Serikali inao maofisa wa elimu
katika kila kata nchini ambao wangetumika kabisa kukusanya kero za elimu na
Serikali kuu kuzifanyia kazi.Kinachoonekana sasa ni kama mpango mwingine wa
kuendeleza porojo kwa kufanya vikao vinavyotumia fedha nyingi badala ya
kuboresha elimu.Hali ya elimu nchini inaonekana kuendelea kuwa mbaya licha ya
ahadi nyingi za Serikali kuiboresha.
Mojawapo ya sababu za kuwepo kwa
hali hiyo mbaya, inaelezwa ni mazingira duni ya kufundishia, uhaba wa vifaa na
walimu kutoridhishwa na malipo kwa kazi wanazofanya.
Agosti 15, mwaka huu Serikali
ilizindua utekelezaji wa mkakati wa ‘Matokeo Makubwa Sasa’ katika elimu nchini,
huku sekta hiyo ikionekana kudidimia.
Elimu ni miongoni mwa sekta sita
zilizochaguliwa katika Mpango wa Serikali hivi karibuni wa kuleta Matokeo
Makubwa Sasa. Sekta nyingine ni Nishati, Maji, Miundombinu, Kilimo na Fedha.
Sekta hizi sita zimechaguliwa ziwe za mwanzo katika kutekeleza Mpango huu wa
Serikali ili kuiletea nchi matokeo makubwa kwa haraka.
Sekta hizi zinabeba msingi wa
kufungulia fursa za ukuaji uchumi wa nchi kwa ujumla na kuchochea ustawi wa
maisha bora kwa Watanzania wote.
Waziri wa Elimu na Mafunzo ya
Ufundi, Dk Shukuru Kawambwa aliyezindua utekelezaji huo, Jijini Dar es Salaam,
anasema katika sekta ya elimu, washiriki 34 kutoka taasisi 31 zikiwemo za
Serikali na zisizo za Serikali, washirika na wadau wa maendeleo ya elimu
walikutana kati ya 25 Februari hadi 05 Aprili, 2013, kutafakari kwa kina
changamoto zinazoathiri sekta ya elimu.
Changamoto kubwa iliyoainishwa ni
kiwango cha uandikishaji wa wanafunzi kimeongezeka, ubora wa elimu umeshuka,
hususan kuporomoka kwa kiwango cha ufaulu katika Elimu ya Msingi na Sekondari.
Kuboresha elimu ni kichocheo muhimu katika kuleta maendeleo nchini. Ingawa
ufaulu siyo kiashiria pekee cha ubora wa elimu, kwa sasa ni muhimu kutumika
kupima ubora wa elimu nchini kwetu.
Matokeo ya mitihani ya kidato cha
nne yalivyokuwa
Asilimia 60 ya watahiniwa walipata
alama sifuri yaani walifeli.
Mchanganuo ni kama hivi;
Matokeo ya kidato cha nne 2012:
Alama 1 (0.4%) Alama 2 (1.6%) Alama 3 (3.9%) Alama 4 (26.0%) Alama 0 (60.1%).
Baadhi ya wananchi wanasema huenda
ikawa ni mipango mizuri, cha msingi ni itekelezwe kwa vitendo. Hata hivyo
baadhi wana hofu kwamba hakuna chochote cha maana kinaweza kutokea kwa sababu
kwa staili ya sasa walimu hupatikana kutokana na waliofeli.
CHANZO MWANANCHI

No comments:
Post a Comment