![]() |
| Mwenyekiti wa serikali ya kijiji cha Likuyu Said Rupia |
Na
Albano Midelo
WANAWAKE
wajawazito katika kijiji cha
Likuyuseka wilayani Namtumbo mkoani Ruvuma wanadai wanadhalilishwa kupata
huduma ya uzazi katika zahanati ya kijiji hicho ambayo haina chumba maalum cha
kujifungulia.
Kijiji cha Likuyuseka kipo mpakani na mradi wa mgodi
wa uchimbaji wa madini ya urani uliopo ndani ya
pori la akiba la Selous ambalo lilitangazwa na shirika la umoja wa mataifa la UNESCO mwaka 1980 kuwa eneo hilo ni urithi wa Dunia.
pori la akiba la Selous ambalo lilitangazwa na shirika la umoja wa mataifa la UNESCO mwaka 1980 kuwa eneo hilo ni urithi wa Dunia.
Wakizungumza
na mwandishi wa makala hayo akinamama hao walisema zahanati hiyo Haina
chumba maalum kwa ajili ya kujifungulia hali ambayo imesababisha chumba cha kujifungulia wajawazito kuwa mkabala na chumba cha
wagonjwa wa kawaida hali ambayo
inawadhalilisha wanawake wanaojifungua.
“Kila kitu ambacho kinafanywa na muuguzi wakati
anamsaidia mama mjamzito kujifungua,wagonjwa wengine wanasikia,hali hii inatudharirisha
sisi wanawake,ilitakiwa ijengwe chumba maalum kwa ajili ya wazazi kujifungulia,wanawake wengine
wanaona aibu hawafiki hapa kujifungulia,wanajifungulia kwa wakunga wa jadi na
kuhatarisha maisha yao’’,alisema Fatuma Rajabu.
Hata hivyo hakuna utafiti ambao umefanyika kuzunguka
katika vitongoji vya kijiji hicho ili kubaini idadi ya wanawake walioamua
kujifungulia kwa wakunga wa jadi,lakini baadhi ya wanawake waliohojiwa wamedai
kuwa kuna wanawake hawaendi kujifungulia katika zahanati hiyo kutokana na kuona
aibu.
“Upande mmoja daktari anahudumia wagonjwa wa
kawaida,upande wa pili muuguzi mkunga anaangaika kumuhudumia mama mjamzito,
wagonjwa wengine wakiwepo watoto,vijana na wanaume wanasikia kila kitu,ni aibu sana kwa mama anayejifungua
ndiyo maana wengine hawaendi
kujifungulia hapo’’,alidai Mariam Rashid
Mwenyekiti wa kijiji cha Likuyuseka Athuman Rupia
amekiri zahanati ya kijiji hicho kukosa chumba maalum kwa ajili ya kujifungulia
akinamama wajawazito hali ambayo
imesababisha wajawazito kujifungulia sehemu ya chumba ambacho pia kinatoa
huduma kwa wagonjwa wa magonjwa mengine.
“Akinamama wajawazito wanapata shida wakati wa
kujifungua hali hiyo inaweza kuchangia kuongeza tatizo la uzazi usio salama kwa
kuwa kuna taarifa kuwa baadhi yao hawafiki kujifungulia katika zahanati hiyo
kwa sababu ya aibu,wagonjwa wengine wanawasikia unajua tena ndiyo maana
kunakuwa na wodi ya wazazi’’,alisema.
Katika kukabiliana na hali hiyo mwenyekiti huyo wa
serikali ya kijiji amesema mwaka huu kijiji kimefyatua tofali kwa ajili ya
ujenzi wa chumba cha kujifungulia wajawazito ili kuhakikisha kuwa tatizo hilo linapatiwa
ufumbuzi wa kudumu na kulinda hadhi ya mwanamke ambaye ni nguzo ya familia
katika jamii.
Kaimu afisa mtendaji wa kijiji hicho Maulid Kapolo
alisema licha ya kuwepo changamoto ya kutokuwepo chumba cha wazazi, tatizo la
vifo vya mama na mtoto lipo lakini sio kwa kiwango kikubwa kwa kuwa wataalamu
wa afya daktari na wauguzi wapo na
madawa yanapatikana katika zahanati hiyo
ambayo inahudumia watu zaidi ya 7000 .
