TANGU mwaka 1961 hadi 1970 Bonde la
Songwe wilayani Chunya mkoani Mbeya lilikuwa ni ardhi oevu,yenye uoto wa
kijani na msitu mnene wenye miti mbalimbali ya asili.
Wakati huo wakulima
waliweza kuzalisha mazao ya chakula kwa wingi kutokana na bonde kuwa na ardhi
oevu yenye maji yaliokuwa yanatiririka kutoka mto Songwe ambao unaanzia milima
ya Umalila Mbeya na kumwaga maji yake ziwa Rukwa .
Bonde la Songwe ambalo linaundwa
na kata za Totowe,Galula,Namkukwe,Kanga na Mbuyuni wakati huo lilikuwa
linavutia maisha ya viumbehai wakiwemo binadamu, wanyamapori na ndege wa
aina mbalimbali ambao walikuwa wanaimba kwa furaha.
Mtu ambaye alifika kwenye bonde
la Songwe miaka ya 1970 akitembelea leo kwenye bonde hilo hawezi kuamini kwa
kile ambacho atakiona kutokana na mabadiliko makubwa ya kimazingira
ambayo yamejitokeza hivi sasa na kutaharisha maisha ya viumbe hai.
Katika bonde la Songwe hivi sasa miti
imetoweka na ardhi imebaki uchi,mto Songwe ambao ndiyo mto pekee unaomwaga maji
yake ziwa Rukwa kwa mwaka mzima upo katika hatari ya kutoweka,ziwa Rukwa
limesinyaa kuwa dogo na kina chake kinapungua kwa kasi.
Miti karibu yote iliyokuwa
kivutio katika Bonde la Songwe haipo tena,Bonde limejaa makorongo makubwa
ambayo yanatokana na mmomonyoko wa ardhi,vumbi zito na vimbunga vya mara
kwa mara limekuwa ni jambo la kawaida katika bonde hili.
Unapofika kwenye bonde hili
kuanzia mwezi wa Aprili hadi Novemba utaona upepo wenye vumbi zito ambao
unaweza kudhani mvua inataka kunyesha,vumbi hilo huwa zito kiasi kwamba huwezi
kumuona mtu aliye mbele yako.Hali hii inawafanya wakazi wa Bonde hilo
kujifungia ndani ya nyumba zao kuepukana na vumbi hilo.
Vumbi hilo ambalo unaweza
kuliita mvua ya vumbi huchukua kati ya saa nne au siku nzima,hali ambayo huleta
kero kwa wakazi kushindwa kuwajibika ipasavyo katika kazi mbalimbali za
kiuchumi,kijamii na burudani.
Katika Bonde la Songwe
wakulima waliweza kulima mazao mbalimbali yakiwemo mahindi, alizeti,
ufuta, mtama,viazi vitamu,mpunga bila kuweka mbolea ya chumvichumvi,hivi
sasa Bonde hilo linakabiliwa na njaa kila mwaka kutokana na ukame
unaotokana na bonde kukosa mvua za uhakika.
Ziwa Rukwa kwenye bonde hili,tangu
uhuru limetoa ajira katika sekta ya uvuvi ambapo wavuvi wameweza kusomesha
watoto wao,kujipatia kipato kwa kuuza samaki na kupata kitoweo ambacho
kinajenga afya kutokana na samaki wanaopatikana kwenye ziwa hilo.
![]() |
| Moja ya fukwe ziwa Rukwa upande wa Bonde la Songwe imekauka kilometa nane |
Hata hivyo maisha ya wakazi wa Bonde
hili yapo hatarini baada ya athari za kimazingira kuanza kujitokeza kutokana na
uharibifu wa mazingira ikiwemo kuanza kusinyaa kwa vyanzo muhimu vya maji
ambavyo ni mto Songwe na ziwa Rukwa .
Wakati wa masika maelfu ya tani za
mchanga,tope na takataka nyingine husombwa na kuingia mto Songwe na
kupelekwa ziwa Rukwa hali ambayo inasababisha kina cha maji cha mto na
ziwa kupungua kwa kasi.
