![]() |
| Wananchi wakiwemo wanafunzi wakikimbilia ngoma ya sakamimba Tunduru |
Na Albano Midelo
MAFUNZO ya unyago,msondo na ngoma ya sakamimba yanayofanywa na kabila la wayao wilayani Tunduru mkoani Ruvuma yamesababisha idadi kubwa ya wanafunzi wa
kike katika shule za msingi na sekondari kukatishwa masomo kwa
kuolewa.Utafiti wa kina ambao
umefanywa katika za sekondari za Frankweston, Mgomba, Tunduru, Mataka, Namwinyu,
Lukumbule na Nalasi wilayani Tunduru umebaini kuwa karibu nusu ya wanafunzi wa
kike katika shule hizo wameacha masomo yao baada ya kupata mimba na
kuolewa hali ambayo imechangia wilaya
hiyo kuwa ya mwisho kitaaluma katika mkoa wa Ruvuma katika elimu ya msingi na
sekondari.
Azizi Saidi
mwanafunzi wa kidato cha nne katika shule ya sekondari Frankweston anasema utamaduni wa kufanyiwa unyago
umesababisha wanafunzi wa kike wake
kupata mafunzo hayo na kujiona kwamba wapo tayari kuolewa hata wakiwa bado
shuleni hali ambayo inasababisha wanafunzi wengi wa kike kuacha masomo.
“Sisi ambao hivi sasa
tupo kidato cha nne tunaohudhuria darasani ni chini ya wanafunzi 100, tulipoanza kidato
cha kwanza mwaka 2010 tulikuwa wanafunzi zaidi ya 240,wanafunzi wengi wa kike
waliofanyiwa utamaduni wa unyago na msondo wameacha shule kwa kuolewa au kupata
mimba’’,alisema.
Salima Sefu
mwanafunzi sekondari ya Frankweston
ameomba mila hizo alizodai kuwa ni potofu ni vema serikali ingezitazama
upya kwa kuwa wanafunzi wengi wanaolewa wakiwa wadogo bila kuwa na uwezo wa
kulea familia hali ambayo pia imechangia ndoa nyingi kuvunjika na kusababisha
watoto wao kulelewa na mzazi mmoja .
Hemed Ally mwanafunzi
wa kidato cha nne shule ya Frank Weston akizungumzia mila ya msondo na unyago
anasema wanafunzi wa kike baadhi ya mambo ambayo wanafundishwa hayalingani na
umri wa wanafunzi kwa kuwa ni mambo ya ndoa namna ya kuishi na wanaume yanayowahusu
watu wazima.
Anasema katika
mafunzo hayo wanafunzi wa kike wanaelezwa faida za kuishi na mume lakini
hawafundishwi madhara ambayo wanaweza kupata kwa kushiriki katika ndoa wakiwa
wadogo hali hiyo ndiyo inawahamasisha wanafunzi kujiingiza kwenye ngono na
kushawishika kuolewa wakiwa wanafunzi.
“ mimi kama
mwanafunzi wa kike nashauri mila hizi ziachwe,hata hivyo wazee wa mila za
msondo na unyago hawapo tayari mila hizo
kuachwa kwa kuwa wanaamini zinafundisha malezi kwa watoto wa kike na wapo tayari
kupambana na mtu yeyote ambaye anazipiga vita mila na utamaduni huo ’’,
Katika kijiji cha
Nalasi wilayani Tunduru mtoto wa kike ambaye ameshavunja ungo anatolewa katika
nyumba ya wazazi na kujengewa au kupewa chumba cha pekee yake na kwamba mtoto
huyo anakuwa huru kufanya lolote na kurudi nyumbani majira yeyote bila kuulizwa
na mlezi au mzazi wake hali hiyo imechangia kuongezeka kwa mimba utotoni na
utoro wa kudumu.
Rehema Sara mwanafunzi wa kidato cha nne
sekondari ya Mgomba anasema mila za
unyago na msondo zimesababisha wanafunzi wengi wa kike katika shule hiyo kuacha
masomo kwa kupata mimba au kuolewa ambapo hivi sasa katika darasa lao
waliofanikiwa kufika kidato cha nne ni wanafunzi 106 tu kati ya wanafunzi zaidi
ya 230 walioanza nao kidato cha kwanza.
“ Mimi nilifundishwa
mila na desturi za msondo na unyago nikiwa darasa la kwanza mambo ambayo hayafai kusema ni matusi tangu
nilipofundishwa hadi sasa sijasahau ,hizo mila walitakiwa kufundisha malezi
pekee na sio mambo ya ndoa ’’,alisisitiza Mariam Jafari mwanafunzi wa kidato
cha pili sekondari ya Mgomba.
Sala mkombozi wa
kidato cha nne sekondari ya Mgomba ambaye alifanyiwa ngoma ya unyago na msondo
akiwa darasa la tatu amekiri baadhi ya mambo wanayofundishwa ni mazuri kwa
ajili ya malezi lakini kuna mengine hayafai kwa kuwa wanafundishwa namna ya kuishi na mume jambo ambalo ni
hatari kwa wanafunzi.
