Saturday, May 31, 2014

Utumikishaji wanafunzi muda wa masomo bado tatizo

 Na Albano Midelo
WALIMU katika shule za msingi nchini  wamekuwa wanaendelea kuwafanyisha kazi  watoto wa shule za msingi bila kuzingatia muda wa masomo hali ambayo inachangia kushusha kiwango cha elimu nchini.
Mwandishi wa makala haya ameshuhudia hivi karibuni wanafunzi karibu wote shule ya msingi Mfuate pichani kulia iliyopo kata ya Likuyuseka wilayani Namtumbo mkoani Ruvuma wakifanyishwa kazi ya kubeba tofali muda wa masomo.

Mkazi wa kijiji cha Likuyu ambaye hakutaka jina lake kuandikwa alisema watoto kufanyishwa kazi imekuwa ni kitu cha kawaida katika shule za kata hiyo na kusisitiza kuwa watoto wanatumika pia kuwachotea walimu maji,kuosha vyombo na kazi nyingine za nyumbani.
“Huku ni mbali sana na makao makuu ya wilaya hivyo walimu wanawafanyisha kazi wanafunzi kwa kutambua hakuna anayeweza kuona  ingawa viongozi wa serikali za vijiji  wanaona hali hii lakini hakuna anayekemea hivyo imekuwa jambo la kawaida tu’’,alisisitiza.
Uchunguzi ambao umefanywa mwambao mwa ziwa Nyasa mkoani Ruvuma umebaini tatizo la wanafunzi kufanyishwa kazi mbalimbali muda wa masomo na baada ya masomo ni kubwa hali ambayo inachangia kushusha taaluma.
Odo Komba mkazi wa Liuli anasema kuna baadhi ya walimu wakuu wamekuwa wababe wanafanyisha kazi za kubeba kuni,tofali,maji na wengine wanawatumia watoto wao kuvua samaki muda wa masomo ametolea mfano shule ya msingi Muungano iliyopo kata ya Liuli imekithiri kwa vitendo vya kutumikisha wanafunzi.
Tatizo la wanafunzi kufanyishwa kazi muda wa masomo halipo Namtumbo na Nyasa mkoani Ruvuma pekee bali pia kulingana na mwandishi wa kujitegemea Fransis Godwin uongozi  wa shule  ya msingi Kising’a Isimani  wilaya ya  Iringa ulituhumiwa
kuwatumikisha kazi wanafunzi  wakati  wa vipindi  vya masomo.
 Kitendo hicho kililaniwa vikali na  baadhi ya  wazazi  ambao   watoto wao wanasoma katika  shule  hiyo ambapo wameiomba  wizara ya elimu na mafunzo ya ufundi kuingilia kati suala la utumikishaji wanafunzi wakati na baada ya masomo kwa kuwa bado ni sugu nchini.
 Wazazi hao   walidai  kuwa  uongozi  wa  shule  hiyo  kila  siku kabla ya  watoto  kuingia madarasani  wamekuwa  wakiwatuma katika kazi  mbali mbali  ikiwemo ya  kuchota maji ya walimu.  
Hata hivyo baadhi ya Halmashauri nchini zimeanza kuchukua hatua kukabiliana na kuwatumikisha watoto kwa mfano Halmashauri ya Wilaya ya Muleba mkoani Kagera, iliwahi kumvua madaraka ya ukuu wa Shule ya Msingi Kitunga, Mwalimu Salvatory Roman, kutokana na tabia yake ya kuwafanyisha kazi wanafunzi katika muda wa masomo.
Ofisa Elimu wa Halmashauri ya Wilaya ya Muleba, Pastory Kajuna,alisema Halmashauri hiyo ilifikia hatua hiyo baada ya kuchoshwa na tabia aliyokuwa amejijengea mwalimu mkuu huyo ya kuwatumikisha wanafunzi wa shule hiyo anavyotaka.

Alisema uongozi wa Halmashauri kupitia idara ya elimu ulishasambaza waraka maalumu katika shule zote zilizoko katika Halmashauri hiyo zinazowataka walimu kuacha kuwatumikisha wanafunzi wakati wa muda wa masomo.
 Zaidi ya nusu ya Watanzania ni watoto, kuwekeza kwa watoto kunanufaisha familia, jamii na ni kwa mustakbali wa Tanzania. Dira ya Tanzania inayostawi kiuchumi inaweza kufikiwa tu ikiwa watoto  watakua wakiwa na afya, wenye kupata lishe bora, elimu bora na kulindwa dhidi ya vurugu, udhalilishaji na unyonyaji.

