Sunday, April 24, 2016

Upungufu wa madaktari unavyozorotesha afya kwa watanzania



Na Albano Midelo

Uchumi endelevu hauwezi kujengwa na Taifa lenye watu wagonjwa,kwa kuwa watatumia muda mwingi kulala bila kuzalisha mali hali ambayo itachangia kuongezeka kwa umaskini.


Watanzania wengi wanakabiliwa na adui maradhi yanayosababisha kuugua magonjwa mbalimbali na kupoteza maisha kila mwaka kutokana na kuwepo kwa idadi  ndogo ya madaktari ambao hawakidhi idadi ya watanzania wanaofikia milioni 45.


Shirika la afya Duniani WHO linaitaja Tanzania kuwa miongoni mwa nchi zenye madaktari wachache sana ambapo uwiano wa daktari mmoja ni kuhudumia wagonjwa 30,000,wakati WHO inapendekeza daktari mmoja kuhudumia wagonjwa 1000.

Takwimu zinaonesha kuwa katika nchi nzima kuna madaktari wasiozidi 2000 kati ya hao asilimia 32 tu wanafanyakazi katika jiji la Dar es salaam,asilimia tisa wanafanyakazi katika mikoa ya Mbeya,Arusha,Mwanza na Kilimanjaro,asilimia 19 wanafanyakazi katika mikoa mingine ya Tanzania na asilimia 40 ya madaktari hao hawafanyi kabisa kazi ya utabibu licha ya kuwa na taaluma ya utabibu.

Kutokana na takwimu hizo asilimia 80 ya watanzania hawana madaktari, kwa hiyo kuna idadi kubwa ya watanzania hasa katika maeneo ya vijijini ambao wanaugua magonjwa mbalimbali na wengine wanapoteza maisha kwa sababu ya kukosa huduma ya utabibu hali hiyo inachangia kuzorotesha uchumi kwa kuwa kuna nguvukazi kubwa inapotea au kuugua na kushindwa kufanyakazi.

Hali hiyo ndiyo iliyolisukuma Baraza la Maaskofu Tanzania kuanzisha shahada ya kwanza ya udaktari katika chuo kikuu kishiriki cha SAUT tawi la Songea ambacho kinajulikana kwa jina la Archbishop James University College (AJUCO) kampasi ya udaktari Peramiho jimbo kuu katoliki la Songea.

Kutokana na changamoto kubwa ya madaktari nchini hasa vijijini chuo cha AJUCO kupitia kampasi yake ya udaktari Peramiho  inaandaa mfumo maalum wa madaktari watakaohitimu kufanyakazi vijijini ambako kuna idadi kubwa ya watanzania wanaokosa huduma ya utabibu.

Mfumo wa kuwaandaa madaktari kupenda kufanyakazi vijijini umefanikiwa katika nchi za Canada na Brazil  na kwamba AJUCO ina matarajio makubwa ya kufanikisha mfumo huo  katika kozi ya madaktari ambayo ilianza mwaka juzi ikiwa na na jumla ya wanafunzi 257 kozi hiyo itachukua miaka mitano.

Kwa mujibu wa Shirika la Afya Duniani (WHO), Tanzania inatumia kati ya dola za kimarekani 40,000 hadi 60,000 kusomesha daktari mmoja ambapo inakadiriwa madaktari wanne kati ya kumi wanaomaliza elimu ya utabibu wanaacha fani ya utabibu muda mfupi baada ya kuhitimu masomo yao.

Utafiti unaonesha kuwa katika mikoa ya pembezoni kama Kigoma daktari mmoja anahudumia watu 308,000,Mara watu 167,000, Tabora daktari mmoja anahudumia watu 132,000,Pwani watu 32,000,Arusha watu 22,000 na jiji la Dare s salaam watu 24,000.

Ripoti hiyo inaongeza kuwa pamoja na eneo la kusini mwa Jangwa la Sahara kubeba asilimia 24 ya mzigo wa magonjwa duniani, kuna asilimia tatu tu ya nguvukazi katika sekta ya afya na asilimia moja tu ya rasilimali fedha duniani. 

Hata hivyo kitendo cha chuo kikuu kishiriki cha SAUT kampasi ya udaktari Peramiho kuanzisha mfumo maalum wa kuwaandaa madaktari kufanya kazi vijijini huenda kutasaidia kukabiliana na tatizo la uhaba mkubwa wa madaktari hasa katika maeneo ya vijijini.

Chama cha Madaktari Tanzania (MAT), kwa kushirikiana na shirika lisilo la kiserikali la SIKIKA, vimefanya utafiti ambao umeonyesha kwamba asilimia 39.6 ya madaktari nchini hawafanyi kazi ya kutoa huduma za kitabibu wala za kiutawala katika Sekta ya Afya, badala yake wanafanya shughuli nyingine tofauti kabisa na fani ya utabibu.

Utafiti huo ulioshirikisha madaktari 2,246 waliohitimu shahada zao nchini, unabainisha  kuwa  madaktari 890 kati ya 2,246 sawa na asilimia 39.6 ya wataalamu hao wa utabibu nchini hawafanyi kazi ya kitabibu licha ya kusomea hali ambayo inazorotesha sekta hiyo muhimu kwa uhai wa binadamu na maendeleo ya uchumi.

 Kulingana na matokeo ya utafiti huo ni madaktari 964 tu kati ya 2,246 ndio wanaofanya kazi katika hospitali na vituo vya huduma za afya hapa nchini wengi wao wakifanya kazi katika majiji na miji mikubwa na kwamba kuna madaktari 184 wa kitanzania ambao wanafanyakazi nje ya nchi.

 Hata hivyo kuna sababu nyingi ambazo zinatajwa na madaktari hao zinazowasukuma kuacha kufanyakazi waliosomea au wengine kukimbilia maeneo ya mijini au nje ya nchi zikiwemo za uhaba wa vitendeakazi,nyumba bora za kuishi,mishahara ambayo hailingani na ugumu wa kazi,posho na masilahi mengine.

albano.midelo@gmail.com

No comments:

Post a Comment