Monday, April 25, 2016

Wizara ya elimu ibadilishe tafsiri ya elimu ya vyeti kuwa elimu vitendo



Na Albano Midelo
Awali ya yote nampongeza Rais wa Jamuhuri ya Muuungano wa Tanzania katika serikali ya awamu ya tano  Dk.John Magufuli kwa kumteua profesa Joyce Ndalichako kuwa waziri wa Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi.


Nionavyo mimi Rais Magufuli hajafanya makosa kumchagua profesa Ndalichako kutokana na uwezo mkubwa ambao anao katika sekta ya elimu na hasa pale alipokuwa katibu mtendaji wa Baraza la  mitihani(NECTA) alifanyakazi nzuri ambayo iliungwa mkono na wadau wengi wa elimu nchini.


Nionavyo mimi profesa Ndalichako anaweza kuisimamia wizara ya elimu kwa ufanisi mkubwa na kupatia ufumbuzi wa changamoto mbalimbali zinazoikabili wizara hiyo kwa muda mrefu huku wadau wengi wakiinyoshea wizara ya elimu kuchangia kushusha kiwango cha elimu nchini.

Profesa Ndalichako tangu alipoteuliwa na Rais Magufuli kuwa waziri wa elimu na hata kabla ya kuteuliwa nafasi hiyo amekaririwa mara kadhaa katika vyombo vya habari akisisitiza kubadili tafsiri ya ya elimu ya vyeti ambayo inafanyika hapa nchini badala yake elimu ambayo inatakiwa sasa kuwekewa mkazo mkubwa ni elimu ya vitendo na uelewa ambayo itajenga stadi muhimu kwa wahitimu wetu katika ngazi mbalimbali za elimu nchini.

Nakubaliana na waziri wa elimu kwamba wahitimu wengi katika vyuo mbalimbali ni wa vyeti  kwa sababu mtu anaweza kupata alama za juu katika cheti chake lakini katika hali halisi mhitimu huyo kichwani hana uelewa kwa kile ambacho amesomea hivyo kushindwa kuitumia kwa vitendo elimu ambayo ameipata iwe katika chuo kikuu au vyuo vingine.

Nionavyo mimi profesa Ndalichako akipewa ushirikiano na wataalam wa elimu nchini anaweza kujenga ya ubora wa elimu nchini kwa kuhakikisha kuwa changamoto zote zinazosababisha kushuka kwa elimu kupatiwa ufumbuzi wa kudumu.

Nionavyo mimi mfumo mzima wa elimu ya Tanzania unatakiwa kubadilishwa kutoka elimu ya vyeti na kuwa elimu ya vitendo kwa kuhakikisha wanafunzi wetu wanapatiwa ujuzi na stadi muhimu za maisha ili kushindana na soko la ajira katika nchi nyingine ambazo mfumo wao wa elimu ni wa vitendo na si vyeti.

Hata hivyo nionavyo mimi waziri wa elimu anatakiwa pia kushughulikia changamoto mbalimbali zinazowakabili walimu ambao ndiyo wadau muhimu katika sekta ya elimu kwa kuwa wao wanawajibika moja kwa moja kutoa elimu kwa wanafunzi katika ngazi mbalimbali.

Mfumo wa elimu ya Tanzania  kuanzia shule za awali hadi elimu ya chuo kikuu unasababisha kupata wahitimu kila mwaka ambao hawana maarifa na ujuzi ambao utawawezesha kujiajiri wenyewe.

Wahitimu wetu katika vyuo vikuu walio wengi kutokana na mfumo mbovu wa elimu uliopo,umewafanya waamini kuwa kupata cheti chenye alama ya juu ndiyo muhimu zaidi bila kujali kupata ujuzi na maarifa ambayo yatakuwezesha kujiajiri mwenyewe na kuajiri wengine.

Mfumo mbovu wa elimu uliopo Tanzania ndiyo unasababisha watanzania kushindwa katika soko la ajira la kimataifa kwa kuwa unaposhindana na wananchi wanaotoka katika nchi zenye mfumo mzuri wa elimu ambao unazingatia maarifa na vitendo hauwezi kushindana nao .

Nionavyo mimi watanzania wanatakiwa kujifunza katika nchi ambazo mfumo wao wa elimu ni imara hauyumbishwi na wanasiasa.Kuna baadhi ya nchi wataalam wa elimu ndiyo wameachiwa kusimamia elimu kulingana na sera na sheria katika nchi zao.

Nionavyo mimi elimu ya Tanzania sio imara ukilinganisha na nchi nyingine ndiyo maana hadi sasa kwa mfano ukiangalia hakuna kitabu cha somo moja ambacho kinaweza kutumika katika nchi nzima kwa shule za msingi hali ambayo inasababisha kila shule  kuamua kutumia kitabu chake wakati wanafunzi wote wanafanya mtihani wa Taifa mmoja.

Maendeleo ni vita

No comments:

Post a Comment