Na Kwirinus Mapunda
Katika hali isiyokuwa
ya kawaida diwani wa kata ya Linga
wilayani Nyasa mkoani Ruvuma Edmund Magendo ameamua kuanza kuwalipa posho ya
kila mwezi wenyeviti wa vijiji vilivyopo katika kata yake.
![]() |
| Diwani wa kata ya Linga Edmund Magendo kushoto |
Akizungumza na
mwandishi wa habari hizo mjini hapa diwani huyo kijana amesema ameamua kuwalipa
posho kila mwezi kwa kutambua mchango wa maendeleo kwa wenyeviti wa vijiji
katika kata yake hivyo ili kuwatia moyo ameamua kuanza kuwalipa posho viongozi
wa vijiji vitatu vya Ngingama,Litumbakuhamba na Lukali vinavyounda kata mpya ya
Linga ambayo imemegwa kutoka kata ya Lituhi.
Diwani huyo pia
amewalipia kadi za mfuko wa afya ya jamii CHF kwa wenyeviti wote wa
vitongoji 12 vilivyopo katika kata hiyo
ili waweze kupata huduma za afya kwa
urahisi wao na familia zao hali ambayo itawaongezea motisha ya kufanyakazi
zaidi ili kwenda sanjari ya kauli mbiu ya Rais ya hapa kazi tu.
“Kwa mwaka kila
mwenyekiti wa kijiji atapata fedha ya posho zisizozidi laki moja na nusu hivyo
katika bajeti yangu kwa mwaka nimetenga karibu shilingi laki tano kwa ajili ya
posho kwa wenyeviti wangu watatu wa vijiji,nawalipa kila baada ya miezi
mitatu,sina uwezo mkubwa natarajia kuwalipa katika kipindi changu chote cha
miaka mitano ya udiwani’’,alisisitiza.
Kutokana na serikali kutokuwa na bajeti ya kuwalipa posho wenyeviti
wa mitaa,vijiji na vitongoji,diwani huyo kwa tiketi ya Chama Cha Mapinduzi
ametoa wito kwa Rais John Magufuli kuangalia uwezekano wa kuanza kuwalipa posho
wenyeviti hao kama zinavyotolewa kwa madiwani kwa kuwa viongozi hao ni msingi
wa kuchochea na kuhamasisha maendeleo kuanzia ngazi ya chini.
Mwanasheria mahiri
nchini Dk.Nshala Rugemeleza alisema katika sheria ya ardhi ya mwaka 1999
inaonesha kuwa asilimia 70 ya ardhi ipo
chini ya serikali ya kijiji hivyo
serikali ya kijiji ina nguvu ya kisheria na anashangaa kwanini mwenyekiti wa
serikali ya kijiji halipwi mshahara wakati ana majukumu mazito ya kiserikali.
Diwani huyo pia
amefungua mfuko wa kukopeshana kwa gharama nafuu katika vijiji vya kata yake
ambao unamwezesha mwananchi yeyote kukopa fedha na kurudisha ili kutatua
changamoto mbalimbali zinazowakabili wananchi wa kata yake.
Kwa mujibu wa
Magendo,kata ya Linga ina watu karibu 5000 hivi sasa na kwamba kata hiyo
inakabiliwa na changamoto mbalimbali zikiwemo ukosefu wa kituo cha afya hali
inayosababisha watu kusafiri zaidi ya kilometa 30 hadi 40 kufuata huduma za
afya ambapo waathirika wakubwa ni wanawake wajawazito na watoto.
Changamoto nyingine ni
ukosefu wa ofisi mbalimbali ikiwemo ofisi ya afisa mtendaji wa kata,ukosefu wa
shule ya msingi katika kijiji cha Ngingama,ukosefu wa chumba za kuhifadhia dawa
katika zahanati ya Ngingama pamoja na ukosefu wa wodi ya wajawazito katika
zahanati ya kijiji cha Ngingama.
Pamoja na changamoto
hizo diwani Magendo anaitaja miradi ya maendeleo ambayo inatekelezwa katika
vijiji vya kata hiyo kuwa ni pamoja na
ukarabati wa zahanati na ujenzi wa nyumba
za watumishi katika kijiji cha Litumbakuhamba.
“Miradi mingine ni
kilimo cha umwagiliaji katika kijiji cha Ngingama,ujenzi wa ofisi ya kijiji cha
Ngingama,kwa ujumla katika kata yangu shughuli za kiuchumi zilizopo ni
kilimo,uvuvi,ufugaji na biashara ndogo ndogo’’,alisisitiza.
Mwisho

No comments:
Post a Comment