Na Albano Midelo
WATU wanaendelea
kupoteza maisha katika mto Ruhuhu kutokana na kuvuka mto huo kwa mtumbwi baada
ya kivuko cha MV Ruhuhu kushindwa kufanyakazi karibu msimu mzima wa mwaka.
Kutofanyakazi kwa
kivuko cha Ruhuhu kinachounganisha wilaya za Nyasa mkoani Ruvuma na Ludewa
mkoani Njombe kunasababisha vifo vya
watu wanaoamua kuvuka mto Ruhuhu kwa kutumia mitumbwi.
Wiki hii watu wanne
wamepoteza maisha wakati wanajaribu kuvuka mto Ruhuhu kwa kutumia mtumbwi,kasi
ya maji ya mto Ruhuhu ilisababisha kupindua mtumbwi na kusababisha vifo vya
watu wote waliokuwa wanavuka kutoka Lituhi wilayani Nyasa na kwenda wilayani Ludewa.
Kaimu afisa mtendaji
wa kata ya Lituhi Joseph Chawala amethibitisha kutokea kwa vifo hivyo na
kueleza kuwa miongoni mwa abiria waliokuwa ndani ya mtumbwi huo ni mama
aliyekuwa na mtoto na kwamba hadi sasa wamefanikiwa kupata mwili wa mtu mmoja
,miili mingine ukiwemo wa mama na mtoto wake bado haijapatikana hadi sasa.
Hata hivyo alisema
juhudi za wakazi wa Lituhi kuendelea kuitafuta miili mingine bado zinaendelea
ingawa alisema inawezekana miili hiyo imesombwa na maji hadi ziwa Nyasa.
Chawala alisema
wakazi wa kata ya Lituhi wapatao 12,000 wanapata shida kuvuka kutokana na
kivuko mto M.V Ruhuhu kuhshindwa kufanyakazi kwa mtu mrefu hali ambayo
inasababisha kuamua kuvuka kwa kutumia mitumbwi jambo ambalo limekuwa
linasababisha ajali ya mitumbwi hiyo kupinduka na kusababisha vifo.
“Kivuko cha Ruhuhu
kinafanya kazi kwa miezi mitatu tu kwa mwaka kinaanza mwezi Juni hadi
Agosti,hali hiyo inatokana na serikali kushindwa kujenga gati bora kwa ajili ya
kuweka nanga kivuko kinapotoka upande mmoja wa mto na kwenda upande
mwingine,maji ya mto Ruhuhu yanapokuwa mengi kivuko hakiwezi kupaki kwa sababu
gati yake imejengwa vibaya’’,alisema Chawala.
Alisema kuwa magari
yanashindwa kuvushwa katika kivuko hicho hali ambayo inasababisha kuzunguka
kutoka Lituhi, Songea hadi Njombe kisha Ludewa mjini safari ambayo inachukua
siku nzima wakati kwa kutumia kivuko cha M.V Ruhuhu ni mwendo wa saa moja hadi Ludewa mjini.
Baadhi ya wakazi wa
Lituhi na Ludewa walisema kivuko cha Ruhuhu ni kero ya muda mrefu ambayo hata
Rais Jakaya Kikwete anaifahamu na aliahidi kuitafutia ufumbuzi wa kudumu kwa
kuwa inagharimu maisha ya watu kila mwaka pia inazorotesha maendeleo yao
kiuchumi.
Julius Challe
mwenyekiti wa kitongoji cha Lituhi anasema wakazi wa Lituhi wanapata matatizo
makubwa kutokana na ukosefu wa huduma za kivuko cha Ruhuhu hawajui lini tatizo
hilo litapatiwa ufumbuzi wa kudumu kwa kuwa ni tatizo la muda mrefu ambalo
serikali imekuwa itoa ahadi zisizotekelezeka za kujenga daraja.
Joseph Mhagama miaka
69 anasema kivuko hicho licha ya kuwa ni kipya na injini zake zote mbili na
zinafanyakazi, tangu mwaka huu umeanza hakijafanyakazi na serikali haishituki kutokana na idadi ya watu
wanaopoteza maisha kila mwaka kutokana na
kuvuka mto Ruhuhu kwa njia ya mtumbwi.
Wananchi
wanaotegemea kivuko hicho kwa kiwango kikubwa ni kutoka vijiji vya
Msungu,Ilela,Mbongo,Manda,Lupingu na Ngerenge wilayani Ludewa mkoani Njombe na
vijiji vya Lituhi, Nkaya, Mwelampya,Kihulu,Litumbakuhamba
na Ngingama wilayani Nyasa mkoani Ruvuma.
Mbunge wa
Mbinga Magharibi Kapteni John Komba (CCM), amewahi kuiomba Serikali kujenga
daraja katika mto Ruhuhu ili kuwawezesha
wananchi kuvuka mto huo kwa urahisi kutokana na tatizo la kivuko cha M.V Ruhuhu.
Katika
swali lake lililoulizwa bungeni kwa niaba yake na mbunge wa Mbinga Mashariki
Gaudence Kayombo, lilieleza kuwa wananchi wamekuwa wakipata shida kuvuka mto
huo kutokana na kushindwa kufanya kazi kwa kivuko cha MV Ruhuhu katika kipindi
karibu chote cha mwaka.
Alisema
kivuko kipya kilichopo kwenye mto huo kimekuwa kikishindwa kufanya kazi wakati
wa masika maji yanapokuwa mengi na pia wakati wa masika kutokana na kina kifupi
cha maji hali aliyosema inasababisha usumbufu kwa wananchi.
Akijibu
swali hilo Naibu Waziri wa Miundombinu alisema kuwa Serikali inafahamu tatizo
lililopo katika kivuko hicho kipya kushindwa kutumika katika baadhi ya misimu
ya mwaka.
Alisema
kabla ya kununuliwa kwa kivuko hicho kulikuwa na tatizo kubwa la kivuko kwani
kivuko kilichokuwepo kilikuwa ni chakavu ambapo kiliendeshwa kwa kuvutwa na
kamba kwa kutumia nguvu za binadamu.
Alisema
Serikali iliamua kununua kivuko hicho kama suluhisho la muda wakati ikiendelea
na mikakati ya kutafuta fedha kwa ajili ya ujenzi wa daraja ambalo litawahakikishia usafiri wananchi
wanaoishi katika maeneo hayo.
Alisema
wakati mwingine kupungua kwa kina cha maji katika mto huo kumekuwa kukichangiwa
na uharibifu wa mazingira ambapo alitoa wito kwa wananchi wanaoishi kandokando
ya mto huo kushiriki kikamilifu katika kutunza mazingira ya mto huo ili maji
yasipungue.
Wakati
wa kampeni za uchaguzi wa mwaka 2005, Chama cha Mapinduzi kiliahidi kupitia
Ilani yake kutatua tatizo la vivuko kadhaa nchini, kimojawapo kikiwa ni kivuko
cha mto Ruhuhu mkoani Ruvuma ambacho kinaitwa kivuko cha M.V Ruhuhu ingawa ni
kivuko kipya kinashindwa kufanyakazi
karibu msimu wote wa mwaka.
albano.midelo@gmail.com,simu 0766463129

No comments:
Post a Comment