Tuesday, May 13, 2014

Kilimo cha Ngoro kilianzishwa miaka 300 iliyopita Mbinga


Na Albano Midelo 
NGORO pichani ni aina ya kilimo kinachohifadhi mazingira kwa njia ya asili ambacho kinaaminika kilianza kutumika na wakulima wa kabila la wamatengo wilayani Mbinga mkoani Ruvuma zaidi ya miaka 300 iliyopita.
Kilimo cha ngoro kilianzishwa na wazee maarufu wa kabila la wamatengo waliotokea nchini Malawi katika karne ya 17 ambapo tayari vizazi zaidi ya 10 vimepita hivi sasa tangu kilimo cha ngoro kilipoanzishwa wilayani Mbinga.

 Moja ya madhumuni ya kuanzisha kilimo hiki ni kuudhibiti udongo wa juu wa ardhi  ambao kwa kawaida huondolewa na maji au upepo  kutokana na mmomonyoko wa ardhi ya juu ambayo ina rutuba nyingi ya kuifanya mimea iweze kustawi vizuri na hatimaye kutoa mavuno mengi na bora.
‘‘Tunajua kuwa udongo ulio chini ya tabaka la juu hauna rutuba ya kutosha ya kuwezesha mazao kustawi vizuri, Kutoweka kwa udongo wa juu toka shambani au bustani kwa njia ya mmomonyoko ni hasara kubwa , kwa vile kunasababisha upungufu wa mavuno. Hivi basi lazima kuzingatia hifadhi ya ardhi ili mkulima aweze kupata mazao bora’’,anasema Ngwatura Ndunguru mbunge mstaafu wa Mbinga.
Njia za kuhifadhi ardhi zinaweza kutumiwa kwa kutegemea hali ya hewa, mazingira ya eneo kama ni maeneo ya mwinuko au tambarare. Hata hivyo zinaweza kutumika njia mbili au tatu katika shamba moja. Ziko njia kuu mbili za kuhifadhi ardhi ambazo ni njia za asili au za kienyeji na njia ya kisasa ambazo zimefanyiwa utafiti wa kina na wataalamu.
 Wataalamu wazungumzia ngoro
Wataalamu wakongwe kama akina Bike  mwaka 1938, Stenhouse  mwaka 1994,  Temu na Bisanda  mwaka 1966 wanaeleza kuwa Wamatengo walilazimika kutumia kilimo cha ngoro  ili kuhifadhi udongo mzuri uliopo katika miteremko hiyo. Ngoro hulimwa kwa kuchimba mashimo madogo madogo katika miteremko hiyo.
Katika mashimo hayo hupandwa mazao kama maharage,mahindi na ngano kwenye kingo za mashimo hayo. Mkulima hufyeka shamba  lake  na kuzipanga nyasi zilizokatwa katika mistari kwenda juu mpaka chini na toka upande wa kushoto kwenda kulia.
 Mkulima akipindua udongo wa chini kuwa juu na chini ya udongo wa juu hukata nyasi na udongo wenye rutuba hugeuka kuwa mboji na polepole udongo wenye rutuba huongezeka. Maji ya mvua yakisimama katika mashimo hayo  madogo hulinda unyevu wa ardhi na kukinga mmomonyoko wa ardhi.
Inaaminika kuwa kilimo cha ngoro ambacho tunaweza kukiita draft agriculture kinahusishwa na shughuli za kuwepo kwa mapango ya kuishi.Historia ya wilaya ya Mbinga inaonyesha kuwa,hapo zamani wananchi wa wilaya ya Mbinga walikuwa na tabia ya kufanya kilimo cha kuhamahama.
Wakulima wakati huo walilima sehemu moja na wanapogundua sehemu hiyo rutuba imemalizika walikuwa wanahamia sehemu nyingine yenye rutuba na kuendesha kilimo bila kujali athari za kimazingira ambazo zilikuwa zinajitokeza kutokana na aina hiyo ya kilimo.
Kutokana na kuwepo kwa mapango, wazee hao wa kabila la wamatengo waliamua kuanzisha kilimo cha kulima na kufukia majani  ili kupata mbolea ya asili hivyo kuendesha kilimo walichokiita ngoro katika sehemu moja bila kuhama huku wakirutubisha ardhi na kuzuia mmomonyoko wa udongo kutokana na ardhi ya Mbinga kuwa  na milima yenye miteremko mikali.
Mbunge mstaafu wa Mbinga  Ngwatura Ndunguru anasisitiza kuwa wamatengo tangu wameanza kutumia kilimo cha ngoro miaka 300 iliyopita hadi sasa wamekuwa wanazalisha vyakula kwa wingi pamoja na kuhifadhi mazingira kwa njia ya asili kwa kuzuia mmomonyoko wa udongo kutokea kwenye miteremko ya milima ya umatengo wilayani humo.
Anabainisha zaidi kuwa kilimo cha ngoro ni sawa na mchanganyiko wa kilimo cha umwagiliaji  mvua zinaponyesha maji huingia taratibu kuingia kwenye mmea na kuzuia udongo usiharibiwe na kwamba yale majani yaliyowekwa chini yanaoza ambapo katika msimu mwingine wa kilimo majani yaliota kwenye shimo  yatafyekwa mazao yaliosalia yatavunwa na kutandazwa kwenye shimo na kufukuliwa majani ya mwaka jana ambayo tayari yanakuwa mboji.
John Mbunda(80) mkazi wa kijiji cha Kilanga Juu wilayani Mbinga anasema wamatengo walianzisha mfumo  maalumu ya kilimo cha ngoro uliyowasaidia uliyojulikana kwa jina la “Ingoro,” mfumo ambao uliwawezesha kuendelea kulima kwenye maporomoko ya milima bila ya kusababisha mmomonyoko wa udongo au kuathiri vibaya rutuba kwenye mashamba yao.
Alex Ndunguru mkazi wa kijiji cha Ilela anasema wenyeji wa Mbinga  walilazimika kubuni kilimo cha ‘ngoro ili kuhifadhi udongo mzuri ulio katika miteremko ya Umatengo na kwamba ngoro ndiyo mkombozi katika kilimo kwa kuwa kilimo kimekuwa endelevu badala ya mfumo wa zamani ambao wamatengo walifanya kilimo cha kuhamahama.
‘‘Nafurahia sana kilimo cha ngoro ambacho tunachimba vishimo katika miteremko na kupanda mazao kama maharage,mahindi, ngano, kwenye kingo za vishimo hivyo ambapo mkulima hutayarisha shamba kwa kufyeka nyasi,kisha kuzipanga nyasi zilizokatwa katika mistari, kuzigeuza na zikioza hupatikana udongo wenye rutuba’’,alisisitiza Ndunguru.
Teknolojia ya ngoro ni bora
 Utafiti wa kina umeonyesha wazi kwamba  teknolojia ya ngoro ni bora zaidi katika kilimo,ambapo wakulima kutoka  maeneo mbalimbali nchini wamekuwa wakifika katika wilaya ya Mbinga kujionea wenyewe na kujifunza teknolojia hiyo ya kilimo cha ngoro na kwenda kuanzisha aina hiyo ya kilimo katika maeneo yao kwa lengo la kuhifadhi ardhi na kutunza mazingira kwa muda mrefu.

