Tuesday, September 10, 2013

Wazee wapendekeza pensheni asilimia 75



Viongozi wa mtandao wa RUNEA wakiteta jambo

 Na Albano Midelo

ASASI za kiraia mkoani Ruvuma  zimependekeza  eneo la wazee katika rasimu ya katiba ya jamhuri ya muungano wa Tanzania  liwe wazi kwa kuhakikisha kuwa wazee wote nchini wanalipwa pensheni itakayowawezesha kuishi.

Wawakilishi zaidi ya 50 kutoka katika wilaya zote za mkoa wa Ruvuma wametoa mapendekezo  hayo kwenye mkutano wa jukwaa la kujadili rasimu ya katiba mpya ya Jamuhuri ya muungano wa Tanzania ulioandaliwa  na mtandao wa mazingira mkoa wa Ruvuma (RUNEA) kwa ufadhili wa shirika la The Foundation For Civil Society .


Aidan Challe amependekeza rasimu ya katiba iweke wazi katika  katiba kifungu ambacho kinasema bayana kuwa wazee watalipwa pensheni ya asilimia 75 ya mshahara wa kima cha chini serikalini  na kufutwa kifungu ambacho kimewekwa katika rasmu ya katiba kinachosema msaada kwa wazee huku kifungu kikiwa hakionyeshi wazi wazee watapata msaada toka kwa nani na kiasi gani.

Challe alisisitiza kuwa kifungu cha wazee kulipwa pensheni kikiwa wazi katika katiba mpya itakuwa rahisi wazee kwenda kudai endapo serikali itashindwa kulipwa na kwamba kufungu kilichowekwa kwenye rasmu ya katiba hivi sasa kimezungumzwa kwa ujumla bila kuanisha wazi wazee wanastahili haki zipi na nani anawajibika kwa wazee.

Grasias Kipara akichangia kifungu cha wazee katika rasmu alisema sera na sheria zilizopo zinawanyima haki wazee wa Tanzania ambapo katika rasmu mpya ya katiba ameshauri kila mzee wa Tanzania mwenye umri wa kuanzia miaka 60 bila kujali alikuwa ameajiriwa serikali au mkulima alipwe pensheni itakayomwezesha kumudu maisha hadi mwisho wa maisha yake hapa ulimwenguni.

‘‘Sera ya wazee imetaka wazi kuwa wazee wanatakiwa kupata matibabu bure,lakini wote ni mashahidi ni wazee wangapi wanapata matibabu bure,hakuna hata mmoja tunaomba katika rasimu hii mpya kifungu kiwekwe na kutamka bayana atakayehusika na haki zote za wazee ili atakayekiuka atambue kuwa anafanya makosa kikatiba’’,alisema Kipara.

Ally Jaibu amependekeza katika rasimu ya katiba mpya kiongezwe kifungu ambacho kitaonyesha wazi kuwa watu wote ambao wanawadharau wazee waweze kuadhibiwa kisheria tofauti na hivi sasa wazee katika jamii wanaonekana ni balaa.

Jaibu pia amependekeza katika rasimu ya katiba wazee wawe washauri wakuu katika taasisi mbalimbali za umma na binafsi na kwamba kwa kazi hiyo serikali iweke bayana posho ambazo watalipwa wazee hao.

Judith Erasto amesema katika kipengere cha haki za binadamu wazee wameonekana wanakosa hali zao za msingi,licha ya kwamba rasimu ya katiba ya jamhuri ya muungano ibara ya 47 kutamka wazi kuhusu haki za wazee zikiwemo kushiriki katika shughuli za kijamii,kuendeleza maisha yao,kutambuliwa utu wao,kulelewa na kupata misaada kutoka katika familia zao,jamii na mamlaka ya nchi.

Alisema wazee wa Tanzania wanaishi katika mazingira magumu kutokana na serikali kuziweka haki zao kisiasa zaidi kwa kuwa hakuna mtu anayewajibika moja kwa moja kwa wazee ndiyo maana hata wakiugua licha ya kwamba serikali kupitia sera ya wazee ilisema watapatiwa matibabu bure lakini katika hali halisi wazee wa Tanzania hawatibiwi bure.

‘‘Napendekeza katika rasimu hii ihakikishe kwa kutaja bayana haki zote wanazotakiwa kupata wazee na mtu anayewajibika kuhakikisha haki hizo wanazipata,pia hatua za kuchukuliwa kwa yeyote ambaye atashindwa kutimiza wajibu wake katika haki za wazee kikatiba’’,alisisitiza.

Vinsent Kapinga kuhusu haki za wazee kwenye rasimu ya katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ameshauri  katiba mpya kujenga mfumo sawa kwa wazee wote kuhakikisha wanapata haki zote za msingi kama ilivyo kwa wazee wa nchi za Afrika ya kusini ambayo imeamua kila mwezi wazee kuwalipa pensheni ili waweze kuendelea kuishi.

‘‘Katika katiba mpya serikali lazima iweke kifungu ambacho kinasema imekusudia kuwatunza wazee kwa kiwango Fulani cha pensheni ,wazee wa Tanzania wanahangaika na kugeuka ombaomba kila mtu Mungu akimpa maisha kuanzia miaka 60 anaweza kuwa mzee hivyo ni vema katiba ijayo itilie mkazo haki za wazee’’,alisema.

Amesisitiza kuwa katika katiba kuwe na kifungu ambacho kinatamka wazi kuwa wazee wenye umri wa kuanzia miaka 60 wana haki ya kupata matibabu bure  badala ya kusema wazee wasaidiwe huku mtu anayewajibika moja kwa moja wazee hao akiwa hafahamiki  na kuleta matatizo makubwa kwa wazee.

Kuhusu kipengere cha wazee kupata msaada katika familia zao kama kilivyowekwa kwenye rasimu ya katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Nathaniel Lugongo ameshauri kipengele hicho kuondolewa badala yake  ieleze kuwa mtoto ana haki ya kisheria kumtunza mzazi wake na sio msaada kutokana na ukweli kuwa mzazi ndiye aliyemlea,kumtunza na kumsomesha mtoto huyo.

Takwimu zinaonesha kuwa katika manispaa ya  Songea inakadiriwa kuwa na wazee  wenye umri wa miaka zaidi ya 60 kufikia zaidi ya 180,000, hapa nchini inakadiriwa wazee wa zaidi ya miaka 60 wapo zaidi ya  milioni 1.4 na ifikapo mwaka 2050 idadi ya wazee wa Tanzania inatarajia kufikia milioni 8.3 sawa na asilimia 10 ya watanzania wote.

Kulingana na taarifa za umoja wa Mataifa za mwaka 1999 zinaonyesha kuwa mwaka 1950 wazee wenye umri wa miaka zaidi ya 50 duniani walikuwa 200,mwaka 1975 idadi hiyo iliongezeka na kufikia wazee 350,mwaka 2005 idadi ya wazee duniani ilifikia milioni 625 na mwaka 2050  wazee wenye umri wa zaidi ya miaka 60 katika historia ya binadamu  inatarajia kuongezeka kuzidi idadi ya watoto na vijana wenye umri wa miaka 24.

Katika bara la Afrika pekee ifikapo mwaka 2050 idadi ya wazee inatarajia kuongezeka kutoka milioni 38 hadi kufikia milioni 212,ongezeko hilo la wazee ni changamoto kwa serikali ikiwemo serikali ya Tanzania  kuhakikisha kuwa katika rasimu mpya ijayo inawatendea haki wazee ambao asilimia 75 wanaishi vijijini katika maisha ya umaskini uliokithiri.

albano.midelo@gmail.com




No comments:

Post a Comment