Sunday, March 31, 2013

Wengi waweza kuathirika na maji yenye sumu Songea



Na Albano Midelo
WATU  wanaoishi katika wilaya ya Songea, mkoani Ruvuma wapo katika hatari ya kukumbwa na magonjwa mbalimbali na hata kupoteza maisha kutokana na  kutumia maji ya mto  ya Luhira  ambao umechafuliwa kwa kemikali mbalimbali.


Luhira ni chanzo cha mto Ruhuhu ambao unamwaga maji yake ziwa Nyasa, mto Luhira unaanzia kwenye milima ya Matogoro iliyopo nje kidogo ya mji wa Songea,milima hiyo pia ni chanzo cha mito Ruvuma na Luegu ambayo inamwaga maji yake bahari ya Hindi. Mamlaka ya Maji Safi na Maji Taka Songea (SOUWASA) inategemea chanzo cha maji cha mto Luhira kwa ajili ya kusambaza maji kwa wakazi zaidi  180,000 wa mji wa Songea.

Katika chanzo hicho wakulima wanalima nyanya, karoti, chainizi,spinachi,mboga za maboga pamoja na mboga nyingine ambapo hupulizia madawa ya kuuwa wadudu waharibifu ambayo ni hatari kwa afya na baadhi yake yamepigwa marufuku kimataifa yakiwemo bluecopper, redcopper, DDT na  kimatila.


Mkuu wa mkoa wa Ruvuma Said Mwambungu
Wakulima wadogo kutoka katika vijiji vinavyozunguka milima ya Matogoro vikiwemo vijiji vya Mahiro, Matogoro, Ndilima, Chemchem,Mletele na Kikunja ndiyo wanaoendesha kilimo cha bustani na kupulizia madawa ambayo ni hatari  yakitumika jirani na  vyanzo vya maji.


Uchunguzi umebaini kuwa nguvu walionayo wanasiasa kuanzia ngazi ya kijiji, kata hadi juu ndiyo inachangia kilimo kwenye vyanzo vya maji kuendelea kwa kuwa wataalamu licha ya kuzuia kilimo hicho wamezidiwa nguvu na wanasiasa hali ambayo imesababisha kunyamaza kuhofia kuharibu kazi.

Christopher Michael ni daktari wa  mimea,binadamu na wanyama ambaye anafanya utafiti wake mkoani Ruvuma kuhusu athari zinazotokana na uchafuzi wa maji anasema kupulizia kemikali jirani na vyanzo vya maji  zinasababisha magonjwa zaidi ya 30 kwa binadamu wanaokunywa au kula vyakula vilivyoathirika na kemikali hizo.



Ameyataja baadhi ya magonjwa ambayo mtu anaweza kuugua kwa kunywa au kula kemikali kuwa ni ugonjwa wa ini,saratani ya damu, figo, ngozi,kuoza sehemu za siri, kupata mzio,kiharusi, kuoza mapafu, macho, magonjwa ya kuhara, amiba, kichocho na  kuvimba tumbo ambapo magonjwa huanza kujitokeza kati ya miezi mitatu hadi miaka 15.



Kwa mujibu wa Dk.Michael dalili za mtu ambaye ameathirika na matumizi ya kemikali zenye sumu ni magonjwa ya ngozi, kung’oka kwa kucha, kupungukiwa nguvu za uzazi kwa wanaume,kope kuwasha na na macho kupoteza uwezo wa kuona,kuungua chembechembe hai za damu, kuoza mapafu, kuharibika figo, kukosa hewa kwenye ubongo, kupoteza fahamu na matatizo ya akiri.



“Kemikali kama bluecopper ikiingia mwilini hakuna dawa za kuweza kuiondoa ,kinachofanyika hospitalini ni mtu ambaye anakuwa na dalili kwa mfano za kupoteza fahamu anapewa dripu la maji ,tatizo la vyanzo vya maji kuathirika na kemikali zenye sumu lipo kila mahali, kinachotakiwa ni kutoa elimu ya kutochafua maji kwenye vyanzo ’’,anasisitiza Dk.Michael.



