Sunday, May 1, 2016

Watumishi wanne Nyasa watumbuliwa majipu

Na Kwirinus Mapunda,Mbambabay


BARAZA la madiwani katika Halmashauri ya wilaya ya Nyasa mkoani Ruvuma limewatumbua majipu watumishi wanne  akiwemo afisa utumishi mkuu kutokana na makosa mbalimbali ya kiutumishi.
Mwenyekiti wa Halmashauri ya wilaya ya Nyasa Alto Komba

Watumishi waliotumbuliwa majipu katika kikao cha Baraza la madiwani ya Halmashauri hiyo kilichofanyika kwenye ukumbi wa Bay live mjini Mbambabay ni pamoja na Ephrem Kawonga aliyekuwa afisa utumishi mkuu ambaye sasa
ameshushwa cheo baada ya kutuhumiwa kuhujumu mfumo wa utumishi.

Watumishi wengine waliotumbuliwa ni pamoja na aliyekuwa afisa mifugo wa Halmashauri hiyo Kalistus Kisela ambaye amefukuzwa kazi kutokana na kutumia vyeti  feki pamoja na watumishi wawili kutoka idara ya afya ambao ni Pawabu Shaban na Selastine Haule ambao hawakuwepo katika kituo cha kazi kwa muda mrefu.

Katika kikao hicho cha Baraza la madiwani  kimeridhia  taarifa ya mapendekezo ya majina ya watumishi 159 kwa katibu wa Tume ya utumishi wa walimu ya Februari mosi,2016 pamoja na majina 42 ya watumishi wasiokuwa walimu ambapo wamejadili na kukubali watumishi hao kupandishwa vyeo.

Katika hatua nyingine Baraza hilo  limethibitisha wakuu wa idara sita walioteuliwa Septemba 2015,kuwa wakuu wa idara kamili baada ya kuridhishwa na utendaji wao wa kazi kwa mujibu wa masharti ya barua zao za uteuzi.

Mapendekezo ya kuwathibitisha katika vyeo hivyo ni kwa mujibu wa sheria ya utumishi wa umma namba nane ya mwaka 2002 ambayo imefanyiwa marekebisho kwa sheria namba 18 ya mwaka 2007 na kanuni zake za mwaka 2003.

Kikao hicho cha Baraza la madiwani katika Halmashauri ya Nyasa kilihudhuriwa madiwani 27,wakuu wa idara,wataalam mbalimbali pamoja na mbunge wa jimbo la Nyasa ambaye pia ni Naibu waziri wa Elimu,Sayansi,Teknolojia na mafunzo ya ufundi Injinia Stella Manyanya.
mapundakwirinus@yahoo.com

No comments:

Post a Comment