Moja ya faida ya kilimo cha ngoro ni kwamba hata kama mvua hazitanyesha, bado shamba litaendelea kuwa na unyevunyevu kutokana na maji yaliyomo ndani ya mashimo hayo,isitoshe wakati wa mavuno, mabaki ya nafaka huwa yakitupwa kwenye mashimo hayo,husababisha shamba kustawi vizuri zaidi kutokana na mbolea iliyowekwa.
Ngoro kivutio cha utalii
Kulingana na Mbunge  mstaafu wa Mbinga Ndunguru tayari wameanza kukitangaza kilimo hicho na kukiingiza kuwa ni miongoni mwa vivutio vya utalii ambavyo vinapatikana katika wilaya ya Mbinga pekee na hakuna sehemu nyingine yeyote duniani inayoendesha kilimo cha aina hiyo.
  Baadhi ya wageni  ambao wamekuwa wakitembea kwenye magari kupitia barabara ya Mbinga hadi Mbambabay wilayani Nyasa pamoja na maeneo mengine ya milima ya umatengo wamekuwa wakisimama mara kwa mara kwenye milima hiyo na kuchukua picha za kawaida na video kwenye kilimo cha ngoro ambacho kimeonekana kuwavutia  watu wengi wa  ndani na nje ya nchi hasa mimea  inayochomoza na kuonekana mfano wa mapambo yaliopambwa  juu ya milima.
Wizara yatambua kilimo cha ngoro
Wizara ya Kilimo Chakula na Ushirika imeanzisha Mradi wa kufufua Mifumo muhimu ya asili ya kilimo Duniani (Global Importance Agricutural Heritage System- GIAHS) ili kuendeleza Kilimo cha asili (Oranic Farming) na kumpunguzia mkulima gharama za uzalishaji.

Afisa mkuu wa kilimo kutoka idara ya matumizi bora ya ardhi Firmat Banzi anasema mradi huo unatekelezwa na Shirika la chakula na kilimo Duniani (FAO) ambao unalenga kutambua mifumo ya asili na endelevu ya kilimo na ufugaji ili kumsaidia mkulima na kwamba mradi unagharimu zaidi ya dola laki mbili ambazo zimetolewa na Serikali ya Ujerumani.

Alisema kuwa katika Afrika Mashariki nchi ya Tanzania na Kenya ilichaguliwa kufufua mifumo hiyo kwa kuwa na sehemu muhimu za kilimo na kwamba baada ya kuchanguliwa nchi ya Tanzania ilipendekeza mifumo mitatu ya kilimo asili ukiwemo mfumo wa Ngoro ambao unatumiwa na kabila la wamatengo.

Mifumo ya asili ya kilimo ilianza kupendekezwa dunia toka mwaka 2002 na baadhi ya nchi zimeanza kutumia mifumo hii, baadhi ya nchi hizo ni Japani, Philipino, China na Ujerumani.

No comments:

Post a Comment