Wednesday, April 27, 2016

Jiwe la Pomonda ziwa Nyasa ni zaidi ya jiwe la ziwa Viktoria



Na Albano Midelo

Inakuzalazimu kusafiri zaidi ya kilometa 170 kutoka Songea makao makuu ya mkoa wa Ruvuma hadi kulifikia jiwe la kihistoria la Pomonda lenye ukubwa wa nusu hekari ambalo lipo meta takribani 300 ndani ya ziwa Nyasa  kutoka bandari ya Liuli.
Wajerumani walilipa jina la Pomonda jina la sphinxhaven kutokana na kuwa na vivutio vya utalii lukuki.
Utalii wa kihistoria ni aina ya kwanza ya utalii ambayo inapatikana katika jiwe hilo ambapo tangu vita vya kwanza vya dunia mwaka 1914 hadi 1918 pamoja na vita vya pili vya dunia mwaka 1939 hadi 1945  wakoloni wa kijerumani na wakiingereza walitumia pango kubwa lililopo katika jiwe hilo kama sehemu ya kujificha wakati wa  mapambano.
 Jiwe la Pomonda linaweza kuhifadhi watu kati ya 200 hadi 250 ambapo kilele chake kina urefu wa takribani meta 40 kwenda juu ipo taa maalum  kubwa yenye rangi nyekundu ambayo ilikuwa itatumiwa  na nchi tatu za Tanzania,Malawi na Msumbuji wakati wa wakoloni wa kijerumani,kireno na waingereza kwa ajili ya alama ya kuongozea meli katika ziwa Nyasa ili wasiweze kupotea  wanapotaka kutia nanga kwenye bandari ya Liuli,taa hiyo iliwawezesha kuiona bandari ya Liuli  hata wakiwa katika nchi za Malawi na Msumbiji.

 

Kivutio kingine cha utalii ambacho kinapatikana katika eneo la jiwe hilo ni mawe matatu makubwa ambayo wakazi wa eneo hilo wanaamini yamepangwa na mwenyezi Mungu ,huku mpangilio wake ukiwa ni kivutio cha ajabu utadhani yamejengwa na mafundi ujenzi huku yakiwa yameacha njia maalum ambayo unaweza kupita kutokea upande wa pili hali ambayo inawashangaza na kuwavutia wengi.



 Jiwe la kihistoria la Pomonda pia ni sehemu muhimu ambayo inafaa kufanya utalii wa kupiga mbizi  pamoja kuwepo utalii wa  kuruka toka juu ya jiwe la Pomonda hadi ziwani umbali  wa karibu mita 30 hali ambayo inawavutia watalii wengi wa ndani na wa kutoka nje ya nchi kwenda mara kwa mara katika jiwe hilo na kujisikie kana kwamba wapo katika nchi zao ambazo zina maeneo  ambayo wameyatengeneza tofauti na eneo hilo la jiwe la Pomonda ambalo ni la asili.



Katika eneo lote linalozunguka jiwe la Pomonda  kuna aina zaidi ya 150 wa samaki wa mapambo hivyo mtalii akifika katika jiwe hilo kuna eneo maalumu ambalo anaweza kufanya utalii wa  kuvua samaki hao yeye mwenyewe pia anaweza kupika au kupikiwa ugali wa asili wa mhogo  ambao ni chakula maalum kwa wakazi wa mwambao mwa ziwa Nyasa.



Hata hivyo uchunguzi umebaini kuwa kuna makampuni ambayo wanaendelea kuwavua samaki hao wa mapambo katika eneo hilo kama shamba la bibi  na kwenda kuwauza Ulaya na Marekani kwa bei kubwa huku  wenyeji wa kata ya Liuli na maeneo mengine ambako samaki hao wanavuliwa wakibakia mikono mitupu pia serikali inapoteza ushuru halali wa kodi ya samaki hao ambao inakadiriwa wanauzwa ulaya kwa bei ya kati ya shilingi za kitanzania 80,000 hadi 100,000 kwa samaki mmoja.



Jiwe la Pomonda  ni eneo ambalo linafaa kwa ajili ya kufanyia picnic kwa kuwa lina ukumbi mkubwa ambao umefunikwa vizuri kwa mawe na mwenyezi Mungu tangu kuumbwa kwa dunia hata wakati wa mvua mtalii anaweza kukaa na kuwa salama,pia kuna eneo maalum ambalo linafaa kwa kupigia picha huku mtalii akipata upepo mwananana wa ziwa Nyasa pamoja na kufanya utalii wa kuzunguka maeneo yote ya jiwe hilo kwa kutumia boti maalum.



