![]() |
| Pichani ni milima ya Livingstone Kihagara Nyasa |
Na Albano Midelo
WAKULIMA wanaodaiwa
kutokea wilayani Mbinga mkoani Ruvuma wamevamia misitu ya hifadhi ya milima ya
Livingstone iliyopo kando kando mwa ziwa
Nyasa mkoani Ruvuma na kuteketeza maelfu ya misitu kwa kuifyeka na kuichoma
moto.
Hayo yamefahamika
kwenye mafunzo ya hifadhi ya ardhi na vyanzo vya maji yaliofadhiliwa na
shirika lisilo la kiserikali la The Foundation For Civil Society na kushirikisha washiriki 60 kutoka vijiji 12 vilivyopo katika kata nne
zilizopo kwenye Halmashauri ya wilaya ya Nyasa mkoani Ruvuma na kufanyika
katika ukumbi wa Tigo mji mdogo wa Liuli.
Mafunzo hayo ambayo
yameendeshwa na mtandao wa mazingira
mkoa wa Ruvuma (RUNEA) yameshirikisha washiriki kutoka kata za
Mbambabay,Liuli,Kihagara na Lipingu ambao wameanza kupata athari za kimazingira
ambazo zinatokana kuvamiwa,kufyeka na kuchomwa moto milima ya hifadhi ya
Livingstone hali iliyosababisha mvua kupungua katika kiwango kikubwa kwa wakazi
wa vijiji vya kata hizo.
Washiriki katika
mafunzo hayo walidai kuwa eneo kubwa la hifadhi ya milima ya Livingstone
limeteketezwa na wakulima waliotokea
wilayani Mbinga ambao wanaendesha kilimo cha kuhamahama na baadhi yao
wameanzisha makazi ndani ya mlima wa hifadhi hali iliyosababisha safu wa milima
ya livingstone kubakia wazi na kuanza kuleta athari za kimazingira kwa wakazi
wa mwambao mwa ziwa Nyasa.
Mmoja wa washiriki
Onesmo Nkandawile ambaye ni afisa mtendaji wa kata ya Mbambabay alidai kuwa
kilimo cha kuhamahama katika mazao ya mpunga na ulezi kinachofanyika kila mwaka
kwenye milima ya Livingstone kinateketeza ekari nyingi za misitu ya asili na
kusababisha kiwango cha mvua kupungua
ukilinganisha na miaka michache nyuma kabla msitu huo haujavamiwa na kuteketezwa.
“Kwa kweli hali ni
mbaya wakulima kutoka wilayani Mbinga wamevamia msitu wa hifadhi,mkulima mmoja
anakata miti ya asili kati ya ekari tatu hadi tano kila mwaka anaichoma miti
kisha kulima mpunga na ulezi kwenye milima ya hifadhi,wapo ambao wameanzisha
makazi katika milima hiyo,hivi sasa mvua zimepungua mwambao mwa ziwa Nyasa’’,alisisitiza
Nkandawile.
Ameshauri elimu ya
utunzaji wa mazingira kutolewa mara kwa mara kwa wakazi wote kupitia
mikutano ya hadhara pamoja na kuhamasisha upandaji wa miti kila mwaka
ili kukabiliana na upungufu mkubwa uliopo hivi sasa kwenye safu za milima ya
Livingstone.
Afisa mtendaji wa
kata ya Lipingu Michael Milinga anasema misitu ya asili ya milima ya
Livingstone katika kata nzima imevamiwa na watu wa kabila la wamatengo ambao
walikaribishwa na wenyeji wa mwambao mwa ziwa Nyasa miaka ya nyuma ambapo hivi sasa wameteketeza
msitu wa asili katika milima hiyo kuanzia juu ya milima hadi kandokando na kusababisha uharibifu mkubwa wa mazingira
katika milima hiyo.
Hilda Chua,Monica
Njaku,Nathani Mpangala,Abdon Ndunguru na Jerome Ndomba wakazi wa kata ya
Kihagara kwa pamoja wameishauri serikali kuwachukulia hatua kali,wote
wanaohusika na vitendo vya ukataji miti ovyo na uchomaji moto kwenye hifadhi ya
milima ya Livingstone ambao bado wanaendeleza uharibifu unaosababisha milima
hiyo kubakia mitupu baada ya maelfu ya misitu kufyeka na kuchomwa moto.
Mwezeshaji katika
mafunzo hayo ambaye pia ni afisa wa maliasili na mazingira katika Halmashauri
ya wilaya ya Nyasa Bugingo Bugingo alisisitiza shughuli zozote za kibinadamu ikiwemo
kilimo haviruhusiwi katika milima ya
hifadhi kama ilivyo kwenye milima ya Livingtone ambayo kisheria imehifadhiwa.
“Ukanda wote wa
milima ya Livingstone iliyopo kando kando mwa ziwa Nyasa ni hifadhi ndiyo maana
imeingizwa kuwa moja ya vivutio vya utalii,hairuhusiwi kuguswa na kufanya shughuli zozote za
kibinadamu wote waliolima na kuweka makazi wataondolewa kwa mujibu wa
sheria’’,alisisitiza Bugingo.
Akitoa mada ya
hifadhi wa mazingira ya ardhi na vyanzo vya maji,mwezeshaji ambaye pia ni afisa
maliasili na mazingira wa wilaya ya Nyasa Bugingo Bugingo alisema uharibifu wa mazingira ni utekelezaji
wa mifumo mibaya ambayo uharibu hali ya asili iliyopo unaotokana na mambo
mbalimbali.
