
Na Albano Midelo
HATIMAYE Halmashauri
ya wilaya ya Namtumbo mkoani Ruvuma imetoa chumba kimoja cha darasa katika
shule ya msingi ufundi Namtumbo kwa ajili ya kuwafundishia wanafunzi wenye ulemavu
wa akili wapatao 26.
Halmashauri hiyo
imetoa darasa hilo tangu mwezi Septemba mwaka huu hivyo kutatua changamoto ya muda mrefu ya wanafunzi hao
kusomea chini ya mti na kuathiri elimu kwa wenye ulemavu.
Uchunguzi uliofanywa
na mwandishi wa makala haya mwezi Mei mwaka huu katika kitengo cha wenye
ulemavu shule ya msingi Namtumbo ulibaini kuwa licha ya wilaya nzima ya
Namtumbo kuwa na kitengo kimoja cha wenye ulemavu wilaya ilishindwa kujenga
hata darasa moja kwa ajili ya watoto hao hali ambayo inamlazimu mkuu wa kitengo
hicho Lezile Kampango kuwafundisha wanafunzi hao chini ya mti na wakati wa mvua
anakwenda kuwafundishia katika nyumba yake.
Kitengo hicho ambacho
kilianzishwa mwaka 1997 ndiyo kitengo pekee kinachotoa elimu kwa watoto wenye
ulemavu katika wilaya nzima ya Namtumbo kwa kuwa hakuna kitengo wala shule
ambayo inatoa elimu maalum katika makundi mengine ya wenye ulemavu wa wasioona
na viziwi.
Mkuu wa kitengo hicho
amesema anaishukuru serikali kwa kumpatia chumba maalum kwa ajili ya kusomea
wanafunzi wenye ulemavu hali ambayo inaleta unafuu katika ufundishaji.
Hata hivyo Kampango
alidai kuwa tangu alipoletwa katika kitengo hicho mwaka 2005 hadi sasa kitengo
hicho hakijawahi kupata fedha yeyote kwa ajili ya chakula pamoja na mahitaji
mengine muhimu kwa watoto hao licha ya serikali kutoa ahadi ambazo hazijawahi
kutekelezwa.
“Bado watoto hawa
wanashindwa kupata chakula hali ambayo imesababisha watoto kuwa watoro,chakula ni muhimu kwa wanafunzi
wenye ulemavu ili waendelee kusoma,mlemavu bila chakula hasomi,naomba serikali
itoe ruzuku kwa kitengo hiki vinginevyo kinaweza kufa’’,alisisitiza.
Uchunguzi umebaini
kuwa katika kitengo cha walemavu Namtumbo kuna vivutio vichache kama vile
mpira,filimbi,ambapo upatikanaji wa chakula sio wa uhakika hali ambayo
inatokana na kitengo hicho kukosa ruzuku na wazazi wamekuwa wagumu kuchangia
kitengo hicho.
Baada ya kitengo
hicho kupatiwa chumba kimoja cha darasa sasa kitengo kitakuwa na upungufu wa
chumba kimoja cha darasa ambapo Kitengo
hicho hakina nyumba hata moja ya mwalimu kati ya mahitaji ya nyumba
mbili,hakuna stoo kati ya stoo mbili zinazohitajika, hakuna bwalo la
chakula,jiko, hakuna bweni hata moja kati ya mahitaji ya mabweni mawili na
kwamba hakuna ofisi hata moja ya walimu kati ya mahitaji ya ofisi mbili.
Kulingana na
mwenyekiti wa Halmashauri ya wilaya ya Namtumbo Steven Nana katika msimu wa
fedha wa mwaka 2012/2013 Halmashauri
hiyo ilitenga bajeti ya kiasi cha shilingi milioni saba kwa ajili ya kitengo
cha walemavu wa akili Namtumbo.
Hata hivyo alisema
Halmashauri imeshindwa kupeleka kiasi hicho cha fedha katika kitengo hicho
kutokana na wizara ya TAMISEMI hadi kufikia Desemba mwaka huu kupeleka
kiasi cha asilimia 14 tu ya shilingi
bilioni 16 ambazo zimetengwa katika bajeti ya fedha ya mwaka 2012/2013.
‘’Hali ya kifedha
katika Halmashauri ni mbaya ,serikali ikileta fedha kitengo hicho kitapewa
fedha kama tulivyopanga,upungufu wa fedha ndiyo ambao pia umesababisha ujenzi
wa vyumba vya madarasa kushindwa kukamilika’’,alisema.
Takwimu za idara ya
elimu za mwaka 2011 zinaonesha kuwa katika wilaya ya Namtumbo kuna wanafunzi
wenye ulemavu wapatao 181 ndiyo
wanaosoma katika shule mbalimbali
wakiwemo wenye ulemavu wa akiri 34,wasioona 18,viziwi 11,walemavu wa viungo 109
na albino tisa.
Hata hivyo takwimu hizo
zinaonesha kuwa kuna wanafunzi wenye ulemavu wapatao 71 ambao walitakiwa
kuandikishwa shule hawasomi wakiwemo wenye ulemavu wa akiri 21,wasioona
mmoja,viziwi 11,wenye ulemavu wa viungo 35 na albino watatu.
Takwimu za shirika la umoja wa mataifa
la kuhudumia watoto ulimwenguni(UNICEF) za mwaka 2002 zilionesha kuwa asilimia
98 ya watoto wenye ulemavu katika nchi zinazoendelea ikiwemo Tanzania
hawapatiwi kabisa elimu jambo ambalo ni hatari kwa walemavu.
Imeelezwa kuwa asilimia hii ndogo
inasababishwa na kuwepo kwa shule chache maalum hapa nchini kwa ajili ya watu
wenye ulemavu,ukosefu wa wataalamu,sera na sheria nyingi za nchi hizo hazitaji moja kwa moja au kutoa utaratibu
mzuri wa kutoa elimu kuhusu wenye ulemavu,ukosefu wa vifaa maalum na muhimu vya
kuwawezesha kusoma pamoja na miundo mbinu duni
isiyokidhi mahitaji ya watu wenye
ulemavu.
albano.midelo@gmail.com,simu 0766463129
No comments:
Post a Comment