Saturday, August 31, 2013

Watanzania mengi ya kujifunza Afrika ya kusini



Sehemu ya jiji la Johannasburg nchini Afrika ya kusini

Na Albano Midelo

HIVI karibuni nimemaliza mafunzo maalum ya uhifadhi nchini Afrika ya kusini ambako nimeweza kutembelea maeneo karibu yote muhimu katika nchi hiyo inayotajwa kuwa na maendeleo makubwa hata kuzidi baadhi ya nchi za Ulaya.

Takwimu za uchumi duniani zinaonyesha kuwa nchi ya kwanza kwa uchumi mzuri ni Marekani ikifuatiwa na nchi ya China ambapo nchi ya Afrika ya kusini inashika nafasi ya tatu kiuchumi duniani.Hata hivyo nchi ya China inadaiwa mwaka 2050 itakuwa nchi ya kwanza kwa uchumi bora duniani ambayo inatarajia kuizidi Marekani mara mbili.
 Katika makala haya nitayaweka wazi baadhi ya mambo ambayo mimi binafsi yamenifurahisha kiasi kwamba endapo nchi yetu inaweza kuiga baadhi ya mambo basi tunaweza kupiga hatua katika maendeleo ya kijamii,kiuchumi na kisiasa.Wananchi wa Afrika ya kusini sasa wanachapa kazi kwa bidii huku uzalendo wa kweli katika nchi yao wakiwa wameuweka mbele kuliko kitu chochote.


Jambo la kwanza ambalo limenifurahisha katika nchi ya Afrika ya kusini ni serikali ya nchi hiyo kuwajali wananchi wake kwa kutambua kuwa mwananchi ndiyo mwajiri mkuu wa viongozi wote serikalini kuanzia ngazi ya chini hadi Rais wa nchi.

Moja ya barabara za Afrika ya kusini zenye viwango vy
Katika nchi ya Afrika ya kusini kila mwananchi anaruhusiwa kuingia eneo la Ikulu ya nchi hiyo iliyopo Pretoria kuanzia asubuhi hadi saa 12 jioni ambako anaweza kufanya lolote ikiwa ni pamoja na kupiga picha na kufanya mazoezi ndani ya viwanja vya Ikulu bila kuomba kibali serikali.

Hapa nchini jambo hilo ni ndoto kwani Ikulu ya Dar es salaam huwezi kuingia bila kibali,watanzania wanaogopa eneo la Ikulu kwa kuwa ni makazi ya Rais,lakini nchini Afrika ya kusini wananchi wanaingia Ikulu kama nyumbani kwao unaweza kupiga picha na kufanya lolote hakuna mtu anayekuuliza kwanini Tanzania tusiige jambo hili ili watu waweze kuingia Ikulu bila mizengwe.

Jambo la pili ambalo limenifurahisha nchini Afrika ya kusini ni utaratibu mzuri waliouweka kuhusu askari wa barabarani ambao wamedhibitiwa kiasi kwamba hawana nafasi ya kuchukua rushwa kutoka katika vyombo vya moto vya usafiri kama ilivyo hapa Tanzania.

Katika nchi ya Afrika ya kusini kila mtu anafahamika mtaa na namba ya nyumba anayoishi,hata kama nyumba hiyo ni ya chumba kimoja imepewa namba.Pia kila mwenye chombo cha usafiri anafahamika endapo amefanya kosa la barabarani ,wenzetu wameweka kamera maalum ambazo zinapiga picha makosa yote yanayotokea barabarani.

Iwapo dereva amefanya kosa barabarani kwa mfano kwenda mwendo kasi anapigwa picha na siku inayofuata analetewa faini nyumbani kwake ili aweze kulipa kulingana na kosa lake hivyo askari wa barabarani hawana nafasi ya kuomba rushwa kama ilivyo hapa Tanzania ambapo askari wa barabarani kuomba rushwa kwa madereva imekuwa ni kitega uchumi chao kwa kuwa wanaomba rushwa bila aibu.

