Wednesday, September 25, 2013

Hifadhi ya Serengeti Eden ya Afrika


Ina nyumbu milioni moja na nusu
Nyumbu katika hifadhi ya Taifa Serengeti
 Na Albano Midelo

HIFADHI ya Taifa ya Serengeti inayopita katika mikoa ya Arusha,Mwanza,Mara na Shinyanga ni eneo pekee duniani lenye kundi kubwa la wanyama wanaohama katika mfumo mzima wa mlishano.
Inasemekena neno Serengeti linatokana na neno la kimasai la sirenget lenye maana ya  uwanda mpana wa nyasi fupi,malisho mengi na maji ya kutosha pengine ndiyo maana hifadhi hiyo inapewa majina mengi kama vile lulu,bustani ya Afrika na Edeni ya Afrika kutokana na utajiri wa maliasili uliopo ndani ya hifadhi hii.hifadhi ya Taifa ya Serengeti yenye ukubwa wa  kilometa za mraba 14,763 ilianzishwa mwaka 1951, ni Hifadhi ya Taifa ya pili kwa ukubwa nchini ikitanguliwa na hifadhi ya Taifa ya Ruaha yenye ukubwa wa kilometa za mraba 20,226.
Umaarufu wa hifadhi ya Taifa ya Serengeti  unatokana na kuwa na misururu mirefu ya nyumbu wanaohama kwa makundi  na kuvuka hata mpaka wa Tanzania hadi hifadhi ya wanyama pori ya Maasai Mara nchini Kenya ambapo takwimu za TANAPA zinaonyesha kuwa kila mwaka zaidi ya nyumbu milioni moja,pundamilia 200,000, swala tomi zaidi ya 300,000 na pofu 12,000 huunga misafara ya kutafuta malisho na maji.