Mimi wenzangu wengi
ambao nilikuwa nao shule na msingi na wengine ilitakiwa niwe nao katika shule
ya sekondari wameacha masomo kwa kuwa wana watoto baada ya kupata mimba na
wengine wameolewa na kuachika hivyo wanaangaika na maisha kwa kuwa waliingia
kwenye maisha ya ndoa katika umri mdogo.
Sharifa Hamisi
mwanafunzi wa kidato cha nne sekondari ya Mataka anasema mila za msondo na unyago ndiyo chanzo
kikuu cha mimba na wanafunzi kuolewa tofauti na siku za nyuma walikuwa
wanafundishwa zaidi maadili mema wakiwa na umri wa kuanzia miaka 18 lakini hivi
sasa watoto wa kike wanafundishwa katika
umri mdogo kuanzia darasa la tatu.
Hawa Mponda mwalimu
shule ya msingi Mlingoti anadai mila za msondo na unyago hivi sasa watoto
wadogo kuanzia darasa la kwanza wanaingizwa kwenye mafunzo ya unyago namna ya
kuishi na wanaume hali ambayo wanapoendelea kukua wanafanya majaribio na kuleta
athari za mimba na kuolewa wakiwa wanafunzi.
Hassan Musa mkuu wa
shule ya sekondari Frankweston anasema kipaumbele kwa wakazi wa wilayani
Tunduru ni mila za msondo,unyago na jando hali ambayo inasababisha utoro,mimba
na wanafunzi kuolewa hali ambayo imechangia kushusha elimu katika wilaya.
“Mimi nimefundisha
katika shule mbalimbali za wilaya ya Tunduru,ukitembelea vijijini utabaini kuwa
ndoa nyingi zimevunjika na hivi sasa watoto wanalelewa na mzazi mmoja ambaye ni
mama,mwanamke anaweza kuolewa zaidi ya mara moja na kuachwa hivyo mama anakosa
uwezo wa kumlea na kumsomesha mtoto wake hivyo mtoto kujiingiza kwenye mapenzi
na kupata ujauzito’’,alisema.
Elice Mapunda mkuu wa
sekondari ya Mgomba amekiri tatizo la mimba kwa wanafunzi kuwa kubwa katika
shule za sekondari na kwamba hali hiyo
inatokana na watoto wa kike kuwaficha wanaume ambao wamewapa mimba na kwamba
hata hivyo mimba zinaendelea kupungua.
“Mimi ni mngoni wa
Songea lakini nimezaliwa Tunduru,nina rafiki zangu wamechezwa msondo na unyago,
lakini hivi sasa wamesoma hadi kiwango cha kuwa na shahada mimi sikubaliani
sana kuwa mila na desturi hii ndiyo
chanzo cha mimba za utotoni,kwanza watoto wa kike waliopitia mafunzo hayo
kikamilifu hawasemi nini wanajifunza huko,hao wanaosema nani amewaruhusu
kusema’’,alihoji.
Hadija Said mwalimu
wa malezi na ushauri nasaha katika sekondari ya Mataka amekiri shule hiyo mara
kadhaa kukabiliwa na mimba za utotoni,utoro wa kudumu na kuolewa wakiwa bado
wanafunzi na kwamba mila ya msondo na unyago zamani ilikuwa inafanyika lakini
idadi ya wanafunzi waliokuwa wanapata mimba mimba za utotoni na kuolewa haikuwa
kubwa kama ilivyo sasa.
Flavian Nchimbi kaimu afisa
elimu msingi wilaya ya Tunduru anasema tatizo la mimba katika shule za
msingi zimepungua ukilinganisha na miaka mitatu nyuma kulikuwa na mimba karibu
250 ambapo takwimu za mwaka jana zinaonyesha kuwa katika shule za msingi
zililipotiwa mimba 16 na kwamba kuanzia mwezi Januari hadi Aprili mwaka huu
imeripotiwa mimba moja tu.
Kwa
mujibu wa Takwimu za Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi, wasichana 8000 kila
mwaka huacha shule kutokana na ujauzito. Kati yao 3,000 ni wanafunzi wa shule
za msingi.
Kila
siku, wanawake 24 hufariki dunia kutokana na mimba au wakati wa kujifungua.
Wanawake watano mpaka sita wanaofariki kati ya hao ni watoto wadogo, watoto hao
hufariki dunia kwa kuwa miili yao haijakomaa vya kutosha kwa ajili ya
kujifungua.
Mkuu wa wilaya ya Tunduru Chande Nalicho amekiri
mila na desturi za kabila la wayao zinachangia wilaya hiyo kuwa duni kielimu
ambapo amesema tayari serikali imeunda kikosi kazi cha kuonana na viongozi wa
mila, makungwi na manyakanga kuwaelimisha juu ya utoaji wa elimu kwa watoto wa
kike kupenda masomo.
“Binti aliyechezwa unyago ukimuuliza
umefundishwa nini anasema tumekatazwa kusema tulichofundishwa,ina maana mtu
anayeweza kumsikiliza na kumkubali ni kungwi ambaye ndiye mwalimu wake wa unyago
kwa hiyo sisi kama serikali tukiwaelekeza wanaweza kutusaidia kuwasisitizia hao
watoto umuhimu wa elimu wakati wanawapa elimu ya jando na unyago”anasema.
albano.midelo@gmail.com,simu 0766463129

No comments:
Post a Comment