Nadhani utaratibu kama wa Afrika ya kusini ungefanyika hapa nchini rushwa kwa askari wa barabarani ingemalizika na pesa nyingi ingeingia serikalini,utaratibu huu ungepunguza makosa ya barabarani kama ilivyo nchini Afrika ya kusini ambako hata ajali zinatokea mara chache ,madereva wapo makini kuhofia kufanya makosa ambayo yangedhibitiwa.

Katika usafiri wa abiria wa daladala nchini Afrika ya kusini  wenzetu wamepiga hatua kubwa kwa kuwa wameweka utaratibu mzuri ambapo daladala zinabeba watu wanaokuwa wamekaa kwenye viti,tena katika daladala hizo hakuna kondakta,abiria waliopo wakiwa tayari abiria mmoja anamkusanyia dereva pesa na kumkabidhi kisha gari linaondoka. Hapa Tanzania daladala zetu kila mmoja anajua kero iliyopo.

Jambo la tatu ambalo limenifurahisha sana ni wananchi wa Afrika ya kusini kuwa na uzalendo wa kweli katika nchi yao.Serikali ya Afrika ya kusini ni mfano wa kuigwa kutokana na kumpatia heshima kubwa Rais mstaafu Nelson Mandela ambapo nyumbani kwake SOWETO wameanzisha makumbusho maalum ya Nelson Mandela.

Makumbusho hiyo ina kila kitu cha Rais mstaafu Mandela ikiwemo Nyumba yake,vitu mbalimbali alivyotumia kama vile kitanda alichokuwa analalia,mkanda wa ngumi alioshinda wakati anacheza mchezo wa ngumi,viatu vyake,samani mbalimbali alizotumia,barua alizokuwa anaandika akiwa gerezani,miti aliyopanda pamoja na vivutio vingine vingi ambavyo vinawavutia wengi wanaotembelea SOWETO katika nyumba ya Mandela.

Unapofika katika nyumba ya Mandela muda wote unakutana na watalii kutoka nchi mbalimbali duniani ambao wanalipa fedha nyingi kuangalia vivutio na kupata habari za Rais mstaafu Nelson Mandela.

Makumbusho ya Nelson Mandela ya SOWETO imeanzishwa mara baada ya kustaafu kwa Rais huyo kipenzi cha watu wa Afrika ya kusini.Watanzania tumeshindwa kuanzisha makumbusho ya mwalimu Nyerere licha ya kwamba amefanya mengi katika nchi hii.

Hata hivyo hatujachelewa serikali inaweza kuanzisha makumbusho ya mwalimu Nyerere na kuweka vitu vyote alivyofanya kabla ya kuwa Rais,baada ya kuwa na Rais na mara baada ya kustaafu kama wenzetu Afrika ya kusini wanavyomuenzi Rais wao kila kona ya nchi yao ambako wameweka picha yake na maeneo mengine wameweka video yake ambayo inaonyesha kazi alizokuwa anafanya kwa ajili ya Afrika ya kusini.

Mzee Mandela ingawa hivi sasa anaumwa yupo mahututi katika hospitali ya Medical Clinic mjini Pretoria,bado serikali ya nchi hiyo inauzalendo wa hali ya juu kwa kuwa kutokana na nafasi ya mzee Mandela katika nchi hiyo angeweza kwenda kutibiwa katika nchi za  Ulaya na Marekani ambazo zinaaminika kuwa na hospitali zenye huduma bora zaidi,hata hivyo serikali inayoongozwa na Rais Zuma imeamua kumtibu mzee Mandela ndani ya nchi yao huu ni uzalendo unaofaa kuigwa na nchi nyingine kama Tanzania ambayo viongozi wake wengi wakiugua wanakwenda kutibiwa nje ya nchi.

Jambo jingine ambalo watanzania tunatakiwa kujifunza kutoka Afrika ya kusini ni uzalendo walionao katika maliasili za Taifa ambapo idadi ya wananchi wanaofanya utalii wa ndani ni kubwa kuliko watalii wanaotoka nje. Hapa Tanzania ni tofauti tunategemea zaidi watalii wa kutoka nje ya nchi hivyo endapo watalii wa nje wanapungua sekta ya utalii inaathirika kwa kuwa watanzania hatuna utamaduni wa kufanya utalii wa ndani.

