![]() |
| Wanajeshi wakipiga mizinga kuwakumbuka mashujaa wa vita vya majimaji |
Na Albano Midelo
WAZIRI wa maliasili
na utalii Balozi Hamisi Kagasheki ametoa mwito kwa wadau mbalimbali wa mikoa ya
kusini kuyatambua maeneo yote ya kihistoria na yenye vivutio vingine vya utalii
ili kuboresha utalii ukanda wa kusini.
Waziri Kagasheki ametoa
mwito huo wakati anazungumza katika kilele cha siku ya kumbukizi la vita vya
Majimaji zilizofanyika katika viwanja vya makumbusho ya Taifa ya Majimaji mjini
Songea.
Kilele cha makumbusho
hayo kilihudhuriwa na wageni mbalimbali wa ndani na nje ya nchi wakiwemo mkuu
wa mkoa wa Mbeya Abasi Kandoro,mkuu wa mkoa wa Rukwa Stella Manyanya,mkuu wa
mkoa wa Kilimanjaro Leonidas Gama na mstahiki Agusto Assifue meya wa jiji la
Lichinga nchini Msumbiji.
Waziri Kagasheki
amewahimiza wakuu wa mikoa nchini kuhakikisha kuwa wanavitangaza kwa nguvu zote
vivutio vya utalii ambavyo vitaibuliwa pamoja na kutoa elimu kwa umma kuhusu
umuhimu wa sekta ya utalii nchini inavyochangia kuinua uchumi wa mtu binafsi na
Taifa kwa ujumla.
“Ni vizuri
uendelezaji wa vivutio vya utalii uhusishe kuboresha miundo mbinu kwa
kuwashirikisha wadau mbalimbali kuelekea maeneo ya utalii,kutengeneza ramani ya
mkoa,kuwa na wataalamu wa kuongoza watalii,kuajiri maafisa utalii na malikale
kuwa na usafiri wa uhakika na kuweka taarifa za vivutio kwenye
tovuti’’,anasisitiza.
Ameshauri kila mkoa
kushirikiana na wizara yenye dhamana yaani maliasili na utalii pamoja na wadau
wengine kutoka sekta binafsi kuhakikisha kuwa uboreshaji wa sekta ya utalii
nchini unahitaji wadau wengi na sio jukumu la wizara ,mkoa au shirika la
makumbusho ya Taifa pekee.
Akizungumzia kuhusu
siku ya kumbukizi la vita vya Majimaji waziri Kagasheki amelitaja lengo la
kufanya kumbukizi hizo kuwa ni kivutio cha utalii wa kihistoria na utamaduni
ili kuwapa fursa wananchi wa mikoa ya kusini kutangaza utalii wao wa
kiutamaduni.
“Nimefurahi kuona
kuwa kwa siku tatu ambazo zilikuwa za kumbukiz hili wananchi wamepata fursa ya
kutembelea vivutio vilivyopo mkoani Ruvuma,kufanya mdahalo na warsha kuangalia
namna ya kuviendeleza na kuweka mikakati au maazimio ya namna ya kuvitunza na
kuviendeleza vivutio vya utalii’’,anasema.
Waziri huyo mwenye
dhamana ya utalii ameagiza kumbukizi hizo kuwa kichocheo cha mabadiliko chanya
kwa jamii ambapo ameshauri watoto na vijana kuibua vipaji vyao,ameahidi wizara
yake kuanzia sasa itaanza kuandaa program kwa watoto na vijana ili kukidhi
matakwa hayo.
Ametoa rai kwa mikoa
mingine nchini kuiga mfano wa mkoa wa Ruvuma kwa kuwa ni njia mojawapo ya
kuelimisha jamii umuhimu na kuyaweka vizuri maeneo ya kihistoria yaliopo kusini
mwa nchi ili yaweze kutumika katika kutolea vielelezo vya historia ya nchi na
kuvutia watalii wengi na hatimaye kutoa ajira kwa watanzania.
Katika hatua nyingine
waziri Kagasheki ametoa rai kwa watafiti,wadau na wanajamii wote kufanya
utafiti wa habari za Mama Mkomanile ili
taarifa zake zifahamike kwa watu wengi kwa kuwa alikuwa mwanamke pekee wa mashujaa wa vita vya
Majimaji.
Awali Bi.Eliwasa Maro
kaimu mkurugenzi mkuu wa shirika la makumbusho ya Taifa la Tanzania alibainisha
kuwa maadhimisho ya tamasha la kumbukizi ya vita vya Majimaji na utalii wa
utamaduni kitaifa yamekuwa yakiadhimishwa kila mwaka Februari 27 ambapo dhana
ya maadhimisho hayo ni kuchochea mabadiliko ya kifkra na kiutamaduni kwa jamii.
“Makumbusho ya Taifa
yamekabidhiwa jukumu la kuendesha kituo cha makumbusho ya Majimaji tangu mwaka
2010,makumbusho haya yanasaidia wadau mbalimbali kuhakikisha kuwa sherehe za
maadhimisho ya kumbukizi zinafanyika kila mwaka zikihusisha dhana nzima ya
ukusanyaji,utunzaji na utoaji wa elimu kwa jamii’’,alisisitiza.