Aliyataja baadhi ya
mambo hayo kuwa ni kukata miti ovyo,kuchoma moto misitu ovyo,kilimo cha
umwagiliaji kisicho endelevu,kulima matuta kwa kufuata mteremko na kilimo
kwenye miteremko mikali kisichofuata kanuni bora za kilimo na kusababisha
mmomonyoko wa udongo na upotevu wa rutuba.
Kwa mujibu wa
mtaalamu huyo sababu nyingine za uharibifu wa mazingira ni kufuga mifugo
mingi,kuendesha kilimo katika vilele vya milima na kingo za mito,uchimbaji
madini,kokoto,mchanga na matofali usiofuata utaratibu. uharibu mazingira ya misitu,ardhi na vyanzo vya maji.
Alizitaja athari za uharibifu wa mazingira kuwa ni pamoja na
kutoweka kwa uoto wa asili, kupungua kwa mazao ya misitu kama vile
mbao,kuni,asali,uyoga na matunda,kuongezeka kwa joto duniani na kusababisha
kutoboka kwa tabaka salama angani(o-zone
layer),mafuriko,ukame,jangwa,njaa,uchafuzi wa hewa kutokana na mlundikano wa
hewa ukaa(carbon dioxide) na upotevu wa rutuba kutokana na mmomonyoko.
Hata hivyo ili
kukabiliana na uharibifu wa mazingira Bugingo amewashauri wadau wote kuacha kukata miti ovyo,kudhibiti
uchomaji wa moto holela,kupanda na kuitunza miti inayohifadhiwa maji kwenye
vilele vya milima na vyanzo vya maji hususani safu za milima ya
Livingstone,mito na mabonde yote ya ziwa Nyasa.
Uchunguzi ambao
umefanywa na gazeti hili umebaini kuwa kuna idadi kubwa ya watu wameweka makazi
ya kudumu na tayari wamefyeka misitu ya
asili kwenye safu za milima ya
Livingstone ambayo awali kulikuwa na wanyamapori wa aina mbalimbali wakiwemo mbega
weupe,nyani,sungura ,chui na wanyama wengine ambao wametoweka baada ya mlima kubaki bila miti kutokana na kufyekwa miti na kuchomwa na wavamizi kwa ajili ya kilimo na makazi.
Uchunguzi umebaini
kuwa wananchi wameweka makazi na kulima kwenye hifadhi za milima Livingstone
baada ya kupata baraka kutoka kwa wanasiasa ambao wamekuwa wanawazuia wataalamu
wa maliasili na mazingira kusimamia sera
na sheria za mazingira zinazopiga marufuku shughuli zote za kibinadamu kwenye hifadhi na vyanzo vya maji.
Kwa upande wake mwenyekiti wa mtandao wa
mazingira mkoa wa Ruvuma (RUNEA) Method Ngerangera ameelezea masikitiko yake
kufuatia uharibifu mkubwa ambao umefanywa na wavamizi kwenye milima ya hifadhi
ya Livingstone na kusababisha maelfu ya ekari za misitu ya asili kuteketezwa
kutokana na kilimo na kuweka makazi.
Hata hivyo Ngerangera
ameahidi ofisi yake ambayo inahusika
kulinda na kuzuia uharibifu wa mazingira,itatoa bure miche 500 ya miti
ya asili kwa ajili ya kupanda kwenye maeneo ya hifadhi ya milima ya Livingstone
ambayo yamebakia wazi hasa katika kata za Liuli,Mbambabay,Kihagara na Lipingu
na ametoa mwito kwa serikali kutumia sheria zilizopo ili kuwakamata wote ambao
wanaendelea kufyeka misitu na kuchoma moto kila mwaka katika hifadhi ya milima
ya Livingstone.
Kwa mujibu wa sera ya Taifa ya misitu ya mwaka
1998, Tanzania ina karibu hekta milioni 33.5 za misitu ambapo theluthi mbili ya
hekta hizo ipo mashakani kutokana na
ukosefu wa usimamizi mzuri hali inayosababisha watu kuvamia na kuharibu misitu
kwa ajili ya kilimo,malisho ya mifugo,moto,uchimbaji madini,ujenzi na shughuli
nyingine.
Licha ya kwamba
hakuna takwimu za kuaminika kuhusu kasi ya kutoweka kwa misitu,inakadiriwa kuwa
hapa nchini ni kati ya hekta 130,000 hadi 500,000 za misitu zinafyekwa kila
mwaka hali inayokatisha tamaa jitihada za kukabiliana na mabadiliko ya
tabianchi ambayo yanahitaji miti ili kupunguza hewa ukaa .
Sheria ya usimamizi
wa mazingira namba 20 ya mwaka 2004 fungu namba 187 kwa makosa yanayohusu
uchafuzi wa mazingira ya maji,hewa,ardhi na uchomaji moto ovyo,pia fungu namba
188 kwa makosa yanayohusu uharibifu wa bioanuwai ,adhabu ya jumla fungu namba
191 inasema kuwa mtu yeyote atakayekiuka
chochote cha sheria hiyo akitiwa hatiani atatozwa faini isiyopungua sh.50,000
na isiyozidi milioni 50 au kifungo kisichopungua miezi mitatu au kisichozidi
miaka saba jela ama vyote viwili.
albano.midelo@gmail.com,simu
0766463129

No comments:
Post a Comment