![]() |
| Baadhi ya wakazi wa Mfaranyaki Songea wakigombea maji |
Na Albano
Midelo
WAKAZI wa manispaa ya
Songea mkoani Ruvuma wapo katika vita kali ya kugombea maji huku wakiwa katika
hatari ya kupata magonjwa kutokana na kutumia maji ya mito na visima ambayo sio
safi na salama.
Wakazi hao wameamua
kutumia maji hayo kutokana na mgawo mkali wa maji unaofanywa na mamlaka ya maji
safi na salama Songea SOUWASA tangu mwezi Septemba mwaka huu.
Uchunguzi ambao
umefanywa katika maeneo mbalimbali ya pembezoni na katikati ya mji umebaini kuwa
tatizo la maji ni kubwa ambapo wakazi
wake wengi wao wakiwemo wanawake na watoto wanazunguka katika maeneo mbalimbali
kutafuta maji ya bomba bila mafanikio hali iliyosababisha wananchi kutumia maji
ambayo sio salama.
Christina Komba mkazi
wa Mfaranyaki alisema sasa miezi miwili hajapata maji ya bomba kutoka SOUWASA
hali ambayo imemlazimisha kutumia maji ya visima ambayo pia yanapatikana kwa
shida kutokana na idadi kubwa ya watu wanaotumia maji hayo.
Ngohi Nkondola mkazi
wa Mjimwema anasema ni miezi miwili na nusu sasa hawajapata maji kutoka
SOUWASA hata hivyo SOUWASA kila mwisho
wa mwezi wamekuwa wanasoma mita na kuleta bili yenye VAT na kwamba baadhi ya
mamalishe hulazimika kila siku kutumia sh.10,000 kukodi gari la kubebea maji
toka Matogoro umbali wa kilometa saba.
Mwandishi ameshuhudi
misululu mirefu ya foleni ya akinamama na watoto wakijipanga kuchota maji
kwenye visima asubuhi na jioni katika maeneo karibu yote ya mji wa Songea na
kwamba maji yanayotoka kwenye visima hivyo yamepungua hali inayosababisha
foleni kubwa ya watu wakisubiri kupata walau ndoo moja ya maji na baadhi yao
wanadai kuibiwa ndoo na simu.
Baadhi ya maeneo
wananchi wameonekana wanachota maji yenye rangi ya tope huku wadudu wakionekana
hali ambayo kiafya yanaweza kusababisha magonjwa mbalimbali yakiwemo ya ngozi
na matumbo jambo ambalo linaweza kuathiri nguvukazi.
Veronika Ndunguru
mkazi wa Ruhuwiko alisema uhaba wa maji katika mji wa Songea unaendelea
kuongezeka kwa kasi kila mwaka na kwamba
mwaka huu hali imekuwa mbaya zaidi kwa kuwa SOUWASA wameshindwa kabisa
kusambaza maji hivyo wananchi wengi wanategemea zaidi maji kutoka kwenye visima
na mito.
Mhandisi Jones Salema
ni meneja uzalishaji wa maji
SOUWASA amekiri kuwepo upungufu
wa uzalishaji na usambazaji wa maji kwa wakazi wa mji wa Songea ambao mwezi Oktoba mwaka huu umefikia meta za ujazo 2150 ukilinganisha na mwezi Oktoba mwaka jana ulikuwa meta za ujazo
2400 .
“SOUWASA hivi sasa
tunazalisha maji kwa siku lita za ujazo milioni mbili tu wakati mahitaji ya
maji kwa siku katika mji wa Songea ni lita za ujazo milioni 13,hali ni mbaya
sana chanzo tunachokitegemea zaidi ni cha Lipasi ambacho kina uwezo wa
kuzalisha mita za ujazo 1287 kwa siku’’,alisema Salema.
Mhandisi Salema
amekiri kuwa maji yamepungua katika kiwango cha kutisha kwenye vyanzo vya
maji milima ya Matogoro vinavyotegemewa
na SOUWASA kwa takribani miaka mitano sasa mfululizo kutokana na sababu mbalimbali.
Alizitaja sababu hizo
kuwa ni mabadiliko ya tabianchi,kuongezeka kwa idadi ya watu katika manispaa ya
Songea ,kuongezeka kwa shughuli za kibinadamu ambazo zinachangia kuharibu
vyanzo hivyo kwa kulima na kulisha mifugo kwenye vyanzo hivyo.
Ameyataja matarajio
ya muda mrefu ya SOUWASA katika kukabiliana na uhaba wa maji katika mji wa
Songea kuwa ni kujenga bwawa kubwa katika chanzo cha Mahiro ambalo litakuwa na uwezo wa kuzalisha maji
lita za ujazo milioni tano pamoja na kujenga bwawa la kuhifadhia maji katika
chanzo cha maji cha Luhira darajani lenye uwezo wa meta za ujazo milioni moja
na kwamba tayari serikali imetoa sh.milioni 400 kwa ajili ya ujenzi huo.
Hata hivyo Contancia
Timoth afisa maji Bonde la ziwa Nyasa ofisi ndogo Songea alisema SOUWASA
wanatumia vyanzo vitatu vya maji vya bonde hilo kusambazia maji katika mji wa
Songea ambavyo alivitaja vyanzo hivyo vilivyopo milima ya Matogoro kuwa ni
Luhira A,Luhira B na Mahiro.
