![]() |
| Zao la tumbaku |
Na Albano Midelo
UZALISHAJI wa tumbaku katika mikoa ambayo zao hilo linalimwa umekuwa
hauendi sanjari na ongezeko la upandaji miti kwa ajili ya kuchomea tumbaku hali
ambayo inachangia uharibifu mkubwa wa mazingira .
Ofisa kilimo wa wilaya ya Songea Kaswam Maswaga anasema hakuna juhudi za
makusudi zinazofanywa na wakulima za kupanda miti kwa ajili ya kupata nishati
ya kukaushia tumbaku hivyo ametoa wito kwa wakulima kuhakikisha juhudi za
kupanua mashamba mapya ya tumbaku zisilete athari za kukata miti kwa ajili ya kuchomea tumbaku.
Frank Komba ni mwanaharakati wa
mazingira katika wilaya ya Namtumbo anasema mashamba ya tumbaku yanasababisha
uharibifu mkubwa wa misitu katika wilaya
ya Namtumbo pamoja na mikoa mingine inayolima tumbaku kama Tabora kutokana na
zao hilo kuhitaji kuni nyingi kwa ajili ya kuchomea tumbaku.
“Ukataji holela wa misitu ili kuchomea
tumbaku umeleta athari kubwa ya mabadiliko ya tabia nchi katika kipindi cha
miongo michache mkoani Tabora, na sasa mkoa umekuwa na ukame pamoja na ukataji
miti unaofanyika mkoani Ruvuma bado mazingira yake ni nafuu tuchukue hatua’’,anasisitiza
Komba.
Hata hivyo Komba anadai kuwa jitihada
za kushawishi wakulima kuacha kulima tumbaku na kuanza kuzalisha mazao mbadala
zimekuwa ni ngumu kwa kuwa wakulima wanaamini zao hilo lina faida kubwa
ukilinganisha na mazao mengine ya biashara.
“Ukataji miti ovyo unaoendelea
kufanyika kila mwaka karibu wilaya nzima ya Namtumbo, umechangia sana uharibifu
wa vyanzo vya maji wilayani Namtumbo ,huku kiwango cha mvua kikiendelea
kupungua mwaka hadi mwaka’’,alisema John Nilahi mkazi wa Namtumbo.
Amosi Luambano ni mkulima mdogo wa tumbaku
katika kijiji cha Mbimbi wilayani Namtumbo mkoani Ruvuma amekuwa akilima
tumbaku tangu miaka ya 1980 ambapo Kwa miaka kadhaa amekuwa akishuhudia msitu
uliokuwa umezunguka katika kijiji chake ukitoweka huku ardhi ikibakia uchi kwa
kukosa miti.
Zao la tumbaku linateketeza maelfu ya
tani za kuni kila mwaka zinazotumika kwa ajili ya kukaushia tumbaku kwa mfano
inakadiriwa katika mkoa wa Tabora kila mwaka kuni zinazotumika ni zaidi ya meta
za ujazo 124,389 za miti hukatwa.
Utafiti uliofanywa kwa kuwahoji baadhi
ya wanavijiji wilayani Namtumbo mkoani Ruvuma, unaonyesha
kwamba wakulima wengi hawajui madhara ya zao la tumbaku katika mazingira licha
ya kwamba athari zinazotokana na ukataji miti ovyo kwa ajili ya kukaushia
tumbaku zimeanza kujitokeza katika vijiji vingi.
Hata hivyo utafiti uliochapishwa na Chuo kikuu cha Kilimo
Sokoine ambao ulifanyika mkoani Tabora Machi 2012, unaonyesha kuwa Tanzania
inapoteza zaidi ya ekari 61,000 za misitu kila mwaka kutokana na zao la tumbaku
hali ambayo inaliweka zao hilo mashakani kwa kuwa linaweza kuleta jangwa.
