Saturday, November 30, 2013

TANESCO yamaliza mgawo wa umeme


Na Albano Midelo
Kaimu meneja wa TANESCO mkoa wa Ruvuma Timoth Ramadhan
HATIMAYE shirika la ugavi wa umeme TANESCO limemaliza kero sugu ya mgawo mkali wa umeme katika manispaa ya Songea baada ya kufungwa vipuri vipya vya mashine za kuzalishia umeme.
Kaimu meneja wa TANESCO mkoa wa Ruvuma mhandisi Timoth Ramadhan alisema katika mahojiano maalum ofisini kwake mjini Songea kuwa mgawo mkali wa umeme umemalizika baada ya TANESCO kufanikiwa  kufunga vipuri vipya katika mashine zake zote.

“Mashine tano zote zinafanyakazi na kuweza kuzalisha umeme wa kilowatt 4600,mahitaji katika mji wa Songea na Peramiho ni kilowatt 4300 hivyo hivi sasa tunazalisha ziada ya umeme wa kilowatt 300,mgawo wa umeme haupo kabisa tangu wiki iliyopita’’,alisisitiza Ramadhan.
Alizitaja aina za mashine zinazozalisha umeme kuwa ni mashine  tatu za zamani  aina ya watisira zilizotolewa kabla ya uhuru,mashine moja aina ya katapila na mashine moja aina ya ABC iliyotolewa na Rais Jakaya Kikwete mwaka 2011 ambayo ilizimwa mwezi Oktoba mwaka huu baada ya kupata hitilafu hali iliyosababisha mgawo mkali wa umeme.
Hata hivyo kaimu meneja huyo wa TANESCO mkoa wa Ruvuma aliongeza kuwa matengenezo bado yanaendelea katika mashine nyingine ikiwemo aina ya ABC  ambayo hivi sasa inazalisha kilowatt 1200 badala ya kilowatt 1700 na kwamba matengenezo hayo yakikamilika mwezi ujao mashine hizo zitazalisha umeme wa kilowatt 6800 na kufanya mgawo wa umeme kubakia kuwa historia.
Kulingana na kaimu meneja huyo kuanzia wiki ijayo TANESCO Ruvuma inatarajia kuanza kuwaunganishia umeme wateja 574 walioomba kuunganishiwa umeme tangu mwezi Mei mwaka huu kutoka katika wilaya za Tunduru,Mbinga,Namtumbo na Songea.
Hata hivyo alisema kuchelewa kuwaunganishia umeme kumetokana na TANESCO kukosa waya mnene unaoanzia kwenye nguzo hadi kwenye mita ambapo waya huo tayari umepatikana na kuanzia wiki ijayo wanaanza kazi ya kuwaunganishia kulingana na wateja waliowahi kuomba.
Baadhi ya wakazi wa mji wa Songea wamelipongeza shirika la umeme nchini kumaliza mgawo wa muda mrefu wa umeme katika manispaa ya Songea ambao walidai ulikuwa kero kubwa na kuchangia kukwamisha shughuli za kiuchumi.
John Haule ameipongeza serikali kwa kusikiliza kilio cha wananchi wa Songea na kusisitiza kuwa sasa huduma ya umeme inapatikana kwa uhakika  saa 24 bila umeme kukatika ovyo huku na kuongeza kuwa maendeleo yanaweza kupatikana kwa kuwa umeme ni muhimu katika shughuli za kijamii na kiuchumi.
Mwandishi ameshuhudia karibu kila mahali katika mjini  Songea na Peramiho wananchi wakifurahia huduma bora ya umeme ambao kwa wiki tatu mfululizo sasa hakuna mgawo wa umeme kama uliokuwepo awali kabla ya kufungwa vipuri vipya mwezi  huu.
Tatizo la mgawo mkali wa umeme liliongezeka mwaka huu mjini Songea kutokana na kile ambacho kilielezwa na TANESCO mkoa wa Ruvuma kuwa ni kuharibika kwa vipuri vya mashine za kuzalishia umeme hali iliyosababisha umeme kuzalishwa kilowatt 3050 tu kati ya mahitaji ya umeme wa kilowatt 4300 .
Kutokana na tatizo la umeme kuongezeka katika mji wa Songea kaimu mkurugenzi wa shirika la umeme nchini  Mhandisi Felchesmi Mramba mwezi Oktoba alilazimika kufanya ziara ya siku moja mjini Songea ili kujionea hali halisi ya tatizo la umeme katika Manispaa ya Songea ambao alisema unatokana  na kuharibika kwa vipuri vya mashine ya kufua umeme aina ya ABC.
Serikali kupitia wizara ya nishati na madini iliagiza vipuri vipya vya mitambo ya kufua umeme   kutoka nchini uholanzi na kuvifunga katika mashine za kuzalishia umeme hali iliyomaliza tatizo la mgawo mkali wa umeme katika mji wa Songea kuanzia mwezi Novemba.
Hata hivyo TANESCO kwa kushirikiana na ufadhili wa serikali ya Sweden chini ya shirika lake la SIDA,inaanza utekelezaji wa mradi wa umeme kutoka Makambako mpaka Songea.
 Taarifa ya wizara ya nishati na madini inaeleza kuwa ujenzi wa mradi wa njia kuu ya kusafirisha umeme wa gridi kutoka Makambako hadi Songea ambao utahusisha pia kujenga mifumo ya kusambaza umeme vijijini katika Wilaya za Ludewa, Namtumbo na Mbinga ni hatua muhimu ya kuleta maendeleo endelevu katika mikoa ya Kusini.
Sera ya Serikali katika umeme ni kuhakikisha wananchi wengi wanapata nishati ya umeme,ingawa takwimu hivi sasa zinaonesha kuwa wananchi wanaopata nishati ya umeme haizidi asilimia 10 ya wananchi wote nchini na kati ya asilimia 10, ni asilimia moja tu ya wananchi wanaoishi vijijini ndio wanaopata nishati ya umeme.


No comments:

Post a Comment