Athari hizo za kimazingira
zinachangiwa na idadi kubwa ya mifugo ambayo inaendelea kuongezeka
kwa kasi kubwa kwenye Bonde la Songwe huku wafugaji hao wahamiaji kutoka kanda
ya ziwa wakifanya uharibifu wa mazingira kwa kufyeka miti ovyo kwa lengo la
kujipatia kuni,mkaa na mashamba.
Afisa mifugo,kilimo na ushirika
katika Halmashauri ya wilaya ya Chunya Adamu Mbale anasema idadi ya
ng,ombe katika bonde zima kati ya mwaka 1961 hadi 1970 ilikuwa ni 800 tu hali
iliyosababisha mazingira katika bonde hilo kuwa ya kuvutia.
Mbale anabainisha kuwa idadi ya
ng’ombe kwenye Bonde hilo iliongezeka kwa kasi na kuathiri mazingira
katika kipindi cha kuanzia mwaka 1981 hadi 1990 ng’ombe walifikia
173,681,mwaka 2000 ng’ombe walifikia 186,800 na hadi kufikia mwaka 2010 idadi
ya ng’ombe ilifikia 286,800.
Mbale anasema eneo
linalofaa kwa ajili ya malisho wilayani Chunya ni hekta 1,353,300 na
kwamba eneo ambalo limepimwa na kutengwa kwa kwa ajili ya malisho ni
622,397.
Diwani mstaafu na mwenyekiti wa
kamati ya mazingira Bonde la Songwe William Mahenge anabainisha kuwa
wafugaji katika bonde hilo wanamiliki makundi makubwa ya ng’ombe kati ya
200 hadi 5000 kwa mfugaji mmoja na kusisitiza kuwa mifugo ni sababu
kubwa ya mazingira ya bonde hilo kuharibika.
Mifugo mingi imesababisha fukwe
za ziwa Rukwa upande wa Bonde la Songwe zilizopo kwenye vijiji vya kata ya
Totowe kukauka na kusababisha ziwa hilo kupungua ukubwa na
kina hali inayohatarisha uwepo wa ziwa hilo ambalo linashika nafasi ya nne kwa
ukubwa hapa Tanzania likitanguliwa na maziwa ya Tanganyika,Viktoria na
Nyasa.
Fukwe ambazo zinapotea kwa kasi
ni pamoja na fukwe ya Handeni ambayo imekauka kwa kilometa 10,Ihovyo kilometa
tatu,Mtanda kilometa saba,kisiwani kilometa tisa,kambipotea kilometa
tano,Kwaboko kilometa sita na fukwe ya Mchangani kilometa tano.Kina cha
maji katika fukwe hizo hivi sasa ni chini ya meta moja .
“Fukwe hii ya kisiwani mwaka 1998
ilikuwa kilometa nane kutoka hapa ,unaweza kutembea katika kina cha maji chini
ya magoti hadi umbali wa meta 300 ndani ya ziwa,hali hii ikiendelea ziwa hili
linaweza kukauka au kuwa bwawa ’’, anasema John Mwakyoma mvuvi katika ziwa
Rukwa.
Peter Sasawata na Stanley Rwamba
ni wavuvi katika fukwe ya Mtanda wanasema fukwe hiyo mwaka 1994 ilikuwa
kilometa saba kutoka hapo ilipo leo na kwamba chanzo kikuu cha kukauka kwa
fukwe ni mifugo mingi ambayo inaingia kunywa maji na kula malisho ndani ya ziwa
kila siku.
“Mimi nimeishi katika kijiji cha
Ihovyo kwa miaka 11 wakati nafika hapa maji ya ziwa hili ulikuwa unayakuta
baada ya kutembea kwa dakika tano tu lakini hivi sasa inakulazimu kutembea
zaidi ya saa mbili ndipo unalikuta ziwa ’’,anasema Beston Mwambene mwalimu wa
shule ya msingi Ihovyo .