Utafiti huo unasema zao la tumbaku
lina mahitaji makubwa ya kuni yanayosababisha miti mbalimbali ya asili kufyekwa hususani miyombo. Kwa mujibu wa utafiti huo, asilimia
75 ya wakazi wa wilaya za Tabora ni wakulima wa tumbaku, wanalima wastani wa
ekari 1.3 za tumbaku kwa mkulima kila msimu, zinazohitaji meta za ujazo 23 za
kuni kuchoma majani ya tumbaku.
Mtafiti Mkuu katika utafiti huo, Mwita
Mangora, anasema masalia ya misitu mkoani Tabora yaliopo sasa hayana uwezo wa
kukidhi matumizi makubwa ya kuni za kuchomea
majani ya tumbaku yanayoongezeka kila mwaka.
Tumbaku
hukaushwa kwa kutumia nishati ya kuni, hali ambayo husababisha ukataji mkubwa
wa miti kwa ajili ya kufanikisha kazi hiyo, hivyo kuchangia kutoweka kwa misitu
ambayo ni vyanzo vikuu vya maji kwa ajili ya binadamu na viumbe hai wengine.
Pamoja na kujulikana kwa uwazi kabisa
juu ya madhara ya matumizi ya tumbaku kwa kiwango hicho, bado serikali na jamii
kwa ujumla wake imeendelea kuchukulia tumbaku kama moja ya zao muhimu ya
kiuchumi katika nchi yetu.
Kulingana na taarifa za benki kuu ya
Tanzania(BOT), mchango wa zao la tumbaku kwenye uchumi wa taifa ni mkubwa,
kutokana na zao hilo kila mwaka katika mauzo ya tumbaku kuchangia zaidi ya dola
za kimarekani milioni 150.
Wakulima
wakubwa kwa wadogo wanalima tumbaku, serikali nyingi duniani ikiwamo ya
Tanzania zinapata kodi kubwa kutoka kwenye mazao ya tumbaku kama sigara na
nyinginezo, hivyo inakuwa vigumu kwa bajeti ya serikali Kupangwa bila tumbaku
kuguswa kama chanzo cha mapato.
Sera na
mikakati mbalimbali ya kilimo imekuwa ikitazama tumbaku kama mkombozi kwa
wakulima na serikali kwa ujumla. Sigara ni biashara ya makampuni makubwa ya
kimataifa yakiwa yametawanya mitandao yao katika mataifa mbalimbali ulimwenguni,ikiwemo
hapa nchini.
Licha ya
kwamba biashara ya tumbaku inaingiza fedha nyingi, ikitazamwa kwa darubini
kali, faida yake haina maana sana kwani serikali kwa kuwa inajikuta inaingia
katika athari za kiafya kwa wananchi na uharibifu mkubwa wa mazingira kutokana
na ukataji wa miti zinazotumika kukaushia tumbaku.
Uchunguzi
umebaini kuwa madhara ya tumbaku ni makubwa zaidi kuliko faida, kwani wakati
sasa dunia inalia kutokana na mabadiliko ya tabia nchi, na juhudi kubwa zikielekezwa
katika shughuli za uzalishaji mali na utunzaji bora wa mazingira, kilimo cha
tumbaku kinabakia kuwa moja ya shughuli yenye madhara zaidi kwa uchumi na kimazingira.
Maeneo yanayolima
zao la tumbaku hapa nchini ikiwemo mkoa wa Morogoro,Tabora,Chunya mkoani Mbeya
na Namtumbo mkoani Ruvuma hali ya mazingira ni mbaya kwa kuwa wakulima
wanafyeka misitu ya asili ili kupata kuni za kuchomea majani ya tumbaku na
kuacha maeneo hayo kuwa wazi na kukaribisha jangwa jambo ambalo ni hatari.
Kutokana na
madhara makubwa ambayo yanaletwa na zao la tumbaku kimazingira na kiafya ni
vema sasa jamii katika maeneo ambayo yanazalisha tumbaku ikaanza kujipanga
kutafuta mbinu endelevu za kuachana na shughuli ya kilimo cha tumbaku na kuanza
kuzalisha mazao mbadala.
albano.midelo@gmail.com,simu
0766463129

No comments:
Post a Comment