![]() |
| Ziwa Rukwa likiwa katika hatari ya kugeuka bwawa |
Albano
Midelo
Utafiti umebaini ziwa Rukwa upande wa wilaya ya Chunya Mbeya linandelea
kusinyaa kwa kasi kutokana na uharibifu mkubwa wa mazingira
unaotokana na shughuli za kibinadamu wilayani humo.
Ziwa Rukwa linapita katika wilaya za Chunya na Momba mkoani Mbeya,wilaya
za Sumbawanga na Nkasi mkoani Rukwa na wilaya ya Mpanda mkoani Katavi.
Utafiti ambao umefanyika mwezi
Juni mwaka huu katika wilaya ya Chunya umebaini kuwa mto Lupa ambao ni mto mkubwa
kuliko mito yote inayoingiza maji katika ziwa hilo ukitoa wilayani Chunya
umekauka kabisa na hivi sasa hakuna maji ambayo yanatiririka kwenda ziwani
kupitia mto huo.
Miaka michache nyuma mto Lupa ulikuwa unatiririsha maji karibu mwaka
mzima isipokuwa mwezi Novemba ndiyo ulikuwa unaweka visiwa lakini kwa mara ya
kwanza mwaka huu hadi kufikia mwezi Juni mto umekauka kabisa na hakuna maji
yanayoingia ziwa Rukwa kutokea mto Lupa jambo ambalo linahatarisha uwepo wa
ziwa Rukwa.
Hata hivyo Mto Songwe unaomwaga
pia maji yake ziwa Rukwa ambao unaanzia milima ya Umalilia wilayani Mbeya ndiyo
mto pekee uliobakia kutokea wilayani Chunya unaendelea kumwaga maji yake mwaka
mzima katika ziwa Rukwa .
Kutokana na uharibifu mkubwa unaotishia kukauka kwa ziwa Rukwa serikali wilayani
Chunya imeamua kuchukua maamuzi magumu
ya ya kusimamisha biashara ya kilimo
kwenye ardhi oevu pembezoni mwa ziwa Rukwa na mito ya Lupa na Songwe
ambavyo vinachangia kuharibu vyanzo vya maji ambapo hivi sasa mito na ziwa vipo
katika hatari ya kukauka.
![]() |
| Moja ya fukwe katika kijiji cha Totowe iliyokauka kwa km 10 |
Mkuu wa wilaya ya Chunya Deodatus
Kinawiro anasisitiza kuwa malisho ya mifugo na kilimo katika ardhi oevu
inasimamishwa kuanzia mwaka huu na kwamba serikali kuanzia sasa itakuwa kama
msumeno unaokata pande zote kwa kupambana na wafugaji wanaolisha mifugo katika
ardhi oevu pamoja na wakulima wanaoendesha kilimo katika maeneo oevu ambayo
hayaruhusiwi kisheria.
“Sisi kama serikali tumeweka mkakati mzito wa kuhakikisha kuwa watoto
wetu watakapokuwa watu wazima walikute ziwa Rukwa likiwa salama na samaki wa aina mbalimbali,hivi sasa ziwa
linajaa tope na mchanga kutokana na uharibifu wa mazingira ya mito na
ziwa,hatua zisipochukuliwa kesho na kesho kutwa ziwa linaweza kugeuka kuwa
bwawa’’,alisema.
Kulingana na mkuu wa wilaya sheria ipo wazi ya faini ya shilingi laki
tatu kwa mtu anayelima katika ardhi oevu, kulisha mifugo au kulima kwenye eneo
la hifadhi
Mkuu wa wilaya ameyataja madhara ya mito mikubwa ya Songwe na Lupa
kushindwa kupeleka maji katika ziwa Rukwa ni pamoja wakazi wote wa tarafa za Songwe na Kwimba
ambao wanategemea samaki kama kitoweo kukosa samaki,wavuvi watakosa
ajira,chakula bora kitakosekana na viumbehai wote wanategemea ziwa hilo
watapata athari mbalimbali za kimazingira na hata wengine kutoweka kwenye uso
wa dunia.
Mifugo mingi iliyopo katika bonde la
Songwe inayokadiriwa kuwa zaidi ya 500,000 imesababisha fukwe za ziwa Rukwa
upande wa Bonde la Songwe zilizopo kwenye vijiji vya kata ya Totowe
kukauka na kusababisha ziwa hilo kupungua ukubwa na kina hali
inayohatarisha uwepo wa ziwa hilo ambalo linashika nafasi ya nne kwa ukubwa
hapa Tanzania likitanguliwa na maziwa ya Tanganyika,Viktoria na Nyasa.
Fukwe ambazo zinapotea kwa kasi
ni pamoja na fukwe ya Handeni ambayo imekauka kwa kilometa 10,Ihovyo kilometa
tatu,Mtanda kilometa saba,kisiwani kilometa tisa,kambipotea kilometa
tano,Kwaboko kilometa sita na fukwe ya Mchangani kilometa tano.Kina cha
maji katika fukwe hizo hivi sasa ni chini ya meta moja .
“Fukwe hii ya kisiwani mwaka 1998
ilikuwa kilometa nane kutoka hapa ,unaweza kutembea katika kina cha maji chini
ya magoti hadi umbali wa meta 300 ndani ya ziwa,hali hii ikiendelea ziwa hili
linaweza kukauka au kuwa bwawa ’’, anasema John Mwakyoma mvuvi katika ziwa
Rukwa.
