![]() |
| B aadhi ya wanachuo wa shahada St.Joseph Songea |
Na Albano Midelo
VYUO vikuu vya kanisa
katoliki nchini vinapokea wanafunzi kutoka imani zote na hata wanafunzi
wasiokuwa na imani za dini lengo likiwa ni kujenga umoja wa Taifa na maelewano baina ya
watanzania.
Hayo yalisemwa na
askofu wa jimbo katoliki la Mbinga mhashamu John Ndimbo kwa niaba ya Askofu mkuu wa jimbo kuu la
Songea katika mahafali ya nne ya chuo kikuu cha mtakatifu Joseph kampasi ya
Songea yaliofanyika kwenye viwanja vya chuo hicho vilivyopo Ruhuwiko mjini
hapa.
Mhashamu Ndimbo kwa
namna ya pekee ameipongeza serikali kutokana na kutoa ushirikiano wa kutosha na
kutambua mchango wa madhehebu ya dini
katika huduma mbalimbali za kijamii ikiwemo elimu.
“Hatuna budi
kuishukuru serikali pale inapotoa sera na miongozo mizuri inayowezesha
mashirika ya dini kushiriki kuilea jamii hususani huduma za elimu,tunayofuraha
kuwepo kwa sera ya elimu ya kanisa
katoliki ya Tanzania ya mwaka 2005 na
2008 inayotaka vyuo vikuu vyote vya
kanisa kupokea wanafunzi kutoka imani zote na hata wale wasiokuwa na imani za
dini lengo ni kujenga maelewano baina na watanzania wote’’,alisisitiza.
Katika mahafali hayo
ambayo mgeni rasmi alikuwa waziri wa elimu na mafunzo ya ufundi Dk.Shukuru
Kawambwa jumla ya wanachuo 97 wametunukiwa vyeti vya kuhitimu stashahada na
shahada katika chuo kikuu cha teknolijia ya habari cha mtakatifu Joseph kampasi
ya Songea kinachomilikiwa na watawa wa katoliki wa Daughters Of Mary Immaculate
(DMI).
Akizungumza katika
mahafali ya nne ya chuo kikuu hicho,mkuu
wa chuo kikuu cha mtakatifu Joseph cha Tanzania padre Dk. Arul Raj alisema kati ya wahitimu
hao wanachuo 58 ni wenye shahada(degree) ya kompyuta ya sayansi na wanachuo 39 wenye stashahada (diploma) ya
sayansi ya kompyuta.
‘‘Leo tunapofanya
mahafali ya nne ni muda muafaka wa kumshukuru mwenyezi Mungu kwa kukiwezesha
chuo chetu kupata mafanikio makubwa kitaaluma kwa kuzalisha wataalamu wengi
katika fani ya teknolojia ya habari na uhandisi,pia kutokana na kupanua matawi
ya chuo chetu ambapo hivi sasa katika Tanzania kuna matawi matano katika mikoa
ya Ruvuma,Njombe,Dar es salaam na Arusha’’,alisema.
Ameyataja malengo ya
baadaye ya chuo kikuu hicho kuwa ni kufungua tawi katika mkoa wa Tanga, katika
kuhakikisha mpango huo unatekelezwa chuo kimetenga bajeti ya shilingi bilioni
moja na tayari kimenunua ekari saba katika jiji la Tanga.
Aliongeza kuwa hivi
sasa chuo kikuu cha mtakatifu Joseph cha Tanzania kina uwezo wa kuchukua
wanafunzi 1350 wanaosoma katika fani za uhandisi na teknolojia ya habari na
kwamba chuo hicho kutokana na kutoa elimu bora kimekuwa ni chagua la watanzania
wengi ambao wanafanikiwa kutimiza ndoto zao.
Kwa upande wake
makamu mkuu wa chuo kikuu cha mtakatifu Joseph Songea Sr.Julian Rani alisema
kuwa chuo hicho hivi sasa kinajulikana ndani na nje ya nchi kutokana na
kuzalisha wataalamu bora katika uandisi na teknolojia ya habari na kwamba
kutokana na kuungwa mkono na serikali baada ya muda mfupi chuo kikuu hicho
kitafahamika ulimwenguni na hivyo kuwa chuo kikuu cha kimataifa.
Alisema chuo kikuu
cha mtakatifu Joseph Songea kilianza mwaka 2004 kikiwa na wanachuo wachache
ambapo hivi sasa chuo hicho kina idadi kubwa ya wanachuo ambao ni 685 kati yao
wanaume ni 558 na wanawake 127 ambao wanasoma stashahada na shahada katika
Sayansi ya kompyuta.
Hata hivyo alisema
kuanzia mwaka wa masomo uliopita chuo kimeanza kutoa masomo ya shahada ya Sayansi ya elimu ambapo
tayari kuna wanachuo 205 wanaosoma kozi hiyo na kwamba katika chuo hicho kampasi
ya Songea tangu mwaka 2010 kinatoa
masomo ya shahada ya kilimo ambapo tayari
kuna wanachuo 173 kati yao wanaume ni 119 na wanawake 54.