Hata hivyo hali hiyo inachangiwa na serikali kwa mfano sekta ya utalii nchini Afrika ya kusini kila mwaka inatengewa bilioni 200 wakati hapa Tanzania inadaiwa serikali inatenga shilingi bilioni sita tu kwa ajili ya utalii.

Vivutio vya utalii vilivyopo nchini Afrika ya kusini kama vile hifadhi ya Taifa ya Kluger ambayo inatajwa kuwa kubwa kuliko zote barani Afrika haina wanyama wengi kama zilivyo hifadhi za Taifa za Tanzania za Serengeti,Ziwa Manyara,Mikumi,Ruaha na nyinginezo ambazo zina wanyama wengi wa aina mbalimbali ambao wanapatikana kirahisi.

Katika hifadhi ya Kluger wanyama ni wa kutafuta,anapatikana mmoja mmoja lakini kwa kuwa serikali ya nchi hiyo imewekeza kikamilifu katika sekta ya utalii kwa kuitangaza hifadhi hiyo,watalii wengi wa ndani na nje ya nchi wanaitembelea hifadhi hiyo kila siku na serikali kuingiza fedha nyingi ambazo zinaimarisha uchumi wa nchi ya Afrika ya kusini hivyo basi serikali ya Tanzania inatakiwa kubadilika na kuongeza bajeti kwa ajili ya matangazo ya vivutio kwenye sekta ya utalii ili kupata mafanikio makubwa katika sekta hiyo.

Sio hayo tu katika nchi ya Afrika ya kusini sio jambo rahisi kwa wafanyabiashara wakubwa na wananchi wa kawaida kukwepa kulipa kodi kutokana na utaratibu mzuri ambao umewekwa na nchi hiyo unapoingiza bidhaa toka nje,kununua na kuuza ambapo serikali inapata kodi yake kikamilifu na hakuna ukwepaji kodi kama unaofanyika hapa nchini.Bidhaa za ndani ya nchi hiyo zimepewa kipaumbele na hakuna bidhaa feki zinazoingizwa nchini Afrika ya kusini tofauti na hapa nyumbani Tanzania ambako ni jalala la bidhaa feki.

Wenzetu katika utunzaji wa mazingira wamepiga hatua kubwa kwa mfano ukitembelea katika mitaa ya jiji la Johannesburg huwezi kuona takataka ambazo zimezagaa ovyo kama ilivyo katika jiji letu la Dar es salaam,ukiangalia barabara za jiji la Johanasburg zinavyovutia unaweza usitamani kuondoka katika jiji hilo.

Magari yaliopo katika jiji la Johansberg yanatajwa kuwa ni mengi zaidi ukilinganisha na idadi ya magari yaliopo katika jiji la Dar es salaam,hata hivyo kutokana barabara bora zilizojengwa chini,katikati na juu zinasababisha jiji hilo kutokuwa na foleni ya magari kama iliyopo jijini Dar es salaam ambako foleni imekuwa kero kubwa kwa wakazi wa jiji hilo.

Kuna mengi ambayo tunaweza kujifunza kutoka nchini Afrika ya kusini,kinachotakiwa ni kubadilika kifkra na kimawazo kuanzia viongozi wetu waliopo madarakani hadi wananchi.Natambua kuwa kutokana na maendeleo makubwa iliyonayo nchi ya Afrika ya kusini,tunaweza kukata tamaa na kusema kuwa hatuwezi kujilinganisha na nchi hiyo badala yake labda tuendelee kujilinganisha na nchi za Afrika Mashariki zikiwemo Kenya, Uganda,Rwanda na Burundi.

 Waswahili walisema Roma haikujengwa kwa siku moja,tukiamua kujenga nchi yetu tunaweza lakini watanzania tunabomoa nchi yetu kutokana na mambo mbalimbali yaliokithiri ikiwemo rushwa,ufisadi,ukosefu wa viongozi bora na wenye uzalendo na ukosefu wa uwajibikaji na uaminifu.



No comments:

Post a Comment