Na
Albano Midelo
WANAWAKE hasa katika nchi zinazoendelea kama
Tanzania bado wanakabiliwa na changamoto mbalimbali ikiwemo matatizo wakati wa
kujifungua ambapo kila mwaka akinamama zaidi ya 8000 hufariki kutokana na
matatizo ya uzazi.
Kana kwamba hilo halitoshi wanawake
pia wanakabiliwa na tatizo jingine la kiafya ambalo ni ugonjwa wa saratani au
kansa ya kizazi ambayo inaelezwa ndiyo kansa inayoongoza katika kusababisha
vifo vitokanavyo na kansa kwa akinamama waliopo katika nchi zinazoendelea.
Utafiti
unaonesha kuwa akinamama zaidi ya 500,000 hupatwa na ugonjwa wa kansa ya uzazi
kila mwaka ulimwenguni, kati ya hao akinamama 250,000 hufariki kila mwaka
kutokana na ugonjwa huo ambapo hapa nchini wanawake 4000 wanagundulika kila
mwaka.
Ugonjwa huo
nchini Tanzania umeelezwa kukua kwa kasi, huku waathirika wa tatizo hilo wakiwa
ni vijana wenye umri wa kati ya miaka 25 na 30. Daktari wa Kitengo cha
Patholojia cha Uchunguzi wa Magonjwa katika Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH)
jijini Dar es Salaam Innocent Mosha anasema, kati ya wagonjwa 17 na 20
hugundulika na saratani kila siku katika hospitali hiyo ya taifa.
“Kwa
mwaka wagonjwa wanaogundulika kuwa na saratani katika hospitali ya Taifa ya
Muhimbili ni zaidi ya 4,000, takwimu hizo ni za Hospitali ya Taifa Muhimbili
tu, bado kuna Ocean Road, mikoani na hospitali nyingine binafsi’’,alisisitiza
Dk.Mosha.
Daktari Bingwa wa Kitengo cha Uchunguzi wa
Magonjwa hospitali ya Taifa ya Muhimbili mjini, Dk.Henry Mwakyoma anazitaja saratani
kuu zinazoongoza nchini kuwa ni pamoja na saratani ya shingo ya kizazi, tezi
dume, ngozi, mifupa, tezi kwa watoto na wakubwa, damu, kongosho, ubongo na ini.
Ugonjwa
wa saratani umekuwa tishio katika nchi za Afrika zilizo chini ya Jangwa la
Sahara ikiwamo Tanzania ambapo kwa mwaka 2010, takwimu zinaonesha ugonjwa huo
umeua watu milioni 9.9 duniani.
Mratibu
wa kampeni ya kupambana na ugonjwa huo nchini kutoka Taasisi ya Tanzania 50
Plus, Mchungaji Dk. Emmanuel Kandusi,amesisitiza kuwa saratani ni hatari
ukilinganisha na takwimu za magonjwa mengine.
Takwimu
za magonjwa za mwaka 2010 zinazoonyesha kuwa ugonjwa wa malaria uliua watu 500,000, kifua kikuu
milioni 2.1, UKIMWI milioni 1.8 na Saratani iliongoza kwa kuua watu milioni
9.9.
Hata
hivyo Dk.Kandusi anabainisha kuwa asilimia 75 ya watu waliokufa kwa ugonjwa wa
saratani (sawa na milioni 7.4), walitoka katika nchi zinazoendelea.
Amezitaja
dalili za saratani ya tezi dume, kuwa ni pamoja na mgonjwa hupata udhaifu
katika kujisaidia haja ndogo, hisia ya kutaka kupata haja ndogo kila wakati
hasa nyakati za usiku, mkojo kutoka wenyewe, maumivu au kuhisi muwasho wakati
wa haja ndogo na uume kusimama kwa shida.
Daktari bingwa wa magonjwa ya wanawake
kutoka katika hospitali ya rufaa ya misheni ya Peramiho iliyopo nje kidogo ya
mji wa Songea mkoani Ruvuma Dk.Gaudence Komba anasema hapa nchini takwimu
zinaonesha kuwa kansa au saratani ya kizazi ndiyo inayoongoza kwa kusababisha
vifo.
Dk.Komba anazitaja saratani nyingine
ambazo zinafuatia katika kusababisha vifo kwa wanawake kuwa ni pamoja na saratani inayoitwa kitaalamu Kapodsarcoma na
saratani ya matiti.
Hata hivyo anasema zaidi ya asilimia
80 ya wagonjwa wa saratani ya kizazi hufika katika vituo vya kutolea huduma za
afya wakiwa wamechelewa yaani ugonjwa
ukiwa tayari umeenea sana jambo ambalo anasema saratani hizo inakuwa ni vigumu
kutibika kwake kwa kuwa ugonjwa unakuwa tayari umeenea sehemu mbalimbali za
mwili.
Amezitaja sababu zinazobabisha
wagonjwa wa saratani ya kizazi kuwa ni pamoja na kwenda hospitali wakiwa
wamechelewa kuwa ni pamoja na kukosekana kwa
huduma za uchunguzi wa awali(screening) hasa katika maeneo ya vijijini pamoja na kutokuwa na
uelewa kuwa saratani ya uzazi inaweza kuzuilika kwa kufanyiwa uchunguzi wa
awali.
