Thursday, April 25, 2013

Mgogoro wa ziwa Nyasa wamponza Rais Banda



Na Albano Midelo
MGOGORO mpaka wa ziwa Nyasa kati ya Tanzania na Malawi umeimarisha mshikamano kwa wananchi wa nchi hizo mbili ambao wanaishi mpakani Kiongozi limebaini.
Baadhi ya wananchi wanaoishi mwambao mwa ziwa Nyasa katika maeneo ya Mbambabay,Liuli na Kihagara wamesema mgogoro ambao unaendelea kuzungumzwa na viongozi wa kitaifa baina ya Tanzania na Malawi umesababisha mahusiano yao maeneo ya mipakani kuimarika na kuongezeka.
Samweli Mawanja katibu kata mstaafu wa Liuli  anasema wananchi wa mipakani baina ya Tanzania na Malawi wamekuwa wanatembeleana na kufanya biashara mbalimbali bila wasiwasi wowote licha ya viongozi wa kitaifa kusikika kushindwa kufikia muafaka wa mpaka wa ziwa Nyasa kati ya nchi hizo mbili.
“Tumekuwa tunasikia katika vyombo vya habari vya Tanzania na Malawi vikizungumzia mgogoro huu,lakini nataka kukuambia kwamba wananchi wa Malawi wanafika hapa kila siku kuleta biashara zao na sisi watanzania tunakwenda kila siku katika nchi ya Malawi  kupeleka biashara mbalimbali hakuna vurugu ni amani na utulivu’’,anasisitiza Mawanja.


Kwa mfano jana usiku kuna boti la Malawi limeingia na kuleta shehena ya sukari toka Malawi,idadi ya watu wa Malawi wanaofika hapa ni kubwa zaidi ukilinganisha na watanzania,wananchi wa Malawi wengi wanalaani na kusikitishwa Rais wao kugombana na watanzania na wameahidi katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2014 kumuangusha anasema Mawanja.
Charles Chawila ni diwani wa kata ya Liuli anasema wavuvi wa Tanzania wamekuwa wanaendelea na kazi ya uvuvi katika ziwa Nyasa kwa amani na utulivu  na kwamba kauli kali zinazotolewa na viongozi wa kitaifa wa nchi zote mbili haziendani na hali halisi ambayo inaendelea tangu kuibuliwa upya kwa mgogoro huo kwa kuwa wananchi wanaendelea kushirikiana vizuri katika sekta za kiuchumi,kijamii na kiutamaduni.
“Viongozi wengi pengine hawajui,kuna watanzania wengi wa mwambao mwa ziwa Nyasa ambao wameoa na kuolewa Malawi na kuna watu wa Malawi wengi ambao wameoa na kuolewa Tanzania mgogoro huu ambao unakuzwa na vyombo vya habari kupitia wanasiasa sio mkubwa kama inavyoelezwa’’,anasisitiza.
John Chiume ni mtanzania ambaye anaishi na kufanya biashara katika kisiwa cha Likoma nchini Malawi  kwa zaidi ya miaka 30 sasa, anasema wananchi wa Malawi hawafurahishwi na kitendo cha Rais wao Joyce Banda kuibua mgogoro wa mpaka wa ziwa Nyasa ambapo amedai huenda kitendo hicho kikamuathiri kisiasa Rais huyo katika uchaguzi mkuu ujao.
Gorge Mkate(70) mkazi wa Mbambabay anasema Mgogoro huo ulianza enzi ya hayati Rais Kamuzu Banda ambaye miaka ya sitini  alikuwa anazungumza kwenye redio yao,kwamba  ziwa lote ni la Malawi  pia wilaya ya Rungwe na hadi Mbeya ni sehemu ya Malawi.
“Hayati baba wa Taifa  Mwalimu Julius Nyerere mwaka 1968  alimwita Kamuzu Banda ni kichaa,alikasirika kwa sababu ya madai ya Kamuzu kwamba sehemu za kusini ya Tanzania ni za Malawi,alidai hata makao makuu ya wilaya mpya Mbamba Bay na sehemu zingine mkoani Ruvuma karibu na Ziwa Nyasa kwamba ni za Malawi’’,alidai Mkate.
Amesema nchi ya Malawi ina mikoa mitatu ambayo aliitaja kuwa ni Lilongwe,Mzuzu na Brinytre  na kwamba wananchi wengi wa Malawi wapo Tanzania katika maeneo ya mpakani wakishirikina vizuri na watanzania ambapo hadi sasa hakuna tatizo lolote licha ya madai yanayoendelea kuchochea mgogoro kuonekana kama ni mkubwa.
Gidion Ntare mvuvi wa samaki katika ziwa Nyasa anasema wamekuwa wanaendelea kufanyakazi ya uvuvi hadi katikati ya ziwa Nyasa bila wasiwasi wowote wa kushambuliwa na nchi ya Malawi  ambapo madai ya kuibuka kwa mgogoro wa ziwa Nyasa wamekuwa wanausikia kupitia vyombo vya habari .
“Wavuvi wanaendelea kuvua usiku na mchana hadi katikati ya ziwa haijawahi kutokea eti kuna mvuvi ameshambuliwa  hali ni ya amani na utulivu,wavuvi wanakufa kutokana na ajali za  mitumbwi  katika ziwa Nyasa ambazo zinasababisha wavuvi wengi kupoteza maisha kila mwaka’’,alisema.
Hata hivyo Ntare anasema wamekuwa wanakwenda kufanya uvuvi katika nchi ya Malawi ambapo hali ya maisha ya wavuvi wa Malawi ni bora zaidi kuliko Tanzania wanatumia vifaa vya kisasa,wavuvi  ndiyo wanaongoza kwa utajiri katika nchi ya Malawi ndiyo sababu kuna wavuvi wengi wa Tanzania wameamua kwenda kufanyakazi ya uvuvi nchini Malawi ambako serikali imewawezesha samaki wanaovuliwa hupelekwa kuuzwa katika nchi za Zimbawe,Afrika ya kusini na Botswana.
Martin Challe  ameiomba serikali ya Tanzania kuhakikisha katika kipindi hiki cha mgogoro wa mpaka wa ziwa Nyasa maeneo yote ya mwambao mwa ziwa yanaendelezwa kwa kuwa yamesahaulika tangu uhuru ukilinganisha na maeneo ya mwambao mwa ziwa Nyasa upande wa Malawi ambapo kuna maendeleo makubwa.
Challe anadai kuwa ukifika mwambao mwa ziwa Nyasa upande wa Malawi barabara zake ni za viwango vya lami,uvuvi wa kisasa,hata fukwe za ziwa Nyasa upande wa Malawi zimeboreshwa  na wawekezaji wameboresha sekta ya utalii wa fukwe ambapo upande wa Tanzania hali ni mbaya kuanzia uvuvi duni, barabara na hata fukwe bora zilizopo bado hazijatambuliwa hadi sasa.
Chanzo cha mgogoro wa ziwa Nyasa kimetokana na mikataba yenye utata iliyoachwa na wakoloni waingereza, ambapo kwa kulitambua hilo marais waliotangulia hasa Bakili Muluzi na Bingu wa Mutharika wa Malawi na wenzao Julius Nyerere, Ali Hassan Mwinyi na Benjamin Mkapa wa Tanzania waliendeleza mazungumzo. kutokana na makubaliano kati ya Waingereza waliokuwa watawala wa Nyasaland na Wajerumani waliokuwa watawala wa Tanganyika, mpaka halali baina ya nchi hizo ulikuwa katikati ya ziwa Nyasa.