Dk.Txa Ananth ambaye
ni Rais wa baraza la vyuo vikuu vya mtakatifu Joseph Afrika vinavyomilikiwa na
watawa wa DMI akitoa ripoti ya vyuo
hivyo kwenye mahafali hayo alisema jamii ya watawa wa DMI ilianzishwa nchini
India mwaka 1984 kwa lengo la kuhudumia masikini ambapo hivi sasa DMI
inahudumia wanawake zaidi ya
500,000,wanafunzi wahandisi 21,000 na watoto 35,000.
“Chuo kikuu cha
mtakatifu Joseph kinamilikiwa na kanisa katoliki chini ya watawa wa DMI
kinafanya kazi zake zote kwa kumtanguliza mwenyezi Mungu mbele, hata hivyo
tunatoa huduma kwa watu wote bila ubaguzi wa dini,kabila wala
rangi’’,alisisitiza.
Kwa mujibu wa Rais
huyo wa watawa wa DMI Afrika,shirika hilo limeenea katika nchi sita za Afrika
ambazo alizitaja kuwa ni Tanzania,Zambia,Malawi,Ethiopia,Sieraleone,Sudan
kusini na nchi ya Brazil katika Amerika ya kusini ambapo hapa Tanzania DMI
ilianza rasmi mwaka 2003.
Katika hatua nyingine
serikali mkoani Ruvuma imekubali ombi la kutoa
ekari zaidi ya 2000 kwa chuo
kikuu cha mtakatifu Joseph Songea ili kiweze kujipanua katika sekta ya
elimu,maombi hayo pia yameungwa mkono na waziri wa elimu Dk.Shukuru Kawambwa
ambaye ameahidi kushughulikia ombi hilo haraka iwezekavyo.
Akizungumza kwa niaba
ya mkuu wa mkoa wa Ruvuma,mkuu wa wilaya ya Songea Joseph Mkirikiti alisema
serikali imekubali ombi hilo itaanza mara moja mchakato wa kuhakikisha ekari
hizo zinapatikana ili kupanua uwezo wa chuo hicho ambacho tayari kina kampasi
mbili katika wilaya ya Songea.
Mgeni rasmi katika
mahafali hayo waziri wa elimu na mafunzo ya ufundi Dk.Shukuru Kawambwa
amelipongeza shirika la watawa wa DMI kwa kutoa taaluma bora ya elimu ya juu
katika fani za uhandisi na teknolojia ya habari,wataalamu ambao alisema ni
muhimu katika ulimwengu huu wa sayansi na teknolojia.
Hata hivyo alisema
serikali katika kipindi hiki cha miaka mitatu imejikita kuboresha elimu ili
kuleta mabadiliko makubwa sasa (Big Results Now) kuanzia elimu ya awali,msingi
na sekondari na kwamba hakuna muda wa kusubiri licha ya changamoto zilizopo.
Alisema matokeo
makubwa sasa yakifanikiwa katika elimu ya awali,msingi na sekondari utakuwa mwanzo wa matokeo makubwa katika
elimu ya juu kutokana na uhusiano uliopo kati ya elimu ya msingi,sekondari na
elimu ya juu.
Kuhusu serikali
kuanza kutoka mikopo kwa wanafunzi wanaosoma stashahada,waziri Dk.Kawambwa
amesema serikali itaangalia uwezekano wa kuanza kutoa mikopo kwa wanafunzi wa
stashada ingawa lisisitiza kuwa ni kazi nzito kwa kuwa hata mikopo inayotolewa
kwa wanafunzi wa shahada haitoshelezi kwa wote kutokana na idadi kubwa ya
wanafunzi wanaosoma elimu ya juu.
Hata hivyo alisema
serikali inajitahidi kila mwaka kuongeza kiwango cha mikopo kwa wanafunzi wa
elimu ya juu ambapo mwaka 2005 jumla ya shilingi bilioni 56 zilitengwa katika
bajeti kwa ajili ya mikopo na kwamba mwaka huu serikali imetenga shilingi
bilioni 326 kwa ajili ya mikopo ya elimu ya juu.
“Tangu serikali
imeanza kutoa mikopo kwa wanafunzi wa elimu ya juu zimetolewa jumla ya trilioni
moja na bilioni mia nne na hamsini,pesa
zilizorudishwa kutoka kwa wanachuo ni bilioni 35 tu,wengi waliochukua mikopo wameingia
mitini licha ya kupata kazi nzuri, natoa wito kwa wanachuo waliopata mikopo
waanze kuirejesha ili wengine waweze kukopeshwa’’,alisisitiza.
Alibainisha kuwa
idadi ya wanafunzi wa elimu ya juu inaongezeka kwa kasi kubwa ukilinganisha na
idadi ya wanafunzi 13 ndiyo waliojiunga na chuo kikuu cha Dar es salaam mwaka
1961 na kwamba idadi imekuwa inaongezeka ambapo takwimu za mwaka 2005
zinaonyesha kuwa wanafunzi waliojiunga na vyuo vikuu ilikuwa ni 42,000 na mwaka
huu idadi ya wanachuo katika vyuo vikuu na vyuo imefika 170,000.
albano.midelo@gmail.com,simu
0766463129

No comments:
Post a Comment