Friday, September 27, 2013

Ardhi ikifa viumbehai vitafutika duniani


 Na Albano Midelo

TANGU mwaka 1961 hadi 1970 bonde la Songwe wilayani Chunya mkoani Mbeya  lilikuwa ni ardhi oevu,yenye uoto wa kijani na msitu mnene wenye miti mbalimbali ya asili.
Shughuli za kibinadamu zinavyoharibu mazingira na kuuwa ardhi
 Wakati huo  wakulima waliweza kuzalisha mazao ya chakula kwa wingi kutokana na bonde kuwa na ardhi oevu yenye maji yaliokuwa yanatiririka kutoka mto Songwe ambao unaanzia milima ya Umalila Mbeya na kumwaga maji yake ziwa Rukwa  .
Bonde la Songwe ambalo linaundwa na kata za Totowe, Galula,Namkukwe,Kanga na Mbuyuni wakati huo lilikuwa linavutia maisha ya viumbehai wakiwemo binadamu, wanyamapori na  ndege wa aina mbalimbali.
Katika bonde la Songwe wakulima  waliweza kulima mazao mbalimbali yakiwemo mahindi, alizeti, ufuta, mtama,viazi vitamu na mpunga.

Mtu ambaye alifika kwenye bonde la Songwe miaka ya 1970 akitembelea leo kwenye bonde hilo hawezi kuamini kwa kile ambacho atakiona kutokana na mabadiliko makubwa ya  kimazingira ambayo yamejitokeza,hivi sasa  bonde hilo linakabiliwa na njaa kila mwaka kutokana na ukame unaotokana na bonde kukosa mvua za uhakika.

  Siku za nyuma hayati Baba wa Taifa mwl.Julius Nyerere alitahadharisha kuwa ardhi ndiyo msingi wa uhai wetu,ardhi ikiwa na afya tutakuwa na afya,ardhi ikiugua tutaugua na ardhi ikifa viumbe wote tunafutika  katika uso wa dunia.
Maneno hayo ya Baba wa Taifa yameanza kutimia katika maeneo mbalimbali nchini likiwemo  bonde la Songwe ambapo hivi sasa katika bonde hilo miti imetoweka,ardhi imebaki uchi,miti karibu yote iliyokuwa kivutio katika bonde la Songwe haipo tena,bonde  limejaa makorongo makubwa ambayo yanatokana na mmomonyoko wa ardhi,vumbi zito na  vimbunga vya mara kwa mara limekuwa ni jambo la kawaida katika bonde hili.
Ufyekaji ovyo misitu unamaliza miti na kuharibu mazingira
Unapofika kwenye bonde hili kuanzia mwezi wa Aprili hadi Novemba utaona upepo wenye vumbi zito ambao unaweza kudhani mvua inataka kunyesha,vumbi hilo huwa zito kiasi kwamba huwezi kumuona mtu aliye mbele yako.Hali hii inawafanya wakazi wa Bonde hilo kujifungia ndani ya nyumba zao kuepukana na vumbi hilo.
 Athari hizo za kimazingira zinachangiwa na   idadi kubwa ya mifugo ambayo inaendelea kuongezeka kwa kasi kubwa kwenye bonde la Songwe huku wafugaji hao wahamiaji kutoka kanda ya ziwa wakifanya uharibifu wa mazingira kwa kufyeka miti ovyo kwa lengo la kujipatia kuni,mkaa na mashamba.
 Afisa mifugo,kilimo na ushirika katika Halmashauri ya wilaya ya Chunya Adamu Mbale  anasema idadi ya ng,ombe katika bonde zima kati ya mwaka 1961 hadi 1970 ilikuwa ni 800 tu hali iliyosababisha mazingira katika bonde hilo kuwa ya kuvutia.
Kwa mujibu wa Mbale idadi ya ng’ombe kwenye bonde hilo iliongezeka kwa kasi na kuathiri mazingira  katika kipindi cha kuanzia mwaka 1981 hadi 1990 ng’ombe walifikia 173,681,mwaka 2000 ng’ombe walifikia 186,800 na hadi kufikia mwaka 2010 idadi ya ng’ombe ilifikia 286,800.
Mkuu wa wilaya ya Chunya Deodatus Kinawiro amekiri kuwa bonde la Songwe na wilaya ya Chunya kwa ujumla wake inapita katika kipindi kigumu sana cha uharibifu wa mazingira ambacho hakijawahi kushuhudiwa tangu kuanzishwa kwa wilaya hiyo.
“Kimsingi hali ya uharibifu wa mazingira katika wilaya yetu ni mbaya sana na kama hatutachukua hatua za haraka  hali inaweza kuwa mbaya zaidi miaka michache ijayo,ni jukumu letu sisi viongozi wa serikali kushirikiana na viongozi kuanzia ngazi ya kitongoji,kijiji,kata na tarafa kuokoa hali hii inayotishia ustawi wa maisha ya watu endapo kutatokea jangwa kwa kuwa dalili zake hasa katika bonde la Songwe zimeanza kujitokeza’’,alisema.
Kinawiro alisema misitu mingi ya asili na  iliyotengwa kwa ajili ya hifadhi katika wilaya ya Chunya imevamiwa licha ya serikali kupiga marufuku kuendesha shughuli zote za kibinadamu kama vile kulima na kufuga na kwamba ndani ya misitu hiyo kuna wafugaji wengi ambao wanakata miti ovyo bila kuangalia athari za kimazingira.
“Kwa mtu ambaye unapenda mazingira ukifika katika misitu ya hifadhi ya wilaya ya Chunya unaweza kulia kwani misitu imebakia vibara vitupu,watu wamekata miti ya asili ambayo imekuwa kwa zaidi ya miaka 100,kibaya zaidi mara baada ya kuikata anaichoma moto inakuwa majivu na kuacha eneo hilo kuwa kama uwanja wa mpira tena ambao hauna nyasi’’,alisema.
Alisisitiza kuwa bila miti hakuna mvua ndiyo maana katika bonde la Songwe ambalo karibu miti yote imekatwa linakabiliwa na ukame ambao unasababisha njaa kila mwaka  hali inayoleta matatizo kwa serikali kila mwaka kupeleka chakula cha msaada kwa wakazi wa bonde hilo ambao eneo lao ni nusu jangwa.
Alisema mwezi Juni mwaka huu imefanyika operesheni maalum katika kata ya Totowe bonde la Songwe kuwaondoa watu waliovamia maeneo ya misitu ya hifadhi na kwamba wanatarajia kwenda katika maeneo mengine yaliokithiri ambayo aliyataja kuwa ni Gua,Ngwala na Kapalala ambako wanatarajia kwenda kuendesha operesheni hiyo  ili kuhakikisha kuwa misitu ya hifadhi inabakia kuwa endelevu.
Utafiti umebaini kuwa Kuna baadhi ya maeneo hapa nchini yakiwemo katika mikoa ya Dodoma,Arusha,Manyara,Shinyanga na Mbeya wameanza kuonja athari za mabadiliko ya tabianchi ambapo kuna wakati  fulani wa mwaka  kunatokea giza kubwa la upepo wa vumbi zito  mfano wa wingu la  mvua ambalo  linaendelea kuuwa ardhi .
 Wanasayansi wanatahadharisha kuwa Dunia hivi sasa inapita katika tatizo kubwa la kubadilika kwa misimu ya mvua,kuongezeka kwa joto,ukame,mafuriko,kuongezeka kwa baridi,kuyeyuka kwa barafu kwenye mlima Kilimanjaro pamoja na sehemu nyingine kutokana na uharibifu mkubwa wa mazingira.
Viumbehai wa kuvutia kama ndege,mimea na wanyama kuna dalili kwamba siku moja wanaweza kufutika katika uso wa dunia kutokana na uharibifu  mkubwa wa mazingira unaofanywa na binadamu ambao hivi sasa unatishia mabadiliko ya tabia nchi.
Waziri wa mazingira Dk.Teresia Huvisa akitoa maagizo kukabiliana na Mazingira
Waziri wa nchi ofisi ya makamu wa Rais mazingira Dk.Teresia Huvisa hivi karibuni amewaasa watanzania wote kushiriki kikamilifu katika utunzaji wa mazingira ili kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi yaliosababishwa na hewa ukaa angani na kusisitiza kuwa uharibifu wa mazingira ni janga la duniani ambalo linaviweka viumbehai njia panda.

