kesi za mimba ingawa wanafunzi hawajawataja walimu kuwa ni miongoni mwa wahusika ambapo mwaka huu pekee kulingana na hotuba ya mkuu wa shule aliyoisoma kwenye mahafali kuna  kesi saba za mimba ambazo zipo mahakamani.

Alipofuatwa ofisini kwake kwa ajili ya kujibu tuhuma zinazomkabili,kaimu mkuu wa shule hiyo alisema haruhusiwi kusema lolote kwa waandishi wa habari hadi atakapopata kibali kutoka kwa mkuu wake ambaye ni afisa elimu sekondari.

“Siwezi kuwapa habari yeyote inayonihusu mimi na sekondari hii hadi mkuu wangu anipe kibali cha kufanya hivyo,mimi siwatambui fanyeni lolote siwezi kujibu tuhuma zozote bila kibali,mkuu wangu amenikataza kutoa habari kwa waandishi,upo waraka ambao unanikataza’’,alisisitiza.

Hata hivyo Afisa elimu kata ya Liuli Abraham Challe alimshangaa kaimu mkuu wa shule hiyo kukataa kutoa habari kwa wana habari ambao wanaibua mafanikio na changamoto za kielimu licha ya diwani wa kata ya Liuli kumuagiza kufanya hivyo.

Alizitaja changamoto zinazoikabili sekondari hiyo  kuwa ni pamoja na kushuka kwa kiwango cha ufaulu,ukosefu wa vifaa vya maabara na vifaa, upungufu wa mabweni,maktaba,bwalo la chakula, upungufu wa matundu ya choo na upungufu wa vifaa vya kufundishia.

Samwel Mawanja katibu wa kata mstaafu anataja sababu kubwa ya kushuka kwa taaluma katika sekondari hiyo ni kuwepo kwa uongozi mbovu wa kaimu mkuu wa shule hiyo ambaye alidai kuwa uwezo wake wa elimu ni wa chini ambaye ana stashahada ambapo kuna walimu wengi wenye shahada ambao anashindwa kuwaongoza.

Anasema taaluma imeshuka katika kipindi cha miaka mitano sasa kutokana na kaimu mkuu huyo alikuwa anatoa adhabu nyingi kwa wanafunzi hali ambayo imesababisha kukithiri kwa utoro kwa wanafunzi na kusababisha taaluma kuwa chini hadi sasa.

Mikakati ambayo inatarajiwa kuchukuliwa ili kuinua taaluma katika shule hiyo kwa mujibu wa diwani wa kata hiyo ni kukamilisha ujenzi wa hoteli ili wanafunzi wote waishi shuleni,walimu kuwajibika ipasavyo kufundisha, wazazi na walezi kuwasimamia watoto katika masomo.

Wazazi na walezi wametoa wito kwa waziri wa elimu na mafunzo ya ufundi kuhakikisha  kaimu mkuu huyo wa shule anaondolewa kwa kuwa ameshindwa kusimamia maendeleo ya shule hiyo kitaaluma pamoja na matumizi mabaya ya fedha za ujenzi wa sekondari hiyo.

Wananchi wa kata ya Liuli pia wametaka kaimu mkuu wa shule aondolewa na kushitakiwa kwa kuwa ameshindwa kusimamia ujenzi wa kidato cha tano na sita katika shule ya sekondari ya kata ambapo wamekuwa wanachangia ujenzi wa shule hiyo ambayo ilitakiwa kufunguliwa tangu mwaka juzi.

“Kaimu mkuu wa shule hajawahi kutusomea mapato na matumizi  licha ya kwamba wananchi tumekuwa na moyo wa kuchangia,kutokana na hilo wananchi hivi sasa hawapo tayari kuendelea kuchangia fedha ambazo hawajui kiasi cha fedha zilizopatikana na zilizotumika’’,walisema wakazi wa Liuli Michael Shauri,Victor Komba,Mathias Erenest na Samwel Mawanja.

Afisa elimu wa Halmashauri ya wilaya ya Mbinga ambaye anasimamia wilaya mpya ya Nyasa David Mkali akizungumzia tuhuma za uongozi wa kaimu mkuu wa shule ya sekondari ya mtakatifu Paulo ya Liuli  ambaye pamoja na tuhuma nyingine wananchi wanataka aondolewa kwa kuwa ameshindwa kusimamia shule hiyo ameahidi kufuatilia tuhuma hizo.

“ Kwa kawaida huwa haondolewi mara moja,ikithibitika kuwa ameshindwa kuongoza,licha ya kupewa maelekezo taratibu za kumuondoa zitafanyika,tunatambua shule hiyo ina walimu wenye shahada na mkuu wa shule ana stashahada,ikumbukwe kuwa walimu wenye shahada wamefika kuanzia mwaka jana kabla  ya hapo walimu wengi walikuwa na stashahada,wakipata uzoefu wa kazi   wanaweza kupata barua za kuteuliwa kuwa wakuu wa shule’’,alisema.



No comments:

Post a Comment