Ziwa Rukwa upande wa wilaya ya Chunya mkoani Mbeya
linatarajiwa kila mwaka kufungwa kwa miezi sita kwa lengo la kutoa fursa kwa
samaki kuzaliana na kukua.
Katibu tawala wa wilaya hiyo akizungumza kwa niaba
ya mkuu wa wilaya ya Chunya Deodatus Kinawiro alisema serikali imeamua kuchukua
hatua hiyo kufuatia kasi ya kutoweka kwa samaki katika ziwa hilo ambapo hivi sasa wavuvi wanavua samaki
wachanga mfano wa dagaa ambao hawafai kwa kitoweo. Ziwa Rukwa tangu uhuru limetoa ajira
katika sekta ya uvuvi ambapo wavuvi wameweza kusomesha watoto wao,kujipatia
kipato kwa kuuza samaki na kupata kitoweo ambacho kinajenga afya kutokana na
samaki wanaopatikana kwenye ziwa hilo.
Kinawiro alisema kutokana na uharibifu wa mazingira
katika ziwa Rukwa upande wa wilaya ya chunya umesababisha mazalia muhimu ya
samaki ndani ya ziwa hilo kuharibika kutokana na shughuli za kibinadamu
zinazotokana na uingizaji wa mifugo mingi pamoja na uvuvi wa kutumia kokoro
ambao umesababisha samaki wengi kutoweka na kubakia samaki wachanga pekee.
“Kutokana na kasi ya kutoweka kwa samaki ziwa Rukwa
sisi kama serikali ya wilaya ya Chunya tumeamua kuchukua maamuzi magumu ikiwemo
kufunga shughuli zote za kibinadamu katika ziwa Rukwa kwa miezi sita kila mwaka
ili kutoa nafasi kwa samaki kuzaliana ’’,alisisitiza.
Alibainisha kuwa serikali tayari imeandaa na
kukamilisha utaratibu ambao kila baada ya miezi sita shughuli zote za uvuvi
katika ziwa hilo zitasimamishwa na miezi sita baadaye wananchi wataruhusiwa
kuendelea na uvuvi katika ziwa hilo na
kwamba kinachosubiriwa hivi sasa ni idara ya maliasili na uvuvi kupata pesa kwa
ajili ya kuwaelimisha wananchi kuhusiana na mpango huo wa serikali kulifunga
ziwa hilo kila baada ya miezi sita.
Alisema idara hiyo itatoa elimu kwa wananchi kufanya
shughuli mbadala ambazo zitawaingizia kipato katika kipindi cha miezi sita
ambayo ziwa litakuwa limefungwa ili maisha ya wananchi waliokuwa wanategemea
shughuli ya uvuvi pekee yaweze kuendelea.
Uchunguzi ambao ulifanywa na mwandishi wa makala
haya mwaka 2011 katika ziwa Rukwa upande wa wilaya ya Chunya katika fukwe saba
za kata ya Totowe na kata za Ivuna na Kamsamba wilayani Momba mkoani Mbeya
ulibaini kutoweka kwa samaki wa aina mbalimbali maarufu katika ziwa hilo.
Mvuvi Stanley Rwamba(65) mkazi wa kijiji cha
Totowe ziwa Rukwa wilayani Chunya aliwataja jamii ya Samaki ambao wapo katika hatari ya
kutoweka katika ziwa Rukwa ni
ngogo,shibe na kachinga ambao walikuwa wanapatikana kwa wingi wakati wa mvua
miaka kumi iliyopita.
Uvuvi
wa kutumia kokoro unaofanyika katika fukwe za ziwa Rukwa
katika kata za Totowe, Ivuna na Kamsamba mkoani Mbeya umechangia kusababisha samaki katika ziwa hilo
kupungua kwa kasi.
Wavuvi
kwenye fukwe hizo wamebainika kutumia nyavu za kokoro kuvulia samaki licha ya
kwamba nyavu hizo haziruhusiwi kisheria kwa kuwa zinaharibu mazalia ya samaki pamoja na kuvua samaki
wadogo.
Fukwe
ambazo uvuvi wa kutumia kokoro umekithiri katika kata ya Totowe ni Handeni, Ihovyo, Mtanda, Kambipotea, Kwaboko, Mchangani
na Kisiwani.Mwandishi wa makala haya alishuhudia wavuvi wanavua bila kuwa na hofu ya kukamatwa na
maofisa uvuvi ambao wanadaiwa kuchangia hali hiyo kuendelea kwa kuwa
hawaonekani katika sehemu zao za kazi.
Staniley
Rwamba mvuvi mkongwe katika ziwa Rukwa anasema wavuvi wameamua kutumia kokoro
ambazo haziruhusiwi kisheria kutokana na samaki wanaoruhisiwa kuvuliwa kisheria
katika ziwa hilo kuanza kutoweka.
Hata
hivyo wavuvi ambao walikuwa wanavua
katika ziwa hilo kila mahali walionekana kukosa samaki ,ambapo wavuvi
wanadai hali hiyo inachangiwa na idadi kubwa ya ng’ombe ambao wametia kambi
kwenye fukwe za ziwa Rukwa ambao hula malisho ambayo ni mazalia ya samaki ndani
ya ziwa hilo.
Bonifasi
Yamlinga ni mvuvi katika fukwe ya Mchangani anasema maelfu ya ng’ombe kila siku
wanaingizwa hadi mita 500 ndani ya ziwa Rukwa kula nyasi ambazo ni mazalia ya
samaki .