Anasema tangu afike mkoani Ruvuma mwezi Juni 2010   amewabaini  wagonjwa zaidi ya 1500 ambao wana dalili zote za kuathirika na madawa ya kemikali nzito zenye sumu yaani heavy metals na tayari ametoa tiba mbadala na elimu kwa  baadhi ya wagonjwa.



 Abel Mapunda ni mratibu wa afya na mazingira hospitali ya misheni Peramiho Songea, anabainisha kuwa matumizi ya kemikali nzito kama vile zebaki na bluecopper  kwenye vyanzo vya maji yanatakiwa yaepukwe kabisa kwa kuwa kemikali hizo zinaingia moja kwa moja kwenye maji na zina madhara makubwa kwa afya ya binadamu na viumbehai.



“Heavy metals zinaleta matatizo makubwa kwenye mfumo wa fahamu hadi kwenye ubongo,katika hospitali ya misheni Peramiho tumekuwa tunapokea wagonjwa ambao wanakuwa wameletwa wakiwa wamepoteza fahamu, tunapowachunguza na  kuwapima magonjwa  ya malaria, UKIMWI na uti wa mgongo tunakuta hawana magonjwa hayo’’,anasema .



 Hata hivyo anabainisha kuwa utafiti wa awali unaonesha kuwa kuna uwezekano mkubwa wagonjwa hao wameathirika na heavy metals ,hata hivyo ili kuthibitisha kuwa wagonjwa hao wameathirika na kemikali hizo inatakiwa kufanya utafiti zaidi kwa wagonjwa .



Uchunguzi unaonesha kuwa Katika chanzo cha maji cha Luhira wakulima  wanaendelea kulima nyanya, kabichi, nyanyachungu, mboga za maboga,mchicha na karoti wakitumia mbolea za chumvichumvi aina ya SA,CAN na NPK pamoja na madawa ya kuuwa wadudu aina ya bluecopper kimatila,DDT,theonix,sumithion,karate,selecrone.



Madawa mengine ambayo wakulima hao wanatumia kupulizia kwenye nyanya kwa lengo la kuzuia ugonjwa wa ukungu ambao unakausha nyanya ni nidithane, milthane, Bravo, rido,ridomil,victory,farmazeb,helicozeb,mancozeb na lincomil.



Msimamizi wa chanzo cha maji cha mto Luhira Swalehe Kinana anasema wakulima katika chanzo cha mto Luhira licha ya kwamba wengi wameanza kuogopa kulima baada ya kuanza kuchukuliwa hatua za kisheria, hata hivyo bado wanalima ambapo mwaka huu wamelima eneo lenye ukubwa wa kilometa nne kando kando ya chanzo hicho cha maji.



“Wakulima hawa bado wanaendelea kutumia kemikali hatari kwenye vyanzo vya maji na huwa wanapulizia kemikali hizo kuanzia  mwezi Desemba hadi Agosti kila mwaka miezi ambayo kuna wadudu wengi waharibifu wa mimea,miezi ambayo huwa hawatumii dawa hizo ni kuanzia mwezi Septemba hadi Novemba tu’’,anasisitiza.



Josephat Maliselo ni mdhibiti wa ubora wa maji na viwango  kutoka SOUWASA anasema kemikali aina ya bluecopper na redcopper zinapoingia kwenye chanzo cha maji cha mto Luhira ,zinaingia na kupenya moja kwa moja kwa kuwa  hawana vifaa vya kuzuia kemikali hizo  kuingia kwenye maji ambayo yanatumiwa na wakazi wa mji wa Songea jambo ambalo linaweza kuathiri afya za watumiaji.