Daktari huyo bingwa wa magonjwa ya
wanawake anasisitiza kuwa ugonjwa wa saratani ya kizazi ukiwa katika hatua za
mwanzo unaweza kutibika kabisa kwa njia ya upasuaji au kwa njia ya mionzi.
Hata hivyo kulingana na Dk.Komba,katika
nchi zilizoendelea uchunguzi wa awali unafanywa mara kwa mara katika nchi
hizo,umepunguza kabisa saratani ya uzazi kwa akinamama na kwamba njia
inayotumika kufanya uchunguzi iitwayo kitaalum Cytology, imeonekana kuwa ni
ngumu kutumika katika nchi za dunia ya
tatu kama Tanzania.
Kulingana na daktari huyo njia hiyo
inahitaji wataalamu wa hali ya juu hali ambayo anasema inasababisha gharama ya
huduma hiyo kuwa ni kubwa na hatimaye kushindwa kufanyika katika nchi
zinazoendelea.
Kutokana na hali hiyo shirika la afya
duniani(WHO) kwa kushirikiana na wadau wengine wa afya ulimwenguni limegundua
njia inayoonekana kuwa mbadala kwa nchi zinazoendelea kama Tanzania,njia ambayo
kitaalaum inaitwa visual inspection with acetic acid(VIA) ambapo huduma hiyo
inaweza kutolewa hata katika vituo vya afya na zahanati kwa kuwatumia wahudumu
waliopo kama wauguzi na waganga.
Dk.Komba anasema tayari WHO inasaidia
serikali za nchi mbalimbali kuanzisha na kuendeleza huduma hiyo ambapo
majaribio ya huduma hiyo tayari yamefanyika katika wilaya mbalimbali na kupata
mafanikio makubwa ili kuanzisha huduma hiyo muhimu kwa maendeleo ya afya za
wanawake.
Changamoto kubwa inayowakabili wanawake ni
kwamba licha ya saratani ya kizazi ambayo inaongoza kwa kusababisha vifo vingi
vya wanawake ulimwenguni,saratani nyingine ambayo inatajwa kuwa ni miongoni mwa
saratani zinazogharimu maisha ya wanawake
ni saratani ya matiti.
Chama cha madaktari wanawake
nchini(MEWATA) kwa kushirikiana, vyombo vya habari nchini na wadau wengine katika miaka ya karibuni vimekuwa mstari wa
mbele katika kufanya kampeni kabambe ya kuhakikisha wanawake wanajitokeza
kupima ili kutambua mapema iwapo wana saratani hiyo ya matiti ili waweze kupatia
matibabu mapema.
Takwimu kutoka MEWATA zinaonesha kuwa
kati ya wanawake zaidi ya 55,000 waliopimwa saratani ya matiti,wanawake 113
wamegundulika kuwa na saratani ya matiti.
Hata hivyo takwimu hizo za MEWATA
zinabainisha kuwa kati ya wanawake hao
waliopimwa, wanawake 2498 wamegundulika kuwa na matatizo ambayo hayahusiani na
saratani ya matiti.MEWATA kwa kushirikiana na wizara ya afya na ustawi wa jamii
imekuwa ikiandaa tiba kwa wanawake waliogundulika kuwa na saratani ya matiti
kulingana na sehemu ambayo ugonjwa huo umefikia.
Wataalamu wa saratani ya matiti
wanasema iwapo ugonjwa huo ni uvimbe na
saratani haijasambaa ,mgonjwa atapelekwa kufanyiwa upasuaji na kupatiwa tiba na
kwamba endapo saratani hiyo itakuwa imesambaa inabidi mgonjwa akatibiwe kwa
mionzi katika Taasisi ya saratani iliyopo katika hospitali ya Ocean Road jijini
Dar es salaam.
Kulingana
na wataalamu,saratani ya matiti ni uvimbe usiokuwa na maumivu ambao mwanamke
yeyote anaweza kuwa anao bila ya yeye
mwenyewe kujijua na kwamba inashauriwa kila mwanamke awe na ufahamu kuhusu afya
yake na mwili wake pamoja na kujenga
tabia ya kujichunguza mwenyewe mara kwa mara.
Shirika la
Afya Duniani (WHO) limesema zaidi ya asilimia 70 ya visa vya ugonjwa wa saratani
vinaweza kuzuiliwa na kwamba saratani inaweza kuzuilika ikiwa nchi zitaongeza
uwezo wao wa kudhibiti saratani.
Kwa
mujibu wa WHO nusu ya nchi kote duniani hazina uwezo wa kukabiliana kikamilifu
na ugonjwa huo, na wala hazina mpango tekelezi wa kuudhibiti , ambao
unajumuisha kuzuia, kugundua mapema, kutibu na huduma za uuguzi.
Takwimu
za WHO zinaonyesha kuwa watu milioni 7.6 wanafariki dunia kila mwaka kutokana
na saratani, huku takriban watu milioni 13 wakiwa wanapatikana na kansa kila
mwaka.
albano.midelo@gmail.com,simu
0766463129

No comments:
Post a Comment