Licha
ya mifugo kuharibu mazalia ya samaki katika ziwa Rukwa wataalamu wa mifugo
wanabainisha kuwa ng’ombe mmoja ana uwezo wa kunywa maji zaidi ya lita 40 kwa
mkupuo ambapo idadi ya zaidi ya ng’ombe 500,000 wanaoingia kunywa maji ziwa
Rukwa kwa siku katika fukwe za ziwa
Rukwa wilayani Chunya wanakunywa zaidi
ya lita milioni 20.
Takwimu zinaonyesha kuwa Halmashauri ya wilaya
ya Chunya ilikuwa na mifugo zaidi ya 800,000 hadi kufikia Desemba 2010 mifugo
mingi ikiwa katika bonde la Songwe ambalo
lina malisho ya kutosha na maji yanayopatikana kwa urahisi kutoka ziwa Rukwa na
mito ya Lupa na Songwe.
Yamlinga anabainisha kuwa licha ya samaki wengi wanaovuliwa ziwa Rukwa upande wa Chunya kuwa ni wale ambao hawaruhusiwi kuvuliwa kisheria, amedai hakuna afisa samaki wa kata anayehoji uhalali wa kuvua samaki hao hali ambayo inasababisha wavuvi kuwa huru na kuendelea kufanya uvuvi haramu katika ziwa Rukwa.
Hata hivyo afisa uvuvi na maliasili wa Halmashauri ya wilaya Momba Agrey Ngalunga baada ya kuona samaki wengi wachanga wanaovuliwa ziwa Rukwa katika kata za Ivuna na Kamsamba alidai serikali ya wilaya hiyo ilitoa ombi kwa Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi, ili wafunge shughuli za uvuvi kwa miezi minne kuanzia Januari hadi Aprili kila mwaka ili samaki waweze kuzaliana maombi ambayo bado hayajakubaliwa.
Kulingana na Ngalunga mwaka 2010 kamati ya ulinzi na usalama wilaya ya Momba kwa kushirikiana na kikosi cha
usimamizi wa raslimali uvuvi cha Tunduma waliweza kukamata nyavu haramu kwenye maduka mjini Tunduma
zipatazo 2236 zenye thamani zaidi ya
shilingi milioni 137 ambazo ziliteketezwa hadharani kwa moto.
Wavuvi kutoka fukwe za Kwaboko, Mtanda, Handeni
na kisiwani ambao ni Peter Sasawata,Staniley Rwamba na John Sichalwe wanadai kuwa kutoweka kwa samaki kunatokana na kina cha maji kupungua,uvuvi wa
kutumia kokoro unaofanywa na baadhi ya wavuvi katika ziwa hilo pamoja na mifugo mingi
inayokula nyasi ambazo ni mazalia ya samaki.
Peter Sasawata mvuvi katika ziwa Rukwa anasema kuwa kwa wiki moja hadi mbili wavuvi wamekuwa wakivua si zaidi ya samaki watano aina ya kachinga ambapo miaka michache nyuma samaki hao walikuwa wanapatikana kwa wingi,ameshauri juhudi za watalaamu na serikali zinahitajika ili kukabiliana na uharibifu wa mazalia ya samaki ili kuzinusuru aina mbalimbali za samaki.
“Kabla
ya uharibifu katika ziwa hili, miaka ya nyuma ziwa hili lilikuwa linavutia,
kulikuwa na wanyama kama viboko, mamba lakini hivi sasa wanyama hao wamekimbia,
hata samaki wamepungua, unaweza kukaa mwezi mzima bila kula samaki,” alisema
Elivathan Silwimba, Ofisa Uvuvi Kata ya Ivuna.
John Sichalwe amewataja samaki wengine ambao hivi sasa wameanza kutoweka kuwa ni magege na kapimoja na kwamba samaki aina ya kambare bado wanapatikana kwa wingi kwa kuwa samaki hao wanapenda kuishi katika matope ambayo yapo mengi ndani ya ziwa Rukwa ambalo kina chake kimejaa tope na mchanga.
Utafiti uliofanywa kwenye fukwe katika
ziwa Rukwa unaonyesha dhahiri serikali imeshindwa kusimamia sekta ya uvuvi na kusababisha kuendelea kuvuliwa
kwa samaki wachanga wanaotokana na tatizo la uvuvi haramu hivyo hatua ya
serikali ya wilaya ya Chunya kuamua kuchukua maamuzi magumu ya kulifungia ziwa
Rukwa kwa miezi sita pamoja na kuendeleza mapambano dhidi ya uvuvi haramu
inafaa kuigwa katika maeneo mengine nchini .
Sensa ya samaki ambayo ilifanywa mwaka 1999
katika ziwa Rukwa ilibaini kuwa ziwa
hilo linazalisha samaki tani 7000 kwa mwaka wakiwemo aina tatu za kambale
ambazo ni kibonde,singa na poroko,aina nyingine ni magege, dagaa, kapimoja na
kachinga.Wilaya zinazopitiwa na ziwa Rukwa ni pamoja na Chunya na Momba mkoani
Mbeya, Sumbawanga na Nkasi mkoani Rukwa na Mpanda mkoani Katavi.
Hata hivyo Sera ya Taifa ya mazingira ya mwaka
1997 kuhusu sekta ya uvuvi kifungu cha 60 inaelekeza wazi kuwa uvuvi
utaendelezwa vema kwa kutumia vifaa vya
uvuvi vinavyofaa na njia bora za kuendeleza bidhaa zinazotokana na uvuvi
ambapo njia zinazoharibu mazingira
katika uvuvi zinadhibitiwa kwa sheria na kuhakikisha unafuu wa upatikanaji wa vifaa bora vya uvuvi
.
albano.midelo@gmail.com,simu
0766463129

No comments:
Post a Comment