Mwambene anabainisha kuwa
Kupungua kwa kina cha maji kisanyasi kunasababisha ukubwa wa ziwa Rukwa
kupungua,kina kikiwa kifupi ziwa litaongezeka kwa muda kisha litarudi nyuma kwa
kasi na kwamba kuongezeka kwa joto kutasababisha kiasi kikubwa cha maji kupotea
kwenda angani hatimaye ziwa hilo linaweza kuwa bwawa.
“Kama kweli serikali inataka
kuliokoa bonde la Songwe lisigeuke jangwa na ziwa Rukwa lisipotee kwenye uso wa
Dunia,waache kuendekeza siasa kwenye mazingira, ziwa Rukwa litakauka, wakulima
wanazidi kusogeza mashamba ya mpunga kwenye fukwe za ziwa’’,anasisitiza
Mwambene.
Kuwepo kwa mifugo mingi kwenye
Bonde la Songwe sio tu kumechangia kuleta athari za kimazingira kwenye bonde
hilo,bali pia kumesababisha migogoro kati ya wafugaji na wakulima.
Migogoro hiyo imesababisha majeruhi na
vifo kwenye bonde hilo kwa mfano mwaka 2006 wafugaji watano walikufa na
wengine 11 kujeruhiwa vibaya katika kijiji cha Totowe bonde la Songwe.
Afisa mtendaji wa kijiji cha Totowe
Paskalia Luwi anasema wafugaji walifikwa na mauti hayo kutokana na chuki ya
muda mrefu iliyojengeka kutokana na tabia yao ya kulisha mifugo yao kwenye
mashamba ya wakulima.
Mkuu wa wilaya ya Chunya Deodatus
Kinawiro katika kukabiliana na uingizaji wa mifugo ametoa wito kwa
wakuu wa wilaya tisa zinazopakana na wilaya yake wasitishe utoaji wa
vibali vya kusafirishia mifugo hasa Ng'ombe wanaoingia wilayani humo.
Afisa wa bonde la maji la Rukwa
Idris Msuya anasema“mifugo iliyopo ziwa Rukwa inatisha hata mimi mwenyewe
nilipoiona mara ya kwanza ilinichanganya,nimeshuhudia maelfu ya mifugo
ambayo inaishi, kula na kunywa maji ziwa Rukwa kwenye fukwe
za kijiji cha Totowe.hali hii inatisha’’,anasema.
Hata hivyo Msuya
anakiri kina cha maji cha ziwa Rukwa kinaendelea kupungua mwaka hadi mwaka
kutokana na uharibifu wa mazingira unaochangiwa na idadi kubwa ya ng’ombe
katika wilaya zinazozunguka ziwa Rukwa ambazo alizitaja kuwa ni Chunya, Mbeya,
Sumbawanga, Mpanda, Mbozi na Nkasi.
Kulingana na Msuya, Ziwa Rukwa hivi
sasa lina wastani wa kina cha juu cha maji cha mita 800, kina cha chini ni mita
nne , eneo la maji la ziwa hilo ni kati ya kilometa 800 hadi 2300
kutegemeana na kiasi cha mvua inayonyesha.
Makamu wa Rais Dk.Mohamed Ghalib Bilal
akizungumza katika moja ya siku ya mazingira duniani alisema baadhi
ya gharama za uharibifu wa mazingira tumekwishaanza kuzibeba
ambapo kutokana na uharibifu huo vina vya maji katika mabwawa, mito
na maziwa vimekuwa vikishuka.
Utafiti tayari imebaini kuwa katika
kipindi cha mwaka 1970 hadi 2006 Ziwa
Rukwa limepungua kwa kiasi cha zaidi ya kilomita saba, kina na ukubwa wa ziwa
Manyara umepungua kwa asilimia 65, na ukubwa wa Ziwa Jipe umepungua kwa
asilimia 65.
Ni dhahiri kuwa, hatuwezi kuitazama
miaka 50 ijayo kwa matumaini bila kutafakari hali ya mazingira. Hali hii
isipodhibitiwa haraka, mifumo ya mvua itabadilika, vyanzo vya maji vitakauka,
ubora wa maji utaathirika, bioanuai itatoweka, maeneo mengi yatakuwa kame.
albano.midelo@gmail.com,simu 0766463129


No comments:
Post a Comment