ASASI za kiraia
kutoka katika wilaya zote za mkoa wa Ruvuma wameridhia mapendekezo ya Tume ya rasimu ya katiba ya Jamuhuri ya Muungano
iundwe shirikisho lenye serikali tatu.
Viongozi wa asasi
hizo zaidi ya 50 wamekubali mapendekezo ya Tume ya rasimu ya katibu katika mkutano wa jukwaa la kujadili Rasimu
ya katiba mpya ya Jamuhuri ya muungano wa Tanzania ulioandaliwa na mtandao wa mazingira mkoa wa Ruvuma (RUNEA)
kwa ufadhili wa shirika la The Foundation For Civil Society.
Wakizungumza kwenye mkutano huo wa siku tatu
katika ukumbi wa Songea Klabu,viongozi hao wamesema serikali ijayo ni muhimu
kuundwa na shirikisho la serikali tatu ambazo ni serikali ya Jamuhuri ya
Muungano,serikali ya mapinduzi ya Zanzibar na serikali ya Tanganyika.
Akichangia mjadala
huo Nathaniel Luoga ambaye ni kiongozi wa asasi ya Mwangaza Foundation alisema
kuundwa kwa serikali tatu kutaimarisha muungano na kuwezesha sasa serikali ya
Tanganyika kuwa na Rais wake kama ilivyo kwa serikali ya mapinduzi ya Zanzibar.
Kuhusu uendeshaji wa
serikali tatu Luoga alipendekeza serikali ya Jamhuri ya muungano inapaswa
kuchangiwa na serikali mbili za mapinduzi Zanzibar na Tanganyika ili kuendesha
shughuli zake za muungano hatimaye iweze
kutekeleza kazi zake kuanzia mwaka 2015.
Vitalis Nkomera mwanamazingira kutoka manispaa ya Songea
akichangia kuhusu muundo wa serikali tatu ameseme wanaridhia uwepo wa serikali
tatu na kusisitiza kuwa serikali ya Jamuhuri ya muungano itakuwa ndiyo
mlezi mkuu wa serikali mbili za Zanzibar na Tanganyika .
‘‘Kazi kubwa ya
serikali ya Jamuhuri ya Muungano iwe ni kusimamia na kuwa mwangalizi wa kulinda mambo yote muhimu yanayohusiana na
muungano,napendekeza kuwa serikali mbili za Zanzibar na Tanganyika ndiyo
zijihusishe na ukusanyaji wa mapato yanayotokana na ushuru na tozo
mbalimbali,serikali ya Jamuhuri ya muungano isihusike na kutoza ushuru wala
ukusanyaji mapato yenyewe itapewa gawio tu toka serikali mbili’’,alisema.
Nkomera alipendekeza
serikali ya Jamhuri ya muungano kuendeshwa kama ilivyo jumuiya ya Afrika ya
mashariki ambayo inaundwa na nchi zenye
serikali kamili ambazo zimekuwa zinaichangia jumuiya hiyo bila kujali kama nchi
hiyo ni kubwa au ndogo na kwamba muungano
ndiyo unatakiwa kuchangiwa na wote bila kujali uwezo wa serikali husika.
Regnad Mapunda akitoa
mapendekezo yake kuhusu serikali tatu ameshauri serikali ya Jamhuri ya muungano
wa Tanzania kuruhusiwa kutafuta vyanzo vyake vingine vya mapato bila kuingilia
vyanzo vya serikali mbili zinazounda serikali ya muungano .
Mapunda pia ameshauri
sehemu ya kwanza ibara ya pili katika rasimu ya katiba eneo la Jamhuri ya
muungano,liondolewe eneo lote la Tanzania bara badala yake liandikwe eneo lote
la Tanganyika na kuongeza kuwa rasimali zote ikiwemo bahari, maziwa, mito, milima
na raslimali nyingine zilizopo zitajwe bayana katika serikali zote.
Viongozi hao wa asasi
za kiraia wametaja baadhi ya faida za serikali tatu kuwa ni pamoja na kila
serikali kuwa na Rais wake,katiba yake,Bunge lake na kwamba kila serikali
itasimamia uchumi katika serikali yake pia serikali ya jamhuri ya muungano
ambayo itasimamia mambo yote ya muungano.
Wamesema serikali
tatu itawezesha kuwepo uhuru katika maamuzi katika kila serikali,migogoro ya
ukusanyaji wa mapato haitakuwepo,kila serikali itakuwa na mamlaka yake
kiutendaji, hata hivyo wamependekeza kuwepo na jeshi moja tu la wananchi wa
Jamhuri ya muungano wa Tanzania na polisi na pasiwepo na jeshi kwa kila
serikali.