Hivi sasa jopo la usuluhishi wa sakata la mgogoro wa ziwa Nyasa limeundwa wakiwemo marais wa zamani barani Afrika ambao ni Festus Mogae (Botswana),Thabo Mbeki (Afrika Kusini) na Joachim Chissano (Msumbiji) ambaye ndiye mwenyekiti..
 Tayari nchi ya Malawi imetangaza kujitoa katika mazungumzo ya mgogoro wa mpaka kati yake na Tanzania kwenye Ziwa Nyasa, ambapo Serikali ya Tanzania kupitia waziri wa mambo ya nje na ushirikiano wa kimataifa Bernad Membe imeitaka nchi hiyo kuacha kutapatapa na kamwe isithubutu kugusa eneo hilo la mpaka.
Waziri Membe kwa niaba ya serikali amesema kama nchi hiyo itakiuka, Serikali ya Tanzania itaomba ushauri wa nini cha kufanya kutoka kwa jopo la usuluhishi .
Kauli hiyo ya Serikali imekuja siku chache baada ya Rais wa Malawi, Joyce Banda kusema kuwa mgogoro huo sasa utapelekwa katika Mahakama ya Kimataifa ya Haki (ICJ), kwa madai kwamba juhudi za usuluhishi wa kidiplomasia zimeshindikana.
Hata hivyo, uamuzi huo wa Malawi ni kinyume na makubaliano baina ya nchi hizo mbili yaliyofanyika Novemba 7 mwaka jana, jijini Dar es Salaam ambapo serikali zote zilikubaliana kwamba jopo hilo ndiyo sehemu ya mwisho ya makubaliano.
Waziri huyo wa mambo ya nje na ushirikiano wa kimataifa alisema kuwa tangu kuibuka kwa mgogoro huo, Malawi imekwenda kulalamika katika nchi za Uingereza, Marekani, Umoja wa Afrika (AU) na katika Jumuiya ya Maendeleo ya Nchi za Kusini mwa Afrika (SADC).
Mgogoro huo uliibuka baada ya Serikali ya Malawi bila kushauriana na Tanzania kutoa leseni kwa kampuni mbili za kigeni kutafuta mafuta baada ya kubainika kuwa katika eneo la ziwa Nyasa  kuna kiasi kikubwa cha Mafuta.

No comments:

Post a Comment