Maliselo ambaye ni daktari wa maji wa SOUWASA anaongeza kuwa  maabara yao ya maji iliyopo Songea haina mashine ya  kupima  na kutambua kemikali za blue coper au red copper ambazo zimeingia kwenye maji na kwamba hapa nchini mashine ambazo zinaweza kupima zipo maabara ya wizara ya maji ,Mkemia mkuu, na chuo kikuu cha Dare s salaam.



Meneja wa ufundi wa SOUWASA mwandisi John Kapinga  anabainisha kuwa uharibifu  na uchafuzi unaofanywa kwenye chanzo cha maji cha mto Luhira unachangia kupunguza kiasi cha maji yanayoweza kutiririka kutoka milima ya Matogoro pamoja na maji yanayosukumwa kutoka Luhira darajani.



 Anasema mamlaka yake katika kipindi cha kuanzia mwezi wa Septemba hadi Desemba kila mwaka inakabiliwa na uzalishaji mdogo wa maji na kusababisha mgawo mkali wa maji kwa wananchi wa mji wa Songea kutokana na uharibifu unaendelea kufanywa na wananchi katika vyanzo vya maji vilivyopo katika milima ya Matogoro hususani kwenye chanzo cha maji cha mto Luhira .



 Charles Haule,Oliver Mbilinyi na Alois Haule ni baadhi ya wakulima ambao wanalima bustani katika vyanzo vya maji katika vijiji vya Mahiro na Chemchem wamekiri kulima katika vyanzo vya maji pamoja na kutumia kemikali za sumu na kueleza kuwa wanatumia kemikali hizo kwa uzoefu tu kwa kuwa hawana elimu ya athari za mazingira zinazotokana na kemikali hizo ambazo wanazitumia kila mwaka.



“Sisi wakulima tunaozunguka milima ya Matogoro tunalima kahawa ambayo tunapulizia dawa aina ya bluecopper ambayo wakati wa masika inachuruzika na kuingia kwenye vyanzo vya maji vilivyopo Matogoro hatujui serikali imedhibiti kitu gani kwa kutuzuia kulima bustani’’,alihoji mkulima John Nchimbi wa Mahiro.



Luis Ngonyani ni mtaalamu wa mimea kutoka kampuni binafsi ya RAPCO  anasema matumizi ya dawa ya kahawa aina ya bluecopper  karibu na vyanzo vya maji ni hatari kwa kuwa wakati wa masika dawa hizo zinachurizika na kuingia moja kwa moja kwenye vyanzo vya maji.



Meneja wa maji Bonde la ziwa Nyasa Witgal Mkondora anasema bonde hilo linahusika na kuulinda mto Luhira  ambapo amekiri bonde kupata changamoto ya kushindwa kuwadhibiti wakulima wanaolima jirani na chanzo cha mto huo kutokana na wakulima kupenda kulima katika maeneo oevu ambayo yana rutuba nyingi na maji ya kumwagilia.



Hata hivyo Mkondora anabainisha kuwa  sheria ya mazingira namba 57 ya mwaka 2004 inataka shughuli za kibinadamu kufanyika umbali wa meta 60 kutoka katika kingo za mto na kwamba wote wanaolima  kando kando ya mito  wanafanya makosa na wanatakiwa kuchukukuliwa hatua za kisheria.



“Siku ya Jumanne na Alhamisi tunafanya operesheni ya kuwakamata wote wanaolima katika bonde la mto Luhira lenye ukubwa wa hekta 15,000  tumeshawakamata watuhumiwa kadhaa kutoka kata za Matogoro,Mletele na Ndilima ambao walikuwa wanalima bustani ndani ya chanzo cha mto, kesi zao zipo mahakamani’’,anasema.



Sera maji ya mwaka 2002 inalenga kuhakikisha kuwa vyanzo vya maji vilivyopo vinatunzwa,kulindwa na kuendelezwa kwa utaratibu unaozingatia uwiano wa mahitaji ya viumbehai wote










                                 


No comments:

Post a Comment