Judith Erasto
ameshauri katika rasmu ya katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, jeshi la
mgambo kuingizwa katika katiba na kutambuliwa rasmi kuwa ni miongoni mwa
majeshi muhimu kwa kuwa serikali kila mwaka inatoa mafunzo ya askari mgambo na
mara baada ya kuhitimu wanaachwa hawafahamiki wanafanya nini.
‘‘Mgambo ni jeshi la
akiba ambalo linapewa mafunzo ya kijeshi na wanajeshi wenyewe,katika rasimu ya
katiba hakuna kipengele kinacholitambua jeshi la mgambo,unapowazalisha askari
mgambo wengi kila mwaka bila kuwapa ajira,wale mgambo wanaweza kujiingiza hata
katika vitendo vya uharifu,naomba katiba mpya ilitambue rasmi jeshi la mgambo
baada ya mafunzo waweze kuajiriwa’’,alisisitiza.
Vinsent Kapinga
kutoka Mbinga akichangia kuhusu serikali tatu amesisitiza kuwa kasoro za muungano zinazojitokeza hivi sasa
katika serikali mbili zitamalizika au kupungua sana mara baada ya kuwepo na
serikali tatu kikatiba.
Amesema hakuna haja
ya kuhofia gharama za uendeshaji kwa kuwa nchi ina rasilimali nyingi za kutosha
ambazo zinaweza kusaidia katika uendeshaji wa serikali tatu ili mradi
wapatikane viongozi wazalendo na wanaoweza kusimamia kikamilifu rasilimali za
Taifa.
Pius Kayombo kutoka
kikundi cha wenye ulemavu Peramiho anasema rasimu ya katiba ya Jamhuri ya
muungano inakidhi malengo ya kuwa na serikali tatu isipokuwa amependekeza marekebisho
yafanyike polepole na kwa uhakika kutokana na ukweli kuwa katiba ni kitu kigeni
ambacho hakifahamiki na watanzania wengi.
‘‘Katiba ni kitu cha
kudumu ikishaandikwa inaweza kutumika kwa miaka 50 hadi 100 ijayo, hivyo makosa
yakifanyika leo yatawaumiza watanzania kwa miaka mingi,mchakato wa rasmu ya
marekebisho ya katiba ya Jamhuri ya muungano naona unafanyika kwa haraka sana
tunakimbilia wapi,watu wangepewa muda wa kutosha kuisoma na kuifanyia
marekebisho kabla ya kuandikwa’’,alidai Kayombo.
Mchungaji Faustine
Luoga amependekeza kuwa katika rasimu hiyo iwekwe wazi mambo yote ya maliasili
za Taifa kama vile misitu,madini,maziwa na mengineyo kwa kuwa mazingira ndiyo
maisha badala ya kuwekwa kwa ujumla kama ilivyo katika rasimu ya katiba hivi sasa.
Awali mwenyekiti wa mtandao wamazingira mkoa wa
Ruvuma (RUNEA) ambao ndiyo waandaaji wa mkutano huo Method Ngerangera aliyataja
malengo ya kuendesha mabaraza ya katiba yanayoundwa na asasi za kiraia kuwa ni
kutokana na umuhimu wa watanzania kuwa na katiba mpya ili washiriki wajadili na
kutoa maoni yao juu ya vipengere vilivyopo kama vinakidhi au vifanyiwe
marekebisho ili viingizwe kwenye katiba mpya ijayo.
‘‘Uendeshaji wa
Baraza la rasmu ya katiba unaangalia na
kutoa haki sawa kwa wote katika kutoa mawazo au maoni ya kila mshiriki kwa kuwa
lengo la Baraza hili ni kuwa hakuna mwalimu au mwanafunzi wa kutoa maelekezo
yatakayotumiwa na mtu au kikundi Fulani kwa kutaka kuyakubali au kukataa maoni
kwa lengo la kuwakilisha mtu,kikundi,taasisi,dini,kabila au chama Fulani
kisiasa bali maoni hayo yawe na sura ya umoja’’,alisisitiza.
Naye mstahiki meya wa
manispaa ya Songea Charles Mhagama akizungumza wakati anafungua mkutano huo
aliwatahadharisha washiriki wote kuacha tofauti zao zote kuhakikisha kuwa mapendekezo yote
yatakayotolewa kwenye rasimu ya katiba
yawe kwa ajili ya Taifa letu la Tanzania.
Sura ya kwanza katika
rasimu ya katiba ya Jamhuri ya muungano wa Tanzania sehemu ya kwanza,ibara ya
kwanza kifungu cha kwanza kinaonyesha
Jamhuri ya muungano wa Tanzania ni shirikisho lenye mamlaka kamili ambayo
imetokana na muungano wan chi mbili za Tanganyika na Zanzibar ambazo kabla ya
hati ya makubaliano ya muungano ya mwaka 1964 zilikuwa nchi huru.
albano.midelo@gmail.com

No comments:
Post a Comment