 |
| Waziri wa fedha Dk.William Mgimwa |
KAMATI ya Bunge ya Hesabu za
Serikali za Mitaa (LAAC) imebaini mtandano wa baadhi ya maofisi wa Hazina
ambao kwa kushirikiana na halmashauri wanachote fedha za serikali kwa njia
ya kuzidisha viwango vinavyokuwa vimeombwa.
Akizungumza na waandishi wa
habari katika ofisi ndogo za Bunge jijini Dar es Salaam, mwenyekiti wa
kamati hiyo, Rajab Mohamed Mbarouk, alisema kupitia mtandao huo wa kifisadi
zaidi ya sh bilioni moja zimetoroshwa kutoka Hazina kupitia halmashauri
mbalimbali nchini.Alisema mchezo huo umefanywa na
baadhi ya watendaji wasiokuwa waaminifu na kuzitaja baadhi ya halmashauri
za wilaya hizo kuwa ni Mbarali ambako waliingiziwa sh milioni 700 na hazina
badala ya sh milioni 70 zilizokuwa zimeombwa.Mbarouk aliitaja pia halmashauri
ya wilaya ya Korogwe mjini kuwa iliingiziwa milioni 500 wakati ile ya
Mvomero nayo ikingiziwa sh milioni 89 zaidi ya mahitaji yao.
Alisema mtandao huo wa walanguzi
baada ya kutekeleza azma yao hiyo huzitakatisha fedha hizo kwa kuzirudisha
kwa ajili ya maslahi yao binafsi na hivyo kuitia hasara serikali.
“Tulichogundua ni utoroshaji wa
fedha nyingi za serikari kutoka hazina kwenda kwenye njia haramu jambo
lililotushangaza,” alisema.
Akizungumzia hati za hesabu
zisizoridhisha za halmashauri nchini, Mbarouk alisema katika kipindi cha
mwaka wa fedha uliopita, zimepungua ikiliganishwa na kipindi cha nyuma.
Alisema kiumjumla bado yapo
matatizo ya watendaji wa halmashauri hizo kutokuwa na nidhamu ya fedha
zilizotengwa kwa ajili ya miradi ya maendeleo ya wananchi.
“Halmashauri nyingi zimekutwa na
matumizi ya fedha za miradi huku baadhi ya watendaji wakishindwa kutoa
maelezo ya jinsi zilivyotumika jambo ambalo linatia shaka wakati wote,”
alisema.
Mbarouk alisema kamati
imewaagiza wakurugenzi wote wahakikishe kila tofauti iliyojitokeza kipindi
hiki inasawazishwa na isitokee tena.
Wakati huohuo, Kamati ya Bunge
ya Hesabu za Serikali (PAC) imekataa kupitisha ripoti ya hesabu ya mwaka
2011/12 za Mamlaka ya Bandari Tanzania (TPA) kutokana na dosari ikiwemo
kufanya matumizi ya sh bilioni tisa kwa ajili ya kulipana posho za vikao vya
mabaraza ya wafanyakazi.
Mbali na hilo ripoti hiyo
imebaini mamlaka hiyo kufanya manunuzi yao kiholela bila kuzingatia sheria
ya manunuzi ya umma ambapo walitumia sh bilioni 30 kwa manunuzi ya vifaa
bila kuwa na kibali cha Wizara ya Fedha na Uchumi.
Akizungumza jana na watendaji wa
mamlaka hiyo walioambatana na Mwenyekiti wa Bodi wa Bandari, Makamu
Mwenyekiti wa PAC, Deo Filikunjombe, alisema kuwa kamati imeikataa ripoti
hiyo na wanamuandikia barua Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali
(CAG), Ludovick Utouh, ili kufanya ukaguzi maalum katika maeneo yenye
dosari.
Filikunjombe alisema kuwa CAG
atalazimika kupitia upya maeneo hayo ambayo hesabu zake zina utata ikiwemo
matumizi ya sh bilioni 6.2 yaliyofanywa na mamlaka hiyo kwa ajili ya
kugharamia matangazo.
“Huu ni uzembe na ni lazima hili
lifanyiwe ukaguzi. Hivi unaposema mmetumia sh bilioni 6.2 kwa ajili ya
matangazo ina maana leo kila Mtanzania ukimuuliza shughuli mnazofanya
atakuwa anazifahamu?” alihoji.
Aliongeza kuwa taarifa za
matangazo hayo zinaonekana tofauti katika ripoti hiyo wakati ni kitu
kimoja.
“Unaposema katika ripoti
umefanya publicity na advertisement kwa gharama tofauti hapo unamaanisha
nini, hicho si ni kitu kimoja jamani au nakosea,” alisema.
Kiukweli ni kuwa publicity
hailipiwi isipokuwa advertisement.
Alisema kuwa Utouh anatakiwa
kufanya ukaguzi pia katika eneo la safari za watendaji wa mamlaka hiyo
ambao wametumia sh bilioni 10 kwa ajili ya posho za safari pekee.
Filikunjombe aliwataka watendaji
hao kuwa wazi iwapo matumizi hayo yamekuwa yakihusisha na wizara ya
uchukuzi.
“Labda mkurugenzi utueleze kama
fedha hizo zinagharamia na watu wa wizara yenu maana kuna maeneo mengine
tumepata malalamiko hayo ya mamlaka kuombwa fedha.”
Alisema kuwa katika ripoti hiyo
kwa mara nne mfululizo imeonyesha jinsi mamlaka hiyo inavyoshindwa
kuzingatia manunuzi ya umma hatua iliyosababisha kufanya manunuzi yao
kiholela ya kununua vifaa vya sh bilioni 30 bila kibali.
Filikunjombe ambaye ni mbunge wa
Ludewa (CCM), alisema kuwa mamlaka imetumia sh bilioni 3.2 kwa ajili ya
kulipa matibabu ya wafanyakazi na kutaka kuanzia sasa mamlaka hiyo ijiunge
na Mfuko wa Bima ya Afya ili kuepuka upotevu wa fedha za serikali.
“Yaani kuna wizi unaofanyika
huwezi kusema umejaza magari mafuta ya lita 100; ni gari lipi hilo lazima
tuangalie hilo na CAG afanye ukaguzi upya na tutakutana nanyi Desemba mwaka
huu,” alisema.
Naye mjumbe wa kamati hiyo,
Esther Matiku (CHADEMA), alihoji hatua ya mamlaka hiyo kumpatia zabuni ya
ujenzi wa mnara wa Bandari ya Mtwara mzabuni ambaye hakushinda huku
akiachwa aliyeshinda na ambaye ana vigezo.
Alishangazwa na mamlaka hiyo
kuamua kuunganisha kwa pamoja thamani ya ardhi na majengo yao jambo ambalo
limewasababishia kupata hati chafu.
Mbunge wa Nkasi Kaskazini, Ally
Keissy (CCM), alihoji sh milioni 100 zilizotolewa kwa mkandarasi wa bandari
ya Tanga ambaye hakufanya kazi hiyo na badala yake alitokomea
kusikojulikana.
Akijibu hoja hizo, Mkurugenzi
Mkuu wa mamlaka hiyo, Madeni Kipande, alikiri kuwepo kwa tatizo hilo na
kusema kuwa kazi hiyo ilikuwa ifanyike kwa sh milioni 500 lakini walitoa
fedha za kuanza kazi sh milioni 100.
CHANZO GAZETI LA TANZANIA DAIMA
|
No comments:
Post a Comment