Wilaya ya Namtumbo ina vituo 43 vya kutolea huduma
za afya. Kati ya hivyo, vituo vya afya ni sita,vinne vya serikali na viwili vya
shirika la dini, Zahanati 37 kati ya hizo zahanati 43 za serikali na zahanati tatu za taasisi za dini tatu..
Taarifa
ya idara ya afya ya Halmashauri ya wilaya ya Namtumbo imeyataja malengo makuu
ya uboreshaji wa huduma za afya kuwa ni kuongeza kiwango cha chanjo kwa watoto
chini ya miaka mitano kutoka asilimia 90 hadi 95 ifikapo 2015.Pia kupunguza
vifo vya watoto chini ya miaka mitano, vifo vya kinamama vinavyotokea wakati wa
kujifungua.
Katika
kutimiza malengo ya maendeleo ya milenia hususani lengo la tano la kupunguza vifo
vya wajawazito, takwimu za wizara ya afya zinaonyesha kuwa vifo vya wajawazito
vimepungua kwa asilimia 21 kutoka vifo 578 kwa kila vizazi hai Laki Moja
kati ya mwaka 2004/2005 hadi vifo 454 kwa kiwango hicho kati ya mwaka 2009/
2010.
Benedicto Ngaiza ni Mganga Mafawidhi
katika hospitali ya rufaa mkoani Ruvuma anaeleza mikakati ya
hospitali hiyo ni kuongeza juhudi katika kuisaidia Serikali ili kuzuia vifo vya
wanawake ambavyo hutokea wakati wa kujifungua.
Alisema
licha ya juhudi kufanywa na Serikali na wadau katika kupunguza vifo vya
akinamana, bado takwimu zinaonyesha kwamba kuna kazi kubwa ya kufanya. Na
kwamba inatakiwa kufanya kazi ya ziada
ili kuhakikisha wanawake wote wanajifungua salama bila kifo kutokea.
Alisema
kuzinduliwa kwa dawa hiyo ni silaha nyingine katika mapambano ya kumkomboa
mwanamke dhidi ya vifo vinavyotokea wakati wa kujifungua.
Wanawake 8,700 hufariki Dunia kila
mwaka nchini Tanzania kutokana na matatizo ya ujauzito na hasa wakati wa
kujifungua. Takwimu hizi zinaonesha takribani wanawake 24 hupoteza maisha kila
siku huku ikikadiriwa mmoja kufa kila baada ya saa moja.
Hata hivyo Sera ya afya ya mwaka 2007 inaeleza
mipango madhubuti ya kuhakikisha huduma bora za afya zinapatikana katika kila
kata ambapo kila kijiji kinatakiwa kuwe na Zahanati na kila kata iwe na kituo
cha afya na wataalamu wenye taaluma.
Vingi
kati ya vifo hivi vingeweza kuzuilika kama huduma za dharura zingekuwepo katika
Vituo vya Tiba wakati wa kujifungua. Huduma zenyewe ni kama vile chumba cha
upasuaji na wataalamu wake, vifaa tiba na uwezekano wa kuongezewa damu.
“Si
sahihi mama mjamzito kufa wakati wa kujifungua au kupoteza uhai wake kwa kuleta
kiumbe kingine duniani, hii haiwezi kukubalika. Na inasikitisha zaidi pale
maisha ya mama huyu yanapotea hata kwa mambo ambayo yanaweza kuzuilika,”
anasema Rais Kikwete katika hotuba yake mbele ya Katibu Mkuu wa Umoja wa
Mataifa, Ban Ki-moon.
Sera ya afya inaeleza wazi kuwa serikali kwa kushirikiana na wananchi
na wadau wengine yakiwemo mashirika mbalimbali itahakikisha inaboresha huduma
za afya ili ziwe na mazingira mazuri na vifaa tiba. Hata hivyo sera hiyo
inakwenda kinyume na hali halisi unapofika kwenye vituo vya kutolea huduma za
afya hasa vijijini mazingira sio rafiki.
Mazingira ya zahanati ya kijiji cha
Likuyuseka yanafanana na mazingira mabovu ya kutolea huduma ya mama na mtoto
katika baadhi ya zahanati, vituo vya afya, hospitali za wilaya, mikoa na hata
hospitali za rufaa katika nchi nzima.
Kwa mujibu wa utafiti wa masuala ya
afya ya uzazi ya Kitaifa wa serikali mwaka 2010 (TDHS) kila siku wajawazito 23
wanapoteza maisha kwa matatizo mbalimbali ya uzazi wakati wa kujifungua na
baada ya kujifungua.