“Mimi kama Rais wa mazingira Afrika ambaye nilichaguliwa mwaka jana na mawaziri wote wa mazingira barani Afrika nina wajibu wa kutoa tahadhari sio tu kwa watanzania bali Afrika nzima na ulimwengu kote kwa ujumla,  dunia inaweza kuangamia kama sisi sote hatutafanya juhudi za makusudi kupambana na mabadiliko ya tabianchi’’,alisisitiza.
Kulingana na waziri huyo,tangu kuumbwa kwa dunia shughuli mbalimbali za kibinadamu zimesababisha dunia kuharibika na kuongezeka kwa joto kwa kwa asilimia 0.7 na kusababisha madhara yote yanayotokea sasa duniani yakiwemo ukame,mafuriko na mabadiliko ya tabianchi kwa ujumla.
Hata hivyo wanasayansi wanatahadharisha kuwa iwapo joto  duniani litaongezeka  hadi kufikia asilimia 1.5 ambalo ni ongezeko la asilimia 0.8  viumbehai  wote waliopo duniani hawataweza kumudu  kuishi.
“Mwaka juzi tulipokuwa nchini Afrika ya kusini  ongezeko la joto duniani lilikuwa 0.7,katika mkutano wa kidunia wa mawaziri wa mazingira ambao tuliufanya mwaka jana jijini Doha nchini Quatar kiwango cha joto kilifikia 0.8, mwaka huu tunafanya mkutano mwingine nchini Poland hatujui joto litafikia kiwango gani linawezekana kufikia 0.9,kupambana na hali hii inatakiwa kupanda miti ya kutosha na sio vinginevyo’’,alisisitiza waziri Dk.Huvisa.
Kwa mujibu wa sera ya Taifa ya misitu ya mwaka 1998, Tanzania ina karibu hekta milioni 33.5 za misitu ambapo theluthi mbili ya hekta hizo  ipo mashakani kutokana na ukosefu wa usimamizi mzuri hali inayosababisha watu kuvamia na kuharibu misitu kwa ajili ya kilimo,malisho ya mifugo,moto,uchimbaji madini,ujenzi na shughuli nyingine.
Licha ya kwamba hakuna takwimu za kuaminika kuhusu kasi ya kutoweka kwa misitu,inakadiriwa kuwa hapa nchini ni kati ya hekta 130,000 hadi 500,000 za misitu zinafyekwa kila mwaka hali inayokatisha tamaa jitihada za kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi ambayo yanahitaji miti ili kupunguza hewa ukaa .
Mwanadamu ndiyo mtaji mkubwa katika mapambano dhidi ya uharibifu wa mazingira hivyo wananchi watambua kuwa mabadiliko ya tabia ya nchi yameanza kutuathiri inatakiwa kupanda miti kila mwaka na kuitunza ili kupunguza matatizo haya yanayoiweka dunia njia panda.
albano.midelo@gmail.com


No comments:

Post a Comment