Sunday, April 24, 2016

Hakuna sababu ya Tanzania kuendelea kuwa nchi masikini



Na Albano Midelo

Ukuaji wa kiuchumi nchini Tanzania, taifa la tatu kwa kuzalisha dhahabu katika bara la Afrika, ulifikia asilimia saba kwa mwaka tangu mwaka 2001.


Inadaiwa katika kipindi cha miaka kumi wa utawala wa Rais wa awamu ya nne ukuaji wa uchumi wa Tanzania uliendelea kusimama kwa asilimia saba huku nchi ikiwa na rasilimali lukuki na ukuaji huo wa uchumi ukionekana zaidi kwenye makaratasi huku wananchi kila kona ya nchi wakilia na umaskini na ufukara unaoendelea kwa kasi.

Tanzania inabakia kuwa moja ya mataifa maskini duniani. Ripoti ya Maendeleo ya Umoja wa Mataifa, ambayo inapima kiwango cha maendeleo kwa kutumia vigezo vya kijamii na kiuchumi, inaiweka Tanzania nafasi ya 159 kati ya mataifa 177.

Watanzania wengi waliopo vijijini na mijini ni maskini zaidi wamekuwa na mabadiliko madogo au hawajaona kabisa mabadiliko ya ubora wa maisha yao licha ya serikali kudai inafanya vizuri kukuza uchumi wa Tanzania na kwamba mataifa makubwa eti yaliridhika na kasi ya ukuaji wa Tanzania katika serikali ya awamu ya nne iliyoongozwa na Rais mstaafu Jakaya Kikwete.

Kutokana na umaskini unaendelea na kuwakabili wananchi wengi Tanzania ni miongoni mwa nchi ambazo zimeshindwa kutimiza Malengo manane ya Maendeleo ya Milenia (MDGs) ambayo mwisho wake ulikuwa ni mwaka 2015.

Wataalam wa uchumi wa kimataifa wanasemaTanzania itahitaji miongo kadhaa ya ukuaji wa kiuchumi kusaidia kuwaondoa watu wake katika ufukara na kutoa huduma muhimu za msingi kama vile maji,huduma za afya,barabara na umeme.  

Utafiti umebaini kuwa ni  watanzania wachache wenye uwezo wa kupata huduma za msingi ambapo hivi sasa katika maeneo yote mijini na vijijini wanakosa huduma muhimu kama maji na vituo vya kutolea huduma za afya jambo ambalo ni hatari.

Wakati taarifa za ukuaji wa uchumi  kwenye makaratasi zikionesha uchumi wa Tanzania unakua kwa asilimia saba kwa kipindi cha miaka kumi iliyopita ya Rais wa awamu ya nne Jakaya Kikwete, bado mamilioni ya Watanzania wanaishi katika lindi la umaskini,baadhi yao wanapata mlo mmoja kwa siku.

 Nchi zinazotajwa kuwa tajiri kama Malaysia,Taiwan na Singapore, zilikuwa kundi moja na  Tanzania katika kundi la nchi maskini sana duniani wakati tunapata uhuru mwaka 1961.Jambo la kusikitisha nchi hizo hazina maliasili nyingi kama zilizopo Tanzania hali ambayo nchi zinazotuzunguka kama Rwanda zinashangaa kwanini nchi yenye rasilimali nyingi kama Tanzania inaendelea kuwa masikini badala ya kuwa nchi tajiri.


Bila shaka nchi imeshindwa kusonga mbele kwa miaka mingi kutokana na vitendo vya rushwa na ufisadi pamoja na sheria mbovu zinazosababisha nchi inashindwa kukusanya kodi ambazo serikali inastahili kuzipata.



Tunaamini hatua za dhati ambazo zimeanza kuchukuliwa na uongozi wa serikali ya awamu ya tano zinaweza kusaidia kuirudisha nchi katika njia yake hatimaye nchi inaweza kupaa kiuchumi na kuwa miongoni mwa nchi zenye uchumi wa kati Duniani hata kabla ya mwaka 2025.




Tanzania imeeendelea kuhesabika kuwa miongoni mwa nchi maskini kabisa duniani,huku pengo kubwa la watu masikini na matajiri likiongezeka kwa kasi ya kutisha jambo ambalo linaleta chuki kwa wananchi masikini ambao wanawaona watanzania wachache waliopewa dhamana kubwa serikalini wakiwemo wabunge wakiishi katika maisha ya anasa.

Idadi kubwa ya watanzania hawana uhakika wa kupata walau mlo mmoja wa siku,watu wanaishi katika nyumba zilizojengwa kwa tope na kuezekwa kwa nyasi,watu hawana maji ya kunywa ,wanatumia vibatali na mishumaa,watu wanalaa kwenye mkeka kwa ujumla maisha ya watanzania yapo enzi za ujima.

 Watumishi wa ngazi ya chini serikalini wakiwemo walimu,polisi na wauguzi kutokana na kulipwa mishahara midogo ambayo haikidhi hata wiki moja hivi sasa wanakabiliwa na madeni makubwa kutokana na kukopa huku baadhi yao wakiwa hawana mshahara kutokana na madeni hivyo wamekata tamaa ya kufanyakazi.

Wakulima licha ya kulima kwa shida kununua pembejeo za kilimo kwa gharama kubwa bado serikali inawakopa mazao wanayolima na kuongeza ugumu wa maisha.

Rais Magufuli amekuwa anasema Tanzania ni nchi tajiri sana ina rasilimali lukuki na adimu,walioifikisha hapo Tanzania ni mafisadi ambao wameiba fedha za serikali nyingine wamekwenda kuzificha nje ya nchi,wamefuta azimio la Arusha ambalo lilikuwa linawabana kwa kuwa mtumishi wa umma alikuwa haruhusiwi kujilimbikizia mali.

Hatua ambazo zinachukuliwa na Rais Dk.Magufuli za kupambana na ufisadi wa kuhakikisha kuwa vigogo wote serikalini bila kujali wadhifa wake ambao wameiba mali za umma wafilisiwe na kuchukuliwa hatua za kisheria chini ya mahakama ya mafisadi ambayo imeahidiwa kuundwa na serikali ya awamu ya tano ili mali hizo zirudishwe serikalini na kutumika kwa manufaa ya watanzania wote.

Tayari ndani ya siku 100 za utawala wake Rais Magufuli amekusanya karibu shilingi trilioni tatu,ameokoa shilingi bilioni saba ambazo zingetumika kwa safari za nje za vigogo serikalini na anaendelea kupambana na wafanyabiashara wakwepa kulipa kodi na watumishi wazembe.

Pia mfumo wa upendelea serikalini ubadilishwe ambapo mianya yote ya kujinufaisha vigogo serikalini ifutwe,sheria ya manunuzi serikalini ibadilishwe,posho za kujipendelea kwa vigogo wakiwemo wabunge zifutwe badala yake mabilioni hayo yatumika kwa manufaa ya watanzania wote na sio watu wachache wanafaidi keki ya Taifa huku wengine wakipiga miayo kwa njaa.

Hayo yakifanyika Tanzania yenye neema sawa kwa kila mtanzania inawezekana,kwa kuwa sasa kila mmoja atanufaika na rasilimali za Taifa badala ya hali inayoendelea sasa imejenga mafukara wengi huku watu wachache mabilionea wakitanua na kufanya kila wanachotaka kutokana na nguvu ya fedha walionayo.



No comments:

Post a Comment