Martin Ndomba kutoka kikundi cha Ntembo Tours  Liuli anashauri watalaamu kutoka wizara ya utalii na maliasili kutembelea katika jiwe la kihistoria la Pomonda ili kufanya utafiti zaidi na kubaini vivutio vingine zaidi na hata umri wa jiwe hilo ambalo linafanana na lile lililopo ziwa Viktoria.



 Serikali mkoani Ruvuma  imesema vivutio vya utalii ambavyo vimetambuliwa katika mwambao mwa ziwa Nyasa vitaingizwa kuwa miongoni mwa vivutio vya utalii vilivyopo katika mkoa wa Ruvuma pamoja na kuviendeleza ili hatimaye wananchi na serikali waanze kunufaika na vivutio hivyo ambavyo vitafungua milango ya utalii katika ukanda wa kusini.



Mbunge wa jimbo la Nyasa ambaye pia ni mjumbe wa Bodi ya utalii katika mkoa wa Ruvuma na Naibu waziri wa Elimu,Sayansi,Teknolojia na ufundi Injinia Stella Manyanya anasema matangazo ya vivutio mbalimbali vya utalii  katika vyombo mbalimbali vikiwemo vya ndani ya nchi na vyombo vya kimataifa yatawezesha vivutio hivyo kufahamika kitaifa na kimataifa hivyo idadi ya watalii kuendelea kuongezeka mwaka  hadi mwaka na kuliingizia taifa mapato makubwa.



 Injinia Manyanya anasema tafiti zinaonesha kuwa ni watanzania wachache  ambao wanaonekana kuwa na tabia ya kutembelea vivutio mbalimbali vya utalii vilivyopo nchini,mbali ya wanafunzi wa shule za msingi,sekondari na vyuo bado watu wengi hawajaonesha kipaumbele katika sekta ya utalii.



 Hata hivyo anasisitiza elimu sahihi kuhusu utalii itawezesha kujenga  mazoea ya kutembelea vivutio hivyo na hatimaye kuifanya sekta ya utalii  katika mikoa ya kusini kusimama kwa miguu miwili huku ikipata uwezo wa kutimiza malengo yake hata bila ya kutumia nguvu kubwa ya kujitangaza.



Anasema mkoa wa Ruvuma umebahatika kuwa na ziwa Nyasa wilayani  ambako unaweza kufanya utalii wa aina mbalimbali kama vile fukwe za ziwa,samaki wa mapambo wanaopatikana katika ziwa  pamoja na ngoma za asili na vyakula vya jadi ambavyo kinaweza kuwa kivutio cha kipekee katika utalii .




Manyanya anabainisha zaidi kuwa  licha ya kuwepo utalii wa kuona wanyama au mambo ya kale, katika mkoa wa Ruvuma kuna utalii wa ngoma za asili na kwamba mkoa wa Ruvuma una utajiri mkubwa wa ngoma hivyo kuna fursa ya kuutangaza utalii wa ngoma na amezitaja baadhi ya ngoma hizo kuwa ni lizombe,kioda,kitoto,mganda,ligihu pamoja na aina nyingine nyingi za ngoma za jadi.



 Ngwatura Ndunguru ni mbunge mstaafu wa jimbo la Mbinga magharibi na afisa maliasili na utalii mstaafu anabainisha kuwa Moja ya mambo ambayo yanaweza kuwa ni matunda ya sekta ya utalii katika ukanda wa kusini ni uboreshaji wa miundombinu hususani ya mawasiliano ya barabara

,usafiri,hoteli za kisasa ili kukidhi matakwa ya wageni wanaofika kusini kwa shughuli za kitalii.



Mataifa mengi duniani hivi sasa yanatoka kwenye utalii wa kutegemea mbuga za wanyamapori na kuingia kwenye utalii wa mambo ya kale,ngoma,hadithi na simulizi za kale hivyo fursa za utalii katika mkoa wa Ruvuma ni nyingi na zikiibuliwa,zikiendelezwa na kutangazwa mkoa unaweza kupiga hatua kubwa katika utalii.



albano.midelo@gmail.com








No comments:

Post a Comment