Saturday, June 8, 2013

Mimba zapungua shule za msingi Tunduru



Na Albano Midelo
Mmoja wa wanafunzi aliyepewa mimba Tunduru
MABADILIKO makubwa yametokea katika shule za msingi wilayani Tunduru ambapo idadi ya wanafunzi wanaopata mimba katika shule za msingi imepungua kutoka mimba  zaidi ya 250 kwa mwaka miaka mitatu iliyopita hadi kufikia mimba 16 tu mwaka 2012.
Flavian Nchimbi  kaimu afisa  elimu msingi wilaya ya Tunduru alisema tatizo la mimba katika shule za msingi zimepungua ukilinganisha na miaka mitatu nyuma ambapo  zaidi ya nusu ya mimba zilizoripotiwa za mkoa wa Ruvuma kwa wanafunzi zilitokea wilayani humo.
“Kwa mfano mwaka 2010 katika mkoa wa Ruvuma kulikuwa na mimba za wanafunzi 544 kati ya hizo mimba karibu 250 ziliripotiwa kutoka wilaya ya Tunduru pekee huku idadi nyingine inayobakia ni kwa wilaya za Songea,Mbinga na Namtumbo kwa hivi sasa tumefanikiwa sana kupunguza tatizo la mimba kwa wanafunzi wa shule za msingi katika wilaya ya Tunduru hadi mimba 16 tu mwaka mwaka jana’’,alisema.

Aliongeza kuwa mwaka huu huenda idadi ya mimba katika shule za msingi ikapungua zaidi kutokana na takwimu kuonyesha kuwa katika kipindi cha mwezi Januari hadi Mei mwaka huu ni mimba moja tu ndiyo iliyoripotiwa.
Hata hivyo afisa elimu huyo alikiri msukumo ambayo ulifanywa na vyombo vya habari kutoa kipaumbele katika tatizo la mimba za utotoni na utoro ambao ulikithiri  na kuathiri sekta ya elimu, uliamsha uongozi katika ngazi mbalimbali kuchukua hatua za kuhakikisha matatizo hayo yanapatiwa ufumbuzi wa kudumu.
Alizitaja hatua ambazo zilichukuliwa kuwa  ni pamoja na kuamua kufanya operesheni maalum ya kuwatafuta wanafunzi  watoro na ambao wameshindwa kuendelea na masomo kwa sababu ya mimba,kuwasaka wanaume waliowapa mimba ili kuwachukulia hatua za kisheria na kutoa fundisho kwa wanaume wengine wenye tabia hiyo.
  “Tunafungua kesi  nyingi kila mwaka kwa wazazi na walezi ambao wameshindwa kuwapeleka watoto wao  shule za msingi, wanaume waliowapa mimba wanafunzi,wanaume wanaoa wanafunzi pamoja na wanafunzi watoro wa kudumu, tumeshirikiana na Baraza la madiwani,viongozi wa dini  kimila na wadau wengine kuweka msukumo katika elimu ndiyo maana sasa hata idadi ya mimba zimepungua sana’’,alisisitiza Nchimbi.
Mkuu wa wilaya ya Tunduru Chande Nalicho alisema Kutokana na  na takwimu mbaya za mimba za utotoni zilizokuwepo na kuiathiri sekta ya elimu wilayani humo yeye binafsi amefanya ziara katika vijiji vyote vya wilaya hiyo na kuwawaagiza viongozi wa serikali za vijiji,kata na tarafa kuwachukulia hatua wazazi na walezi wote ambao wameshindwa kusimamia mahudhurio ya watoto shuleni,mimba za utotoni na kushindwa kuwapeleka watoto wao waliofaulu shule za msingi kujiunga na sekondari.
 “Hali ya elimu sio nzuri wilayani Tunduru,tumeamua kufanya operesheni maalum ya kuwatafuta wanafunzi ambao wameshindwa kwenda kidato cha kwanza mwaka huu, tumefungua kesi 1054 za wazazi ambao wameshindwa kuwapeleka watoto wao waliofaulu shule za msingi kwenda sekondari,tutahakikisha  tunaweka msukumo wa kudumu katika elimu ili wilaya yetu iweze kupata maendeleo makubwa katika sekta ya elimu ’’,alisisitiza
Kwa mujibu wa Takwimu za kitaifa za Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi za hivi karibuni zinaonyesha kuwa wasichana 8000  kila mwaka huacha shule kutokana na ujauzito kati ya hao  wanafunzi 3,000 ni  shule za msingi na 5000 ni wanafunzi wa shule za sekondari.
albano.midelo@gmail.com

.

1 comment: