MADINI yenye thamani kubwa aina ya shaba ya
bluu(blue copper)yamegundulika katika kata ya Mbesa tarafa ya Nalasi wilayani
Tunduru mkoani Ruvuma.
Kugundulika
kwa madini hayo kunaifanya wilaya ya Tunduru kuwa ndiyo wilaya pekee nchini na
Afrika mashariki kuwa na madini ya shaba ya bluu.
Mkuu
wa wilaya ya Tunduru Chande Nalicho amesema utafiti unaonyesha kuwa tarafa
nzima ya Nalasi ina utajiri wa madini hayo ambayo yanaweza kuchangia kuinua
uchumi wa wilaya hiyo,mkoa wa Ruvuma na Taifa kwa ujumla wake.
“Utafiti
umebaini kuwepo kwa madini ya shaba ya bluu karibu tarafa nzima ya Nalasi
hadi mto Ruvuma mpakani na nchi jirani
ya Msumbiji na pia madini hayo yamesambaa hadi mpakani na wilaya ya Namtumbo
hii ni shaba yenye thamani kubwa ’’,alisema Nalicho.
Wataalamu
wa madini wanaelekeza kuwa madini ya shaba ya bluu yana thamani kuzidi madini
ya shaba aina nyingine zote ikiwemo shaba nyekundu ambayo inachimbwa katika
nchi jirani ya Zambia.
![]() |
| Chande Nalicho DC wa Tunduru akionyesha Blue copper |
Hivi
sasa wachimbaji wadogo wadogo wa madini hayo wapo katika eneo hilo la madini
tangu mwaka 2010 na kwamba utafiti kuhusiana na madini hayo bado unaendelea
kabla ya serikali kupitia wizara ya madini kuanzishwa mgodi rasmi wa madini
hayo.
Utafiti
wa awali wa kijiolojia uliofanyika kwa mara ya kwanza mwaka 1988 katika eneo la
Kata ya Mbesa wilayani Tunduru mkoani Ruvuma umebaini kuwepo kwa madini mengi
aina ya shaba ya bluu(Blue copper).
Utafiti
huo ulifanywa na Wakala wa Jiolojia Tanzania (GST) kuonyesha kuwepo kwa madini aina ya shaba ya
bluu ambapo utafiti wa karibuni uliofanyika mwaka 2010 umebaini ubora wa
mashapo ya shaba ya bluu katika eneo hilo.
Kwa mujibu wa taarifa ya wizara ya madini, utafiti umebaini kuwa madini ya shaba ya bluu yanaweza kuchimbwa kwa faida na kwamba hatua hii ya utafutaji madini inahitaji utaalam, vifaa vya kisasa na fedha nyingi. Aidha Serikali inaendelea kuimarisha STAMICO ili iweze kuwa na uwezo wa kufanya shughuli hizo za utafutaji na uchimbaji madini kwa maslahi ya Taifa badala ya kutegemea zaidi kampuni binafasi.
Hata
hivyo serikali wilayani Tunduru Imetoa miezi miwili kwa kampuni ya IGA &
MWAKI Co. LTD inayo fanya shughuli za uchimbaji wa madini aina ya shaba ya bluu
katika Kijiji cha Mbesa Wilayani humo kukamilisha taratibu za kisheria
vinginevyo itasimamishwa kuendelea kufanyakazi katika eneo hilo.
Mwenyekiti wa kamati ya ulinzi na Usalama,
Mkuu wa Wilaya hiyo Chande Nalicho ametoa agizo hilo baada ya kujionea mambo
mengi vikiwemo vitendo vya kuendesha uchimbaji huo huku wakiwa hawana vibali
vinavyo waruhusu kuendesha shughuli hizo katika mgodi huo.
“Natoa miezi miwili ambayo mwisho wake
utakuwa mwezi Julai mwaka huu muwe mmekamilisha taratibu zote za kisheria
vinginevyo nitachukua hatua kali za
kisheria ikiwa ni pamoja na kuufunga mgodi huu’’,alisisitiza.
Akifafanua taratibu zilizokiukwa na
wamiliki wa mgodi huo kaimu afisa mazingira wa Wilaya ya Tunduru Eberhard Halla
alisema kuwa kampuni hiyo imekuwa ikiendesha shughuli hizo bila kufanya tathimini
za Athari kwa Mazingira (Environmental Impact Assessment) pamoja na kutokuwa na
mikataba ya kisheria kati ya Kampuni na kijiji cha Mbesa ambacho ndiyo mmiliki
wa eneo linalochimbwa madini hayo.
Halla amezitaja taratibu nyingine ambazo
zimekiukwa na kampuni hiyo kuwa ni pamoja na kutowapatia Wachimbaji wao vifaa
vya kujikinga na madhara mbalimbali (Protective gears) yatokanayo na uchimbaji
madini hayo hali ambayo inahatarisha afya zao.
Alisema kutokana na kampuni hiyo
kutotimiza vigezo hivyo inakiuka kanuni na taratibu zinazo simamia sheria ya
mazingira namba 20 ya mwaka 2004 ya uendeshaji wa shughuli za migodi hivyo amewataka viongozi hao kuwasiliana na ofisi
za idara ya mazingira ya Halmashauri na ofisi za Baraza la mazingira la Taifa
kanda ya Mtwara inayosimamia mazingira ili kukamilisha taratibu hizo.
Wakijibu tuhuma hizo kwa niaba ya
Meneja wa kampuni hiyo wataalamu wanaosimamia shughuli za uchimbaji wa madini
hayo katika mgodi huo Wahandisi Thomas Katto na Reymond Njota walisema kuwa
kampuni hiyo ilishindwa kutimiza taratibu hizo kutokana na Wilaya hiyo kutokuwa
na wataalamu walioidhinishwa kukusanya tathimini za mazingira na kutoa Cheti.
Hata hivyo walisema kampuni hiyo
inayomiliki eneo la ekari 30 katika milima ya Kijiji cha Mbesa ilianza kuchimba
madini hayo mwaka 2010 kwa kutumia Majembe na Sululu na kufanikiwa
kuajiri hadi zaidi ya wafanyakazi 70 na kwamba kwa hivi sasa wanatumia vifaa
vichache vya kisasa hali iliyosababisha uzalishaji kushuka
na kupungua wafanyakazi kutoka 70 hadi 25.
Walisema kushuka kwa kiwango cha
upatikanaji wa madini hayo kunatokana pia na Wilaya ya Tunduru na Kampuni hiyo
kutokuwa na vifaa vya kisasa na wataalamu wa kuchoronga miamba (Geoloist) hivyo
kuchimba madini hayo kwa
kubahatisha.
Mkoa wa Ruvuma ni
miongoni mwa mikoa nchini ambayo ina utajiri mkubwa wa madini mbalimbali ambayo
yakichimbwa kwa vifaa vya kisasa yanaweza kuufanya mkoa kupanda juu kiuchumi na
wananchi wake wakaondokana na umasikini.
Madini yanayopatikana
katika mkoa wa Ruvuma ni makaa ya mawe yaliopo katika wilaya za Mbinga na Songea,madini ya vito yaliyopo wilaya za Tunduru,Mbinga,Namtumbo na
Songea, madini ya dhahabu ambayo yanapatikana Mpepo na Ruhekei wilayani Mbinga
na madini ya uranium ambayo yanapatikana kwa wingi wilayani Namtumbo.
Mkuu wa mkoa mstaafu
Nicodemas Banduka anasema mkoa wa Ruvuma licha ya kuwa gwiji katika uzalishaji
wa mazao ya chakula hivi sasa umepata bahati ya kuwa miongoni mwa mikoa
michache nchini yenye utajiri mkubwa wa madini mengi.
“Mimi baada ya
kustaafu kazi serikalini nikiwa na makampuni fulani ya madini tumefanya tafiti
mbalimbali za madini hapa nchini,baada ya tafiti hizo,katika vitabu vya madini
vilivyopo makao makuu ya wizara ya nishati na madini,vinaonesha kuwa mkoa wa
Ruvuma unaoongoza nchini kwa kuwa na kiwango kikubwa cha madini aina ya makaa
ya mawe na chuma”,anasisitiza.
Kulingana na utafiti
huo mkoa wa Ruvuma unashika nafasi ya pili kwa uwingi wa madini ya dhahabu
ambapo nafasi ya kwanza inashikwa na mkoa wa Shinyanga na kwamba madini ya
chuma ambayo yameanzia Liganga na madini ya makaa ya mawe yaliyoanzia Mchuchuma
yamesambaa na kuenea katika eneo kubwa la mkoa wa Ruvuma.
albano.midelo@gmail.com,simu
0766463129


No comments:
Post a Comment