Serikali imeweka malengo ya Milenia kufikia vifo 54 kwa kila vizazi hai 1,000
ifikapo mwaka 2015,Utafiti umebaini licha ya malengo hayo ambayo yamebakiza
miezi tu, wanawake 906 wamefariki dunia kwa matatizo ya uzazi mkoani Mbeya
mwaka 2012.
Baadhi ya sababu ambazo zinasababisha vifo
vitokanavyo na uzazi kuwa ni pamoja na ugonjwa wa Malaria, damu kupungua kwa
mama mjamzito, kutokwa kwa damu nyingi wakati wa kujifungua, uambukizi wa homa
kali, huduma hafifu, VVU na kifafa cha Mimba.
Changamoto kubwa kwa serikali ni
pamoja na kutoa elimu ya kutosha kwa jamii kutambua umuhimu wa kujifungulia
katika vituo vya afya na zahanati ili kuondokana na changamoto mbalimbali
zinazoweza kujitokeza wakati wa kujifungua uzazi salama.
Huko nchini Uganda wanaharakati wa
kutetea haki za wajawazito wanaitaka mahakama ya kikatiba itangaze kuwa mama
kufariki akijifungua ni ukikwaji wa haki zake.
Kwa
mujibu wa takwimu za wizara ya afya nchini Uganda, takriban wanawake 16
hufariki kila siku wakijifungua, nchini Uganda. Kutokana na hali hiyo wanawake
wakiongozwa na wanaharakati 100 wa
kutetea haki za akinamama wajawazito walifanya maandamano ya amani na kutembea
kilomita tano kutoka ofisini kwao hadi kwenye mahakama ya katiba.
"Tunataitaka serikali itangaze kuwa akinamama
wajawazito kufariki wakiwa hospitalini ni ukiukwaji wa haki zao za kuishi na
afya bora. Pili, tuliwasilisha malalamiko yetu kwenye mahakama ya kikatiba
miezi saba iliopita na kufikia sasa hatujapata jibu lolote. Tunaiomba mahakama itoe msimamo kuhusu suala hilo’’,anasema
Nakibuuka Nuru mwanaharakati wa kutetea haki za binadamu nchini Uganda.
Wanaharakati
wa kutetea haki za akinamama wajawazito wanaitaka serikali nchini Uganda
kuwaajiri wakunga na madaktari wa kuwahudumia
wajawazito na kwamba kesi nyingi za wajawazito wanaofariki ni kwa sababu
hawakupata usaidizi unaofaa kwa wakati unaofaa kutokana na takwimu kuonyesha
kuwa mkunga mmoja nchini Uganda anahudumia hadi wajawazito 50 kwa siku..
Ingawa
sheria nchini Uganda kama vile Tanzania
inasema mama mjamzito akienda kwenye hospitali ya serikali anatakiwa kupata huduma za bure wakati wa
kujifungua hali ni tofauti kwa kuwa akinamama hulazimishwa kununua vifaa vya
kujifungulia kama vile pamba, wembe na vinginevyo.
Wakati
hayo yanajiri nchini Uganda ,Takwimu za shirika la afya Duniani WHO, zinaonyesha
kuwa idadi ya vifo vya kimamama vimepungua duniani kutoka nusu milioni mwaka
1980 hadi chini ya vifo 350,000 mwaka 2008.
Kwa mujibu wa uchunguzi ulioshapishwa na
jarida la The Lacent, idadi ya kinamama wanaofariki dunia kutokana na matatizo
ya ujauzito imepungua kwa zaidi ya asilimia 35, katika kipindi cha miaka 30
iliyopita. Nchi kama vile China, Misri, Ecuador na Bolivia zimefanikiwa kufikia
malengo ya kimataifa ya kupunguza idadi ya wanawake wanaofariki dunia kutokana
na matatizo ya ujauzito,
Hata hivyo nchi za
Marekani na Norway zikiripotiwa kushuhudia ongezeko la vifo hivyo. Wengi
wanasema kwamba, sababu kuu inayosababisha ongezeko la vifo hivyo katika nchi
hizo mbili ambazo ni tajiri na zenye huduma bora ya tiba ni kuongezeka magonjwa
miongoni mwa kinamama wajawazito pamoja na kinamama kubeba mimba katika umri
mkubwa.
albano.midelo@gmail.com,simu
0784765917

No comments:
Post a Comment