Hata hivyo alisema
uharibifu mkubwa wa mazingira unaofanywa katika vyanzo hivyo kutokana na
shughuli za kibinadamu umechangia upungufu mkubwa wa maji hali inayosababisha
SOUWASA kukosa maji ya kutosha kila mwaka kuanzia mwezi Septemba hadi Desemba.
“Vyanzo vya maji vimevamiwa,miti iliyokuwa rafiki
ya maji kama vile minyonyo, matete na mikuyu imeteketezwa, wananchi wanalima
hadi kwenye vyanzo vya maji,sisi kama bonde tumekuwa tunatoa elimu ya mazingira
na kuunda jumuiya ya watumia maji lakini bado changamoto ni kubwa’’,alisisitiza.
Kutokana na ukubwa wa
tatizo la maji mjini Songea afisa huyo wa maji amewashauri SOUWASA kuangalia
uwezekana kupata chanzo kingine kilichopo katika bonde hilo ambapo alikitaja
chanzo cha maji cha Lumecha kilichopo takriban kilometa 30 kutoka mjini Songea
kinaweza kumaliza tatizo hilo kwa kuwa kina maji ya kutosha.
Utafiti umebaini kuwa
chanzo cha maji cha Lumecha kinaweza kutumika kwa zaidi ya miaka 50 ijayo hivyo
kumaliza kero kubwa ya uhaba wa maji
inayowakabili wakazi wa mji wa Songea hasa kuanzia mwezi Septemba hadi
Desemba kila mwaka.
Meneja uzalishaji wa
maji wa SOUWASA mhandisi Jones Salema amekiri kuwa chanzo cha Lumecha kinaweza kumaliza
tatizo la maji katika mji wa Songea hata hivyo alisema mradi huo unahitaji pesa
nyingi kwa ajili ya gharama za ujenzi wa
chanzo, umeme na kutibu maji.
Uchunguzi umebaini
kuwa uvunaji wa miti usiokuwa endelevu uliokuwa unafanywa katika msitu wa serikali
wa milima ya Matogoro nje kidogo ya mji wa Songea umeleta athari kubwa za
kimazingira na kufanya vyanzo vya maji vinavyotegemewa na SOUWASA kuwa hatarini
kutoweka .
Uvunaji wa miti hiyo
ulipewa kibali na wizara ya maliasili na utalii kupitia idara ya misitu na
nyuki kuhakikisha kuwa miti yote ambayo sio rafiki inavunwa katika msitu wa
Matogoro ambao una vyanzo vya maji vya mito ya Luhira unaomwaga maji yake ziwa
Nyasa,mto Ruvuma unamwaga maji yake bahari ya Hindi na mto Luegu ambao unazaa
mto Rufiji.
Waziri wa nchi ofisi
ya makamu wa Rais Mazingira Dk.Terezya Luoga akizungumzia uvunaji wa miti
katika msitu wa Matogoro alisema anakubaliana na utafiti ambao umefanywa wa
kuhakikisha kuwa miti yote iliyopo hivi sasa inavunwa na kupandwa miti ya asili
ambayo ni rafiki wa maji hata hivyo alisema hakubaliani na uvunaji wa miti
usiokuwa endelevu unaofanywa katika msitu huo.
“Mimi ni mzaliwa wa
Songea, miaka yote tumekaa Songea na misitu hii ya Matogoro, hatujawahi kukosa
maji,lakini hivi sasa wakati wa kiangazi mji wa Songea unapata upungufu mkubwa
wa maji,kunakuwa na mgawo mkali wa maji hizi ndizo dalili za awali za uharibifu
wa mazingira kwenye msitu huu kwa kuwa mnafanya uvunaji usiokuwa endelevu ”,anasisitiza
Dk.Huvisa.
Licha ya uharibifu
mkubwa wa mazingira katika vyanzo vya maji vilivyopo kwenye milima ya
Matogoro,utafiti umebaini kuwa karibu vyanzo vyote vya maji vinavyozunguka mji
wa Songea vimevamiwa kwa shughuli
mbalimbali za kibinadamu ikiwemo kilimo,uchimbaji mchanga,uchimbaji visima
holela,mabwawa ya samaki na makazi ya watu.
Sheria ya mazingira namba 57 ya mwaka 2004 inataka shughuli za
kibinadamu kufanyika umbali wa meta 60 kutoka katika kingo za mto na kwamba
yeyote anaharibu mazingira anafanya
makosa
akitiwa
hatiani atatozwa faini isiyopungua sh.50,000 na isiyozidi milioni 50 au kifungo
kisichopungua miezi mitatu au kisichozidi miaka saba jela ama vyote viwili.
Sera maji ya mwaka 2002 inalenga kuhakikisha kuwa vyanzo vya maji
vilivyopo vinatunzwa,kulindwa na kuendelezwa kwa utaratibu unaozingatia uwiano
wa mahitaji ya viumbehai wote.
albano.midelo@gmail.com,simu 0766463129

No comments:
Post a Comment