Peter Sasawata na Stanley Rwamba
ni wavuvi katika fukwe ya Mtanda wanasema fukwe hiyo mwaka 1994 ilikuwa
kilometa saba kutoka hapo ilipo leo na kwamba chanzo kikuu cha kukauka kwa
fukwe ni mifugo mingi ambayo inaingia kunywa maji na kula malisho ndani ya ziwa
kila siku.
“Mimi nimeishi katika kijiji cha
Ihovyo kwa miaka 11 wakati nafika hapa maji ya ziwa hili ulikuwa unayakuta
baada ya kutembea kwa dakika tano tu lakini hivi sasa inakulazimu kutembea
zaidi ya saa mbili ndipo unalikuta ziwa ’’,anasema Beston Mwambene mwalimu wa
shule ya msingi Ihovyo .
“Kama kweli serikali inataka
kuliokoa ziwa Rukwa lisipotee kwenye uso wa Dunia,waache kuendekeza siasa
kwenye mazingira, ziwa Rukwa litakauka, wakulima wanazidi kusogeza mashamba ya
mpunga kwenye fukwe za ziwa’’,anasisitiza Mwambene.
Afisa wa bonde la maji la Rukwa
Idris Msuya anasema kuwa maelfu ya
mifugo ambayo inaishi, kula na kunywa maji ziwa Rukwa kwenye
fukwe za kijiji cha Totowe inatishia
uwepo wa ziwa hilo.
Hata hivyo Msuya alikiri
kina cha maji cha ziwa Rukwa kinaendelea kupungua kwa kasi mwaka hadi mwaka
kutokana na uharibifu wa mazingira unaochangiwa na idadi kubwa ya ng’ombe
katika wilaya zinazozunguka ziwa Rukwa ambazo alizitaja kuwa ni Chunya, Mbeya,
Sumbawanga, Mpanda, Mbozi na Nkasi.
Kulingana na Msuya, Ziwa Rukwa hivi
sasa lina wastani wa kina cha juu cha maji cha mita tisa tu kiasi ambacho kitaalamu ni mbaya na kwamba kina
cha chini ni mita nne , eneo la maji la ziwa hilo ni kati ya kilometa 800
hadi 2300 kutegemeana na kiasi cha mvua inayonyesha na kwamba utafiti umebaini kuwa
katika kipindi cha mwaka 1970 hadi 2006
Ziwa Rukwa limepungua kwa kiasi cha zaidi ya kilomita saba.
![]() |
| Mto Songwe,mto pekee unaomwaga maji ziwa Rukwa kwa mwaka mzima |
Waziri
wa maji Profesa Jumanne Maghembe ametahadharisha kuwa kuna hatari kubwa ya Ziwa
Rukwa kukauka katika kipindi cha miaka kumi ijayo endapo uharibifu wa mazingira
na uchafuzi wa vyanzo vya maji unaofanywa na wakazi wa maeneo yanayozunguka
ziwa hilo hautadhibitiwa haraka.
Profesa Maghembe ametoa rai kwa mamlaka
zinazohusika kujipanga vizuri ili
kukabiliana na uharibifu mkubwa wa mazingira ikiwemo kutumia sheria ndogo ndogo
zilizopo kila Halmashauri nchini ili kudhibiti uharibifu wa mazingira
unaofanywa na baadhi ya watu katika
vyanzo vya maji.
Kulingana na Prof. Maghembe Sheria ndogo ndogo zilizotungwa na Halmashauri hazinabudi kuanza kutumika ili kudhibiti tabia iliyojitokeza hivi sasa ya baadhi ya watu kulima katika vyanzo vya maji.
Utafiti ambao ulifanywa katika Ziwa Rukwa kata za Ivuna na Kamsamba wilayani Momba umebaini viumbe hai wakiwemo ndege maarufu aina ya nyange nyange na bata maji wapo katika hatari ya kutoweka kutokana na fukwe nyingi kukauka na ziwa kujaa tope.
Waziri mkuu, Mizengo Pinda amesema kuwa Ziwa Rukwa lipo hatarini kukauka, kutokana na kina chake cha maji kushuka. Akizungumza wakati wa uzinduzi wa kitabu cha Sumbawanga ng’ara kinachohusu masuala ya udhibiti wa mazingira, Pinda alisema katika kipindi cha miaka 50 ijayo ziwa hilo litakuwa limekauka.
Kufuatia kuwepo kwa hali hiyo waziri mkuu amemuagiza Mkuu wa Mkoa wa Rukwa, Injinia Stella Manyanya kwa kushirikiana na Ofisi ya Makamu wa Rais (mazingira) kuhakikisha wanalifanyia kazi suala hilo ili kulinusuru ziwa hilo.
Wataalamu wa mazingira wanazitaja baadhi ya
athari zitokanazo na uharibifu wa mazingira duniani kuwa ni pamoja na kupungua kwa mvua, majira
kubadilika na kuongezeka kwa vipindi vya ukame, kupungua kwa kasi ya theluji
katika ncha ya kaskazini na kusini na kwenye vilele vya milima kote dunia ukiwemo mlima Kilimanjaro.
Athari
nyingine ni kupungua kwa kina cha maji
katika maziwa mbali mbali na katika nchi yetu maziwa yanayoathirika ni Ziwa
Tanganyika, Victoria na Ziwa Rukwa, kuongezeka kwa kina cha bahari na kuathiri
maeneo ya nchi kavu baadhi yake yamezama na mengine yako hatarini kuzama ambapo
hapa Tanzania kisiwa cha Maziwe kilichopo katika Bahari ya Hindi kimezama.
albano.midelo@gmail.com,simu 0766463129



No comments:
Post a Comment