Kila nchi iliyofikia kuwa na maendeleo ya kiuchumi ya kipato cha wastani imewekeza kwa watoto kwa kiwango kikubwa. kuwekeza kwa watoto kwenye elimu bora, huduma za afya zilizoboreshwa na kuwalinda watoto dhidi ya vurugu na udhalilishaji huzaa matunda yanayosababisha kuwepo kwa uchumi imara, kupungua kwa uhalifu na kuwepo kwa familia zenye afya bora.
Maendeleo makubwa yanaweza kupatikana kwa kuzihamasisha jamii , kuongeza uwajibikaji na uwazi na kuhakikisha kuwa Sheria ya Watoto inatekelezwa kikamilifu ili kuwalinda watoto.
Pamoja na kuwepo kwa mikataba ya kuwalinda watoto dhidi ya utumikishwaji,tatizo hili lnaongezeka kwa kasi na watoto kujikuta wakikosa haki zao za msingi kama kucheza,kupata elimu, kutunzwa na kulindwa.
Watoto wamejikuta wakigeuka vibarua katika mazingira hatarishi kama inavyothibitishwa na shirika linaloshughulika na utafiti la(REPOA) ambapo mwaka 2006 matokeo yanaonyesha asilimia 20 ya watoto kuanzia miaka 7-17 wanatumikishwa katika kazi zenye madhara.
Mwaka 2009 Bunge lilitunga Sheria ya mtoto namba 21 yenye lengo la kudumisha haki za watoto na kuwapa haki kisheria,ambapo kwa mujibu wa sheria hiyo faini ya utumikishaji wa watoto ni kiasi kisichopungua milioni tano na suala hilo kuachiwa mahakama kupanga kiasi kulingana na uzito wa kosa.Sheria hiyo inataka watoto kupewa kazi nyepesi zisizoweza kuathiri maumbile yao na makuzi.
Kila mwaka Juni 12 ni siku ya kimataifa ya kupambana na ajira dhidi ya watoto,kulingana na shirika la kazi Ulimwenguni (ILO) watoto milioni 215 wanafanyishwa kazi, nusu yao katika mazingira hatarishi.

Watoto hawa hufanyishwa kazi katika machimbo ya dhahabu, wanatupa taka kutoka katika majumba ya watu wengine, Watoto wanashindwa kusoma,kuandika na kuhesabu baadhi yao wanashindwa hata kuandika majina yao wala kusoma kitabu, hawapati fursa kabisa ya kucheza .

Utafiti kutoka shirika la kazi Duniani unaonyesha kuwa maelfu ya watoto wanatumikishwa katika kazi mbalimbali barani Afrika kwa mfano Zaidi ya watoto 500,000 wanafanyishwa kazi  hatarishi nchini Burkina Faso. 

Kulingana na ILO Karibu nusu wanafanyakazi  nchini Burkina faso katika takriban machimbo 600 ya dhahabu ni watoto. Mikono midogo ya watoto hao hutumika kuvunja vunja mawe ili kuweza kupata dhahabu. Miili midogo ya  watoto hao hutumika kupenya katika mashimo madogo ya machimbo ya dhahabu. 

Mapafu ya watoto hao huvuta hewa chafu ya kemikali zenye sumu  kemikali za asidi salfuriki huku malipo kwa watoto hawa yakiwa ni  shida kwani hupewa chakula tu.

 Mwandishi Köpp Dirke aliyefanya utafiti wa kutumikishwa watoto nchini Burkinafaso anasema katika maeneo ya machimbo watoto wanafanyishwa kazi muda wote isipokuwa mchana na kwamba hakuna Muda wa kisheria wa kufanyakazi katika Migodi wa dhahabu nchini Burkina Faso.

 Kulingana na mwandishi huyo shule nyingi katika eneo lenye machimbo ya dhahabu zina wanafunzi wachache. Watoto  hawana muda wa kwenda shule asilimia kubwa ni watoro.Hata hivyo Shirika la umoja wa mataifa ya kuwahudumia watoto (UNICEF) hat limefanikiwa kuwarejesha watoto 7,000 shule.
 Umoja wa Mataifa uliteua rasmi mwaka 1979, kuwa ni mwaka Kimataifa wa Mtoto. Hii ilifuatiwa na kupitishwa kwa Mkataba wa Kimataifa wa Haki za Mtoto mwaka 1989 na hatimaye mwaka 1990 mkataba ulianza kutekelezwa ukiwa kama sheria za kimataifa kuhusu haki za mtoto.
 Mkataba huo wa Umoja wa Mataifa juu ya haki za mtoto ulikuwa ni sheria ya kimataifa inayotaka kuzingatiwa kwa haki za watoto wote ulimwenguni hadi wanapokuwa wamefikia umri wa miaka18. Baadhi ya haki za mtoto ni kulindwa, kuendelezwa, kuishi, kupata elimu, chakula, malazi na huduma zingine muhimu kama matibabu.




No comments:

Post a Comment