![]() |
| Inayoonekana kwa mbali ni hospitali alikokuwa amelazwa mandela |
Na Mwandishi wetu
Serikali ya Afrika
Kusini imethibitisha kuwa Rais wa zamani, Nelson Mandela ametolewa hospitali
ambako amekuwa akitibiwa matatizo ya mapafu tangu Juni mwaka huu.
Hata hivyo, taarifa iliyotolewa katika tovuti ya
Rais wa Afrika Kusini imeeleza kuwa Mandela bado ni mahututi na hali yake
wakati mwingine inabadilika.
Uthibitisho huo umetolewa siku moja baada ya
maofisa wa Serikali ya nchi hiyo kukanusha taarifa kwamba Mandela (95)
amerudishwa nyumbani kwake, Johannesburg juzi.
Taarifa zilieleza kwamba madaktari wake wanaamini
akiwa nyumbani kwake atapata matibabu sawa na yale ya hospitali... “Wameweka
sawa mazingira yake huko Houghton ili aweze kupata matibabu aliyokuwa akiyapata
hospitali.”
Juzi Serikali ya Afrika Kusini ilikanusha habari
za baadhi ya vyombo vya habari zilizosema kwamba Mandela ameondolewa hospitali.
Msemaji wa Rais wa Afrika Kusini, Mac Maharaj alisema, Mandela bado yuko
hospitali anaendelea vizuri lakini hali yake bado ni mbaya.
Kauli hiyo imekuwa ikitumiwa na Serikali ya
Afrika Kusini kuelezea hali yake Mandela tangu alipolazwa hospitali mwanzoni
mwa Juni kutokana na ugonjwa wa mapafu.
Jumamosi iliyopita, Maharaj alisema mara kwa mara
afya ya Mandela imekuwa ikizorota, lakini alifaulu kukabiliana na ugonjwa
wake. Taarifa zaidi zilieleza kwamba Mandela ambaye ni mshindi wa Tuzo ya
Amani ya Nobel, alisafirishwa kutoka Hospitali ya MediClinic, Pretoria na
kupelekwa nyumbani kwake Johannesburg.
Tangu alipolazwa, watu wamekuwa wakiendelea
kumwombea na kuacha ujumbe wa kumtakia heri nje ya nyumba yake.
Ilielezwa kwamba matatizo ya mapafu
yanayomwandama yalitokana na kuugua kifua kikuu alipokuwa jela akitumikia
kifungo cha miaka 27.
Tangu kuanza kwa mwaka huu, Mandela amelazwa mara
nne lakini safari hii amekaa hospitali kwa muda mrefu zaidi.
CHANZO GAZETI LA MWANANCHI

No comments:
Post a Comment