Maro amebainisha
zaidi kuwa maadhimisho ya mwaka huu yamelenga katika kuhakikisha kuwa kumbukizi
za vita vya majimaji zinakuwa kichocheo cha mabadiliko kwa jamii kifikra na
kiutamaduni ambapo amehimiza kumbukizi
hizo ziwe endelevu kwa ajili ya kusaidia urithi za Taifa kwa ajili ya vizazi
vya sasa vijavyo.
Mkurugenzi na
mhifadhi kiongozi wa makumbusho ya Taifa ya Majimaji ya Songea Balthazar
Nyamusya akzungumzia umuhimu wa makumbusho hayo anabainisha kuwa baada ya vita vya Majimaji viongozi na
askari walioshiriki katika vita hivyo walikamatwa na kuhukumiwa kunyongwa hadi
kufa ambapo Februari 27,mwaka 1907 ilikuwa ni siku ya masikitiko makubwa kwa
watu wa mkoa wa Ruvuma baada ya watu zaidi ya 60 kunyongwa kwa sababu ya
kushiriki katika vita vya majimaji.
Mashujaa hao
walinyongewa nyuma ya eneo ambalo hivi sasa linajulikana kwa jina la Songea
Club,baada ya kunyongwa miili ya mashujaa hao ilizikwa katika kaburi la
halaiki,lililoandaliwa na wafungwa kwa muda wa miezi miwili,siku ya tatu baadaye
chifu wa kabila la wangoni Songea Mbano
alinyongwa na kuzikwa katika kaburi la
pekee yake ambapo inaaminika alizikwa kiwiliwili baada ya kichwa chake kukatwa
na wajerumani na kukipeleka.
Hata hivyo mhifadhi
kiongozi huyo anasisitiza kuwa eneo la Mahenge walilozikwa mashujaa hao ni
muhimu katika historia ya mtanzania ndiyo maana mara baada ya uhuru mwaka 1961
baadhi ya wazee walianzisha harakati za kuwakumbuka mashujaa hao pamoja na
kuanza kufanya maombi ya kimila katika eneo hilo walilonyongewa mashujaa hao.
Kwa mujibu wa Nyamusya,Makumbusho ya vita vya
majimaji kama yalivyo makumbusho mengine ya kihistoria ni chombo cha kuelimisha
jamii kuhusu mambo muhimu ya kujivunia ya Taifa,makumbusho ya majimaji ni
historia nzuri na kiburudisho pamoja na kuwa chombo cha kujenga hamasa ya
kujiamini kama Taifa na kuimarisha umoja,kuheshimiana na kuishi kwa amani.
Utafiti umebaini kuwa Makumbusho ya Taifa ya
majimaji ndiyo makumbusho pekee nchini ambayo inamiliki vifaa halisi na zana halisi za jadi ambazo
zilitumiwa na wazee wa jadi katika mambo
mbalimbali.
“Mimi nimefanya kazi
katika makumbusho ya Taifa Dar es salaam hakuna zana halisi za jadi kama
makumbusho ya majimaji,hivyo nadiriki kusema majimaji ni makumbusho pekee
nchini yenye zana hizi ukiondoa makumbusho ya Ujerumani ambayo ina vifaa halisi
ambavyo vilitumiwa wakati wa vita vya majimaji”,anasisitiza mhifadhi huyo.
Hata hivyo utafiti
umebaini kuwa makumbusho nyingi zimekosa vifaa kwa kuwa vilichukuliwa na kuondoka navyo watawala na kwamba katika
makumbusho hayo kilichofanyika ni kutafuta vifaa ambavyo vinafanana na sio
halisi kama makumbusho ya majimaji.
“Hili ni jambo la kihistoria na ni utalii wa
kiutamaduni ambao watalii wengi wa ndani na nje ya nchi watapenda kuja katika
makumbusho haya na kujifunza,kuona vifaa na zana halisi zilizotumika ambavyo
vimehifadhimiwa katika majengo ya makumbusho ya Taifa ya Majimaji”,anasisitiza.
Makumbusho ya
mashujaa wa vita vya majimaji yalijengwa mwaka 1980 lengo lilikuwa ni kutunza
hadhi ya sehemu ya makumbusho ya majimaji, shinikizo la ujenzi wa majengo hayo
lilitolewa na kauli ya Baba wa Taifa
mwalimu Julius Nyerere kwenye mkutano wea TANU mwaka 1958.
Nyerere aliagiza
ijengwe minara katika mikoa yote nchini kwa ajili ya heshima ya kuwaenzi
mashujaa wa ukoloni ambao ndiyo chimbuko la kupigania uhuru ambapo tafiti
unaonesha kuwa katika maeneo mengine ya nchi walishindwa hata kujenga minara ya
mashujaa ambapo Baba wa taifa mwaka 1965 alisisitiza na kukumbushia kile
alichoahidi kujenga minara mwaka 1958 sasa kila mkoa ujenge minara hiyo ya
mashujaa.
“Mkoa wa Lindi umejenga mnara mwaka 2008 tena kwa shinikizo
la chuo kikuu cha Dar es salaam ambapo mnara huo umejengwa katika eneo la
Nandete ndiyo maana nasema Songea ndiyo pekee ambapo katika makumbusho ya
Songea zimejengwa sanamu mbalimbali za wapiganaji ambao alikuwa nao chifu
Songea Mbano kwenye Baraza lake kupambana na wakoloni’,anasema mhifadhi wa
makumbusho ya taifa Philipo Maligissu.
albano.midelo@gmail.com

No comments:
Post a Comment