Mhifadhi John Makunga anasema Kila mwaka katikati ya mwezi Julai tukio lisilokuwa na kawaida na lenye mvuto wa kipekee hutokea katika hifadhi ya Taifa ya Serengeti kwa kundi kubwa la nyumbu wakikimbia  kutoka upande wa kusini mwa hifadhi hiyo na inapofika mwezi Mei wanyama hao huanza kukumbwa na ukame hivyo kuondoka kuelekea kaskazini mwa hifadhi kwa kufuata malisho mazuri.
“Hifadhi ya Taifa ya Serengeti huchukuliwa kama moja ya maajabu ya dunia kutokana na tendo la uhamaji wa nyumbu kutoka kusini hadi kaskazini na kurudi, tendo ambalo linafanyika mara moja tu kwa mwaka tendo hilo linaifanya hifadhi hii kuwa Eden ya Afrika na kupendwa kutembelewa na watu wengi ulimwenguni kote’’,alisema.
Licha ya nyumbu wanyama wengine maarufu walao nyama katika hifadhi ya Taifa ya Serengeti ni chui na simba ambapo utafiti umebaini kuwa ukubwa wa hifadhi hii umesaidia kudumisha uhai wa wanyama waliokuwa katika hatari ya kutoweka kama vile faru weusi na duma.
Nyumbu wa hifadhi ya Taifa ya Serengeti wakelekea Kenya
Wanasayansi  wanaeleza kuwa wanyama aina nyumbu ambao ni wengi katika hifadhi ya Taifa ya Serengeti wameumbwa na vijinasaba ambavyo huwafanya wahame katika mfumo mzima wa mlishano wa Serengeti kwa kufuata nyasi fupi za Seronera kwenda kusini katika ukanda wa miti michache na nyasi ndani ya hifadhi ya Serengeti maeneo ambayo ndiyo mazalio ya nyumbu.
Mhifadhi Daniel Gumbo anasema maeneo hayo yana asili ya udongo wa volkano uliotokana na  milipuko iliyotokea katika mlima mkubwa wa Ngorongoro miaka mingi iliyopita na kwamba asili ya udongo huo huwezesha wanyama aina ya nyumbu kutoa maziwa kwa wingi kwa ajili ya kunyonyesha ndama wa nyumbu na kuwawezesha kukua kwa muda mfupi.
Mhifadhi huyo anabainisha kuwa mara baada ya nyumbu kuzaliana,katika maeneo ya tambarare ya Seronera huanza safari kuelekea hifadhi ya Taifa ya Serengeti upande wa magharibi na kuvuka mpaka kuingia hifadhi ya Maasai Mara nchini Kenya na baada ya muda mfupi wanarudi Tanzania kupitia Loliondo pamoja na Ngorongoro na kukamilisha mzunguko mzima.
Tafiti zinaonyesha kuwa  katika hifadhi ya Taifa ya Serengeti kuna idadi ya nyumbu inayokadiriwa kuwa milioni moja na nusu ambao hutembea eneo la kilometa za mraba 40,000 katika mfumo mzima wa mlishano wa Serengeti  ambapo nyumbu na wafuasi wao wakiwemo pundamilia,swalatomi na pofu hukumbwa na vifo kutokana na kuchoka njiani kwa sababu ya safari ndefu,umri mkubwa na magonjwa.
Kutokana na sababu hizo wanyama ambao ni maadui wakubwa wa nyumbu ambao ni simba,fisi na mbweha wanakuwa washiriki katika msafara huo wa nyumbu wanaohama katika mfumo wa mlishano  hivyo kufaidi mizoga ya wanyama hao au kuwawinda wanyama wagonjwa na waliochoka.
Watafiti wa wanyama hao wanautaja muda mzuri ambao wanyama hao wanasafiri ni usiku kutokana na muda huo kuwa na hali ya hewa isiyokuwa na joto ambayo huwawezesha kukimbia kwa muda mrefu na kwamba wanyama hao mara nyingi hukimbia katika mstari mmoja na wanapofika kwenye malisho au mapumziko wanatawanyika.
Wanasayansi waliowafanyia tafiti nyumbu wanadai kuwa inapotokea nyumbu wanazaa wakati mvua zinanyesha huweza kuchelewa  tendo la kuzaa kwa wiki mbili hadi tatu na mvua zinapowahi nyumbu huweza kuzaa mapema wiki mbili au tatu kabla ya muda wake .
Kwa mujibu wa wataalamu hao wa wanyama, baada ya kuzaliwa ndama wa nyumbu huweza kusimama na kukimbia na mama yake baada ya dakika chache na kwamba baada ya siku moja tu ndama wa nyumbu huweza kukimbia na kundi zima la nyumbu na baada ya siku kumi huweza kula nyasi huku akiendelea kunyonya kwa miezi sita lakini anaendelea kubaki na mama yake hadi ndama mwingine atakapozaliwa.
Watalii wanaotembelea Hifadhi ya Taifa ya Serengeti  kutokana na makundi makubwa ya nyumbu wameifanya hifadhi hiyo kuwa maarufu Afrika mashariki na ulimwenguni kote hali iliyosababisha shirika la Umoja wa Mataifa la Elimu na Sayansi UNESCO  kuitangaza Serengeti kuwa  eneo la urithi wa Dunia  kwa kuwa ndiyo eneo pekee ulimwenguni lililosalia kundi kubwa la wanyama wahamao.
Nyumbu wa hifadhi ya Taifa Serengeti
Historia inaonyesha kuwa miaka mingi iliyopita kulikuwa na kundi kubwa la wanyamapori waliokuwa wakihama toka Amerika ya kusini hadi Amerika ya kaskazini kupitia safu za milima ya Andes na majangwa ya Atakama na kalifonia ambapo maendeleo ya sayansi na ongezeko la idadi ya watu zilisababisha makundi ya wanyama huko Amerika kutoweka na sasa kubakia hifadhi ya Serengeti pekee duniani.
Hifadhi ya Taifa ya Serengeti inatambulika kama Edeni ya Afrika kwa kuwa ni moja ya maajabu ya dunia hivyo kuvutia hisia za watu wengi kupenda kutembelea hifadhi hii ambapo tafiti mbalimbali za kisanyasi kuhusiana na hifadhi hii zimefanyika na makala nyingi za kisayansi zimeandikwa.
Mwanasayansi  kutoka nchini Ujerumani anayefahamika kwa jina la Gyzmeck Gyzmeck alifanya utafiti wa kisayansi katika hifadhi ya  Taifa ya Serengeti kisha kuandika kitabu kilichoitwa ‘‘Serengeti shall never die” ikiwa na maana Serengeti haitakufa .
Hifadhi ya Taifa ya Serengeti ipo umbali wa kilometa 335 kutoka Arusha ikiambaa kaskazini katika mpaka na nchi ya Kenya,kwa upande wa magharibi inapakana na na ziwa Viktoria,hifadhi hii inafikika kwa kukodi ndege kutokea jijini Dar es salaam,Mwanza,Kilimanjaro na Arusha pia kwa barabara kutokea Arusha,Musoma na Mwanza,wakati mzuri wa kutembelea hifadhi hii ili kuona uhamaji wa nyumbu ni kuanzia mwezi Desemba hadi Julai.
Mkurugenzi wa Hifadhi za Taifa Tanzania TANAPA  Allan Kijazi anasema  utalii katika hifadhi 16 za Taifa ni moja ya vyanzo vikuu vya fedha za kigeni katika Taifa na kwamba juhudi za kuzitangaza hifadhi kimataifa zimesababisha idadi ya watalii kutoka nje ya nchi kuendelea kuongezeka na kwamba TANAPA inafanya juhudi za kuwawezesha watanzania kufanya utalii wa ndani badala ya kutegemea wageni .
Takwimu zinaonyesha kuwa TANAPA imeingiza mapato ya zaidi ya sh. bilioni 549.8  hadi kufikia kipindi cha mwaka wa fedha wa 2011/2012 ikiwa ni mapato yaliyotokana na watalii waliotembelea Hifadhi za Taifa zilizoko chini ya shirika hilo na kwamba katika kipindi hicho jumla ya watalii milioni 5.730,181 walitembelea hifadhi hizo za Taifa.
Balozi Khamis Kagasheki ni waziri wa maliasili na utalii, anasema sekta ya utalii hapa nchini ni ya pili kwa ukubwa katika kuchangia pato la Taifa ambayo inachangia asilimia 17  na kwamba Kutokana na mapato makubwa ya sekta ya utalii waziri Kagasheki anasisitiza kuwa Serikali imekusudia kuongeza mchango wa utalii katika pato la Taifa.
 Mkakati mmoja wapo unaotumika kuboresha sekta ya utalii kama ulivyoainishwa katika Sera ya Utalii ya mwaka 1999  ni kupanua wigo wa utaliii ikiwa ni pamoja na kufungua maeneo mapya ya utalii na kuendeleza mazao mapya ya utalii hivyo kuongeza muda wa mtalii kukaa nchini na kufanya matumizi zaidi hatimaye Taifa kupata mapato zaidi.
Sekta ya utalii ni muhimu sio kwa Tanzania pekee bali  pia duniani kote kutokana na takwimu za kimataifa kuonyesha kuwa Mapato yatokanayo na utalii duniani yalifikia dola za Marekani milioni 919 mwaka 2010 ukilinganisha na  mwaka 2009  ambapo mapato hayo yalikuwa dola za Marekani  milioni 851 sawa na ongezeko la asilimia 4.7
albano.midelo@gmail.com,simu 0